Papa Francisko ajikabidhi chini ya ulinzi wa Bikira Maria!
Baba Mtakatifu Francisko Ijumaa, tarehe 23 Mei 2014 asubuhi na mapema, aliondoka kutoka
mjini Vatican na kwenda kusali kwenye Kanisa kuu la Bikira Maria mkuu lililoko mjini
Roma, kuomba ulinzi na tunza ya Bikira Maria kabla ya kuanza hija yake ya kichungaji
Nchi Takatifu itakayomwezesha kutembelea: Yordan, Palestina na Israeli kama sehemu
ya maadhimisho ya Jubilee ya Miaka 50 tangu Papa Paulo VI alipokutana, akazungumza
na kusali na Patriaki Anathegoras wa Yerusalemu.
Baba Mtakatifu Francisko
alipokuwa anatangaza hija hii ya kitume aliwaambia waamini waliokuwa kwenye Uwanja
wa Kanisa kuu la Mtakatifu Petro mjini Vatican kwamba, hija hii itafikia kilele chake
wakati viongozi wawakilishi wa Makanisa watakaposali kwa pamoja kwenye Kaburi Takatifu,
mwendelezo wa mchakato wa majadiliano ya kiekumene, ili wote wawe wamoja!