2014-05-23 07:31:16

Amani kwenu!


Katika dini nyingi iko desturi nzuri ya kiroho ya kufanya hija pahala patakatifu au sehemu za kihistoria za dini hiyo. Hija hiyo mara nyingi hufanyika kama moja ya kuadhimisha tukio fulani muhimu linalomhusu mtu binafsi ili kujichumia neema anayohitaji mhiji au alhaji. RealAudioMP3

Papa pia hufanya hija sehemu mbalimbali kama vile Lourdes, Fatima, Loreto, Namugongo, Nchi Takatifu, nakadhalika. Hija ya Papa haiwi kwa ajili yake binafsi tu, bali hasa ni kuchuma neema kwa ajili ya kanisa zima, pia inakuwa kwa ajili ya kuimarisha mahusiano ya kuletesha haki, amani na upendo kati ya nchi na nchi.

Mwaka huu kuna jubilei za dhahabu kadhaa za kikanisa zitokanazo na Mtaguso wa pili wa Vatican. Zaidi pia ni mwaka wa 50 tangu Papa Paulo VI alipohiji nchi ya ahadi na kuzungumza na Patriaki Anathagora wa Yerusalemu. Papa Fransis atahiji nchi ya ahadi ikiwa ni kuadhimisha jubilei ya dhahabu ya hija hiyo ya Papa Paulo VI. Katika hija hiyo, Papa atakutana na viongozi muhimu wa serikali na dini, atakutana pia na waumini wenzetu walioko huko.

Papa atazuru sehemu chache muhimu. Mosi, ataenda Bethlehemu kuzuru na kusali pahala alipozaliwa Yesu. Ataenda kuzuru na kusali kando ya mto Yordani alikobatizwa Yesu. Mwisho ataenda kuangalia chumba ambacho Yesu alikula Karamu ya Mwisho na mitume wake. Chumba hicho ni mandhali ya mwisho aliyokuwa Yesu kabla ya kuteswa na kufa kwake.

Kwa hiyo wakristu wote tunaalikwa mosi, kuiombea hija hii ya Papa, kusudi asafiri salama, aende akatuombee na kufanikisha makusudio aliyojipangia kwa faida yake, na kwa manufaa ya kanisa zima na ulimwengu kijumla, na hatimaye arudi salama, kusudi Mungu atukuzwe katika yote. Pili tunaalikwa sisi sote kutanguzana na Papa kwenda katika hija hiyo, usikose kuwepo katika msafara huo wa Baba Mtakatifu. Kutokana na msongamano wa watu na hasa kupanda gharama ya maisha, siyo wote watafanikiwa kwenda hiyo hija.

Tunaalikwa kukata tiketi ya kiroho ambayo gharama yake ni bure sanasana inategemea uhuru wako mwenyewe, na mkatishaji tiketi ni Roho Mtakatifu mwenyewe ambaye hata Yeye mwenyewe ataenda kwenye hija hiyo ya awali tangu atoke huko alipokufa Yesu Msalabani. “Akainama kichwa akaitoa Roho yake”.

Kwa watakaoenda huko kwa tiketi ya Roho Mtakatifu, mnaalikwa kusoma ramani hii au mwongozo ufuatao, utakaowasaidia kujua sehemu mbalimbali mtakazotembelea na kuzihiji pindi mnaongozana na Papa. Hizo ni sehemu muhimu ambazo kulifanyika mambo makuu na mazito yahusuyo ukombozi wetu.

Katika mwongozo huu tutajaribu kuzieleza kwa kifupi sana sehemu hizo kijiografia na kiteolojia. Tutaona pia matukio yaliyotokea sehemu hizo, yahusuhuyo Yesu au mitume wake na sisi tunaweza kupata fundisho gani toka sehemu hiyo. Hebu twendeni kwanza Betlehemu alikozaliwa Yesu tuhimizane kwenda huko kwa maneno ya Wachungaji waliokuwa wanahimizana kwenda huko baada ya kupata taarifa toka kwa malaika: “Twendeni mpaka Betlehemu, tukashuhudie tukio hilo alilotujulisha Bwana.” (Lk 2:15).

“TWENDENI MPAKA BETLEHEMU”
Lk 2:15

Jina hili Bethlehemu linatokana na maneno mawili ya Kiebrania, Bet ni nyumba na Lehem (lexem) ni mkate, kwa hiyo Beth-Lehem au bet-lexem maana yake nyumba ya mkate. Kwa lugha ya kigiriki cha zamani walitamka Bethleem. Ziko sehemu nyingi zenye nyumba ya mkate mathalani Beth-lehem-ephratah, Bethlehemjudah, lakini Bethlehemu iliyokuwa kusini karibu na Yerusalemu ndiyo iliyokuwa inaitwa Bethlehemu katika mji wa Daudi. Hapo ndipo alipozaliwa Yesu. Ni mji ambao toka zamani wameishi wakristu wengi, lakini sasa wanaishi pia watu wa dini mchanganyiko. Sehemu hii wanafurika wahaji na watalii wengi sana hususani wakati wa Kipindi cha Noeli.

Kisa cha kujulikana Betlehemu kilianza na safari ya Yosefu na Maria aliyekuwa na baraka tumboni. Walienda huko kwa ajili ya senza. Katika pilikapilika za kutafuta mahali pa kulala mama akajifungua mtoto wake hapo Betlehemu mji wa Daudi (Lk. 2:4). Baada ya kuzaliwa, mtoto huyo akaviringishwa nguo za mtoto mchanga na kulazwa kwenye hori la kulishilia wanyama. Hii ndiyo alama ambayo malaika waliwapa maelezo wachungaji na kuwaagiza waende huko kumwona mtoto. Malaika wakawaambia wachungaji: “Leo katika mji wa Daudi amezaliwa kwa ajili yenu, Mwokozi, ndiye Kristu Bwana. Na hii ndiyo ishara kwenu; mtamkuta mtoto mchanga amevikwa nguo za kitoto, amelala katika hoi ya kulia ng’ombe.”

Kumbe yawezekana malaika walikuwa wa kwanza kufika hapo Betlehemu na kushuhudia mambo yalivyo kabla ya kwenda kuwahabarisha wachungaji. Tunaambiwa pia kwamba mara tu baada ya malaika kuondoka, wachungaji nao wakaambizana wenyewe, Jamani tusiilazie damu taarifa hii ya malaika: “Twendeni mpaka Betlehemu, tukashuhudie tukio hilo alilotujulisha Bwana.” (Lk. 2:15). Baada ya kumwona mtoto wakaanza nao wakaanza kutawanya habari: “Walipomwona (mtoto Yesu) wakatoa habari waliyoambiwa juu ya huyo mtoto. Halafu wote waliosikia wakastaajabu kwa hayo waliyoambiwa na wachungaji.” (Lk 2:27).

Malaika walipoona utukufu umetua Bethlehemu, hawakuuacha utulie tu pale pangoni, bali wakaondoka kwenda kuutangaza kwa wachungaji. Kwa hiyo utukufu haukuhusu pango ila unawahusu wachungaji wanaowakilisha wanyonge wote. Wachungaji ndiyo wanaodhihirisha utukufu wa Mungu. Mungu anajidhihirisha na kutukuzwa pale tu ambapo wanyonge, fukara wanapofurahi. Huo ni utukufu wa Mungu.

Wachungaji wanafurahi kwa sababu kutokana na hali halisi ya unyonge wao, walijisikia kama watu waliolaaniwa, kwa hiyo hawakutegemea kabisa kupata mawasiliano na Mungu.

Kumbe, amezaliwa mchungaji mwenzao, anayejua unyonge wao. Hawakujiamini wenyewe, na mara moja wakaanza kushauriana wenyewe na kuchukua maamuzi ya kwenda kushuhudia na baadaye kutoa ushuhuda. “Twendeni mpaka Betlehemu, tukashuhudie tukio hilo alilotujulisha Bwana.” Wanaenda haraka, kushuhudia utukufu wa Mungu, ambao ni kutaka watu wapate furaha haraka.

Kwetu sisi tungetegemea kusikia mambo ya ajabu zaidi au hata kusikia muujiza. Hakuna maelekezo zaidi, ni kama vile amezaliwa mtoto wa kawaida. Maisha ya kawaida yanaendelea. Yesu kuwa Mungu hakutegemei muujiza wa pekee, bali yeye mwenyewe jinsi alivyo. Yeye ni kama sisi, Mungu amekuwa mwenzetu. Anayemtegemea Mungu wa kufanya miujiza, ujue mungu aina hiyo ni mungu wa kipagani.

Wachungaji wanaenda Betlehemu na wanamwona mtoto aliyeviringishwa nguo. Hiyo ndiyo picha mpya ya Mungu anayejidhihirisha kwa binadamu. Watoto waliviringishwa nguo ili kuwakinga na baridi lakini pia inayo maana ya kidini. Mtoto ni safi, hivi huwezi kumshika tu kwa mikono, lakini kuna maana pia muhimu ya kiroho, hasa mwinjili anaposisitiza jinsi mtoto alivyoviringishwa nguo, hoja kubwa ni kusudi mtoto huyo aweze kuguswa, kushikwashikwa na kubebwa na watu wote.

Aidha imeandikwa mara tatu kuwa aliwekwa katika hori la kulishia chakula wanyama (ng’ombe). Kwa hiyo msisitizo huo unahusu chakula. Mtoto aliviringishwa nguo, kama vile mkate unavyoviringishwa karatasi au majani na kuwekwa kwenye nyumba ya mkate (Bethlehemu). Kwamba Yesu anadhihirishwa hapa kama mkate yaani chakula. Malaika wanawaelekeza wachungaji kwenda kwenye nyumba ya mkate (bethlehemu) huko watauona mkate umeviringishwa.

“Na hii ndiyo ishara kwenu; mtamkuta mtoto mchanga amevikwa nguo za kitoto, amelala katika hoi ya kulia ng’ombe.”Yesu aliishi na kuhitimisha historia ya maisha yake hapa duniani akijionesha mwenyewe daima kuwa ni mkate utokao mbinguni. Maisha yake yote akayatolea hadi chembe ya mwisho ya mkate. “Twendeni mpaka Betlehemu, tukashuhudie tukio hilo alilotujulisha Bwana.”

Wachungaji wanapofika pangoni wakamwona Maria, Yosefu na mtoto mchanga amelala horini. Hawaoni cha pekee zaidi. Kisha wakatoa taarifa juu ya kile walichoambiwa juu ya huyo mtoto. “Walipomwona (mtoto Yesu) wakatoa habari waliyoambiwa juu ya huyo mtoto. Halafu wote waliosikia wakastaajabu kwa hayo waliyoambiwa na wachungaji.” Nadhani watu wote walishangazwa na taarifa hizo kwani ni Mungu aina gani anayeweza kuwatokea watu wanyonge kama wachungaji. Kama ndivyo basi hayo ni maajabu.

Tunaambiwa jambo jingine lililotokea pale Bethlehemu ni kuwa Maria akayaweka maneno hayo yote, akiyafikiri moyoni mwake. Neno kufikiri, siyo tafsiri sahihi, kwa kigiriki “sinmbalus” inamanisha kuweka mambo pamoja na kutafakari, hasa kule ambako mmoja unapoona mambo lakini unashindwa kuyaelewa. Maria anatulia, anaangalia, anaunganisha mambo anaweka pamoja mambo yanayomtukia. Atakuja kufahamu atakapokuwa amesimama chini ya Msalaba.

Wachungaji wanaondoka wakimshukuru na kumsifu Mungu – wameyaona maisha mapya. Wamemwona Mungu aliyejifanya binadamu na kulingana na watu. Wamemwona Mungu anayejiacha kushikwashikwa na watu wenye mikono michafu, watu wanaonuka, yaani wanyonge, maskini, wazee, wenye dhambi, walalahoi. Watu hawa wanyonge wameona na wanafurahi, wanamshukuru na kumsifu Mungu, kisha wanamshuhudia. Kumbe watu hawa wanyonge tu ndiyo wanaoweza kutambua na kushabikia sera hii kubwa ya Mungu kujifanya mtu. Ni watu kama hawa ndiyo wanaoweza kuwa na furaha, na kusifu na kumshukuru Mungu. Kwa wataalamu, wakuu, matajiri sera hii haiingii akili na mioyoni mwao.

Ni muhimu hata kwetu kwamba badala ya kujihoji na kufikri nini tufanye nini katika maisha, baada ya kumwona Kristu tubaki tu kufurahi. Tumeona tendo kuu la upendo alilotufanyia Mungu. Huo ndiyo mwanzo wa uchumba kati ya Mungu na binadamu, kati ya Yesu na Kanisa lake. Sisi tunafunganishwa na Yesu katika upendo. Ndiyo mwanzo wa maisha ya upendo na ya furaha. Wanaopendana daima wanashika simu mkononi wakisubiri ”message au kupib”, au kuitwa na mpendwa wao ili kuongeana.

Sisi tukitaka kugundua utukufu na upendo huo wa Mungu tuanza Bethlehemu, na kuendelea mbele hadi kwenye majitoleo kamili ya Yesu kule Kalvari. Kwa hiyo ndugu zangu “twendeni na Papa mpaka Betlehemu” tukirudi toka huko tuwapagawaze watu kwa tutakayoyaona. Hebu sasa tutoke Bethlehemu kuongozane na Papa hadi mto Yordani.

“YESU ALIRUDI KUTOKA GALILAYA MPAKA YORDANI KWA YOHANE ILI ABATIZWE”
Mt 3: 13

Baada ya kuzaliwa, kukimbilia Misri na kurudi toka huko, Yesu akaenda na wazazi wake kukaa Galilaya (nyumbani kwake) kwa miaka hii 33. Kabla ya kuanza utume rasmi Yesu anaenda Yordani kubatizwa na Yohane. Baada ya kubatizwa anaenda Kafarnaum na huko ndiko anaanza kazi ya kuhubiri. Ebu tuangalie pahali hapa alipobatizwa Yesu. Kwa kawaida, Yohane mbatizaji alikuwa upande wa mashariki, ng’ambo ya mto Yordani (Galilaya ya Upagani). Huko akawabatiza watu na kuwataka wauvuke tena mto Yordani na kuingia Magharibi yaani nchi ya ahadi. Akawasadikisha watu kwamba sehemu hiyo ya ubatizo ilikuwa ni sehemu halisi ambayo Musa angewaingiza watu katika nchi ya ahadi, walipofika toka utumwani Misri. Kwa hiyo, wale wote waliojidhani kwamba wameingia nchi ya ahadi kumbe walikuwa bado hawajakuingia kidhati.

Kwa hiyo, Yohane akawaita watu toka Yudea warudi tena ng’ambo ya Yordani ili wabatizwe upya, na kuingia nchi ya ahadi kama ilivyokuwa walipotoka Misri. Watu wakafika pahala hapo palipokuwa opanaitwa kwa kiyahudi Bethabàra maana yake ni pahala pa kukatisha, pahala pa kusimama na kuangalia kwa mbali au nyumba ya Bwana. Yaonekana kwamba pahala alisimama Musa juu ya mlima Nebo na kutafakari nchi ya ahadi na kuona ni pahala gani ambapo angewaingiza wayahudi katika nchi ya ahadi. Kwa bahati mbaya yeye mwenyewe hakuingia, badala yake Yoshua ndiye aliyeliingiza taifa katika nchi ya ahadi.

Bethbara iko karibu sana na ziwa la mauti. Yesu anavuka mto na kuingia nchi Takatifu kuanza kufanya kazi ya kuhubiri na hatimaye kwenda kuteswa na kufa na kufufuka. Maelezo ya kiteolojia ya pahala hapa, kwamba yabidi kujiruhusu kuongozwa na Yesu toka nchi ya utumwa wa dhambi na kuingia katika nchi ya uhuru kamili wa kiroho.

Kabla ya kubatizwa, Yesu alibadilishana kauli kidogo na Yohane aliyekuwa anakataa. Kwa hoja kwamba kumbatiza huko kungeonesha kuwa Yesu ni mdhambi aliye mbali na Mungu. Yesu anasema: “Kubali hivi sasa, kwa kuwa ndivyo itupasavyo kuitimiza haki yote.” Hapa Yesu anataka kumwambia Yohane kuwa anayo picha tofauti ya haki yaani, haki anayoijua Yohane ni tofauti na haki ile ya Yesu.

Haki ya Mungu anayotaka kuiingiza Yesu duniani ni ile inayowakomboa na kuwapenda watu wote. Yohane anakubali na kumfanya Yesu avuke mto kwenda nchi ya ahadi yaani nchi ya uhuru. Kuingia huko kwa Yesu katika nchi ya Ahadi (Galilaya) ni kama kule kwa kutoka Misri alikokimbili. Sasa inaamana ya kuingia tena katika nchi ya Misri ya maisha yetu, yaani nchi ya utumwa wakaao Farao wanaotukandamiza na kunuonea. Sasa mkombozi anatujia na kutukomboa. Yesu ni Musa mpya.

Siku ile ya ubatizo wa Yesu pale Yordani kuna vituko vitatu vinavyoweza kutufundisha. Mosi, tunaambiwa kwamba mara tu baada ya kubatizwa, Yesu anapotoka majini anga linafunguka. Maelezo yake ni ya kihistoria ya mahusiano ya Mungu na binadamu. Kwamba, hapo mwanzo karibu katika karne kama tatu hivi, Mungu alikuwa anaongea na watu kwa njia ya manabii aliokuwa anawatuma kwao. Baadaye, akaacha kutuma manabii kwa sababu watu hawakuwa tena wanawasikiliza.

Mungu akafunga mbingu zake zilizokuwa saba. Watu wakabaki wanateseka, wakalalamika kwamba hatuna tena nabii, itakuwaje, tutatambuaje mawazo ya Mungu kama hakuna nabii? Unaona sasa kwa mara nyingine Yesu anapoibuka toka majini, anga linafunguka. Milango ya mbingu zote saba inafunguka.“Bwana ulikuwa na haki ya kutukasirikia, maana tulitenda dhambi; Lakini sasa, Ee Bwana, wewe u baba yetu; sisi tu udongo, nawe u mfinyanzi wetu, sisi sote ni kazi ya mikono yako. Ukifungua mbingu tutaokoka”. (Isaya 64). Kwa ujio wa Yesu, hatuhitaji tena nabii kwani tunaye Mungu hapahapa “Emmanueli”.

Pili, tunasikia kwamba Roho ya Mungu akamshukia Yesu kama njiwa. Njiwa huyo anatukumbusha Agano la Kale, baada ya tufani kuu, alitumwa njiwa kuangalia gharika kuu, baadaye anarudi akiwa na tawi la mzeituni mdomoni. Njiwa ni alama ya wema, uzuri, unyofu. Ndivyo Yesu anavyofika. Baada ya Tufani, Mungu anasema, sitaharibu tena nchi. Hakutakuwa tena tufani itakayoharibu nchi, bali atatuma roho aliye alama ya uzima mpya. Ndivyo sasa Yesu anapoibuka toka majini roho anaingia duniani.

Tatu, sauti ikasikika toka mbinguni. Sauti inayomtambua Yesu. Sauti inatambua kitendo kinachofanyika. Yaani ufunuo au epifania ya Mungu. Sasa ni wakati rasmi Mungu anapoanza shughuli yake mpya. Kwa hiyo anapoibuka toka majini, Mungu anatamtambua kuwa ndiye mwanae mpenzi. Mwana anafanana na wazazi wake katika sifa na thamani zote muhimu, hata namna ya kuongea na kutenda mambo. Sisi tumwangalie mwanae anayefanana na Mungu, nasi tutakuwa na roho hiyohiyo kwani tunafanana na Baba. Wote ni watoto wa Mungu, Yeye ni mwanae wa pekee mpendwa kwani ameleta habari njema ya upendo, na ya haki kwa watu wote.

Tujikubali kwamba tuko katika nchi ya utumwa mwa dhambi, tugeuke kwa kuvuka Yordani pamoja na Yesu, tutaibuka na roho wa Bwana, aliye roho wa unyenyekevu, upole, wema, upendo na haki. Roho atakayetupa nguvu ya kushinda majaribu ya maisha magumu ya humu jangwani (ulimwenguni). Kisha tutaibuka kidedea katika maisha mapya pamoja na Kristu Mfufuka. Yesu anatuagiza kutenda mambo yote kwa kufuata mfano wa maisha yake. Ndivyo alivyowaagiza mitume wake siku ya karamu ya mwisho, “fanyeni hivi kwa kunikumbuka mimi.” Sasa twende tukakiangalie chumba ambacho Yesu alifanya sherehe mara ya mwisho hapa duniani na kuyatamka maneno hayo.

“FANYENI HIVI KWA UKUMBUSHO WANGU.”
Lk 22:19

Karibu Wainjili wote wanatupatia maelezo ya karamu ya mwisho. Katika chumba kilicho juu. Wainjili wanasema kwamba karamu hiyo ilikuwa ya Agano Jipya na la milele. Katika mazingira hayohayo ya kula Yesu akawaosha miguu wafuasi wake. Kila mwenjili anajitahidi kutoa fundisho la pekee kadiri anavyoona yeye. Hapa sisi tufuate maelezo ya mwinjili Luka. Sote tunafahamu kilichotokea siku ile ya karamu ya mwisho. Maneno ambayo Luka anayoyatumia na ambayo yabidi kuyafanyia tafakuri ni yake tunayoyasikia katika kila misa: “fanyeni hivi kwa ukumbusho wangu.” Ni mwinjili Luka peke yake anayesema maneno hayo.

Lengo la Yesu lilikuwa ni kuwaalika wafuasi wake wote kumkumbuka Yeye, yaani daima kurudia kufanya kitendo hicho. Lakini zaidi pia aliwataka wamege mkate na kula ikiwa kama alama ya msingi katika imani yetu. Tendo la kumega mkate ni ufupisho wa maisha yake yote toka kuzaliwa hadi kufa kwake. “Mimi nimejifanya chakula ili kuyalisha maisha.” Ni kama vile angekuwa Bethlehemu inayotembea (mobile bakery). Luka anataka kutuambia kuwa mnapokuwa katika karamu hii, au mnapokula chakula hiki, mnafanya uchaguzi kama wangu wa kujitoa na kujitolea. Huo ni mwaliko wa kuwa kama Kristu, wa kuwa mkate na kujigawa kwa wengine. Kwa hiyo haitaeleweka kabisa kumwona mkristu baada ya kuadhimisha ekaristi, anashindwa kusaidia wengine.

Hali halisi nyingine inayoonekana humo chumbani, wakati wa sherehe hiyo kuliibuka mabishano mazito hasahasa tungeweza kuyaita mahojiano makali kati ya mitume. Kisa walikuwa wanabishana juu ya ukuu, juu ya kuwa na heshima na cheo kati yao “ni nani anayehesabiwa kuwa mkuubwa.” Yesu akawaambia: “Wakuu wa mataifa huwatawala, na wenye mamlaka juu yao huitwa Wenye fadhili; lakini kwenu ninyi sivyo; bali aliye mkubwa kwenu na awe kama aliye mdogo; na mwenye kuongoza kama yule atumikaye. Mimi niko kati yenu kama atumikaye.” Haya tena ni maneno yanayoletwa na Luka peke yake wakati huu wa mlo. Ni maneno kwa ajili ya kila mtu hasahasa yule anayejiita mkristu. Hayo ndiyo mambo yanayoharibu jumuia za kiristu siku za leo. Kazi ya mtu aliyeshiba ni kutafuta cheo.

Mahojiano hayo ya mitume hayakuishia kwao tu. Mabishano hayo yameletwa hapa kuonesha kuwa yanaweza kumpata kila mmoja katika maisha yake. Hasa kuhusu kujihoji wewe mwenyewe kuhusu kuchagua mambo. Hali kadhalika Yesu Kristu katika maisha yake hapa duniani alikabiliwa na changamoto hii ya kujihoji nafsini mwake. Mahojiano hayo ya Yesu tutayaona baada ya karamu ya mwisho akiwa kwenye mlima wa Mizeituni.

Tunaambiwa kuwa alipatwa na uchungu sana ambao katika Injili ya Kiswahili wanafasiri kuwa ni dhiki. “Yesu akatoka akaenda mpaka mlima wa Mizeituni kama ilivyokuwa desturi yake; ...akajitenga na mitume wake… huko akasali... kwa vile alikuwa katika dhiki... hari yake ikawa kama matone ya damu yakidondoka nchi.” Alikuwa katika katika dhidi au tuseme alikuwa na hali mbaya sana. Yaani ni kama hali ile anayokuwa nayo mtu kabla ya kufa. Neno hili uchungu pia limetokea katika injili ya Luka peke yake, kwa kiingereza ni ”Agony”. Maana halisi ya neno hilo agoni lamaanisha mapambano, mashindano au mahojiano makali. Hasa mashindano kama yale ya wanariadha. Yesu aliingia katika mashindano kama hayo.

Toka mwanzo wa maisha yake, Yesu ilimbidi aingie katika mapambano na mashindano na nguvu za shetani. Mapambano hayo hayakwisha katika vishawishi, yaani pale shetani alipomjia Yesu jangwani mara tu baada ya kubatizwa. La hasha, baada ya vishawishi vile tunasikia kuwa shetani alimwacha Yesu kwa muda. “Basi alipomaliza kila jaribu, Ibilisi akamwacha akaenda zake kwa muda.” (Lk. 4:13). Shetani anakuja tena akijua kwamba hapa sasa ni lala salama! Hapa kuna mapambano makali ya roho yanayomdai Yesu kuwa mwaminifu na inabidi kuyashinda. Yesu anashinda! Kuonesha kwamba hayo yalikuwa ni mashindano makali, Yesu anatoka jasho, hilo kama vile jasho linalomtoka mwanariadha wakati wa mashindano. Kwa hiyo agoni siyo uchungu bali ni mapambano, kuvutana, ukinzani, ugomvi ndani ya mtu. Mapigano yaliyoko ndani ya mtu.

Katika mapambano hayo Yesu anajiandaa kwa kujitenga na kusali. “Mwenyewe akajitenga nao kama kiasi cha kutupa jiwe, akapiga magoti akaomba.” Anajiweka katika mahusiano na Mungu ili kuweza kuiona mipango ya Mungu. Anajiweka katika mahusiano na Mungu, ili kujua Mungu anao mpango gani kwa ajili yake. Yesu alisali sana na akawahimiza mitume wake kukesha na kusali. “Alipofika mahali pake aliwaambia: ‘ombeni kwamba msiingie majaribuni. Ondokeni, mkaombe msije mkaingia majaribuni.”

Sala inamsaidia Yesu. Kisha wanafika malaika kumliwaza. Hiyo ni alama ya kuwa na mawazo ya ndani ya Mungu. Endapo alifikiria kutoroka maisha, kutoroka mateso sasa anaimarika, na kuhiari kuurekebisha ulimwengu. Kwa hiyo ili kushinda mapambano ya ndani ya mtu, yabidi kusali sana. Kuunganisha mipango yako na mipango ya Mwenyewe Mungu.
Hatima
Ndugu zangu wahiji au ma-alhaji, nimejaribu kuwapatieni picha ndogo sana ya sehemu atakazoenda kuhiji Papa, ili uweze kutanguzana naye kiroho. Sehemu hizo ni ile aliyozaliwa Yesu hapa duniani, nikitumia kauli mbiu “Twendeni mpaka Betlehemu”, kisha Yordni sehemu aliyobatizwa, tungeweza kusema aliyosimikwa rasmi kama nabii mtangazaji wa habari njema baada ya kushinda majaribu jangwani. Halafu tumeona chumba cha mwisho alichoweka karamu ya mwisho na kuwaagiza mitume wake “Fanyezi hivi kwa ukumbusho wangu.” Sehemu hizi tatu, ni kama mzunguko wa maisha ya binadamu hapa duniani, ambayo ni kuzaliwa, kazi na kufa.

Tofauti ya mzunguko wa maisha yetu na ya Yesu ni kwamba, Yesu anaanza maisha yake (kama mkate ulioshuka toka mbinguni) akishuhudiwa na Mungu Baba kwa njia ya malaika, anaanza kazi yake akishuhudiwa na Mungu Baba (kwa sauti) na Roho Mtakifu (kwa mfano wa njiwa). Anakufa na kufufuka kisha anaendelea kukaa pamoja nasi Fanyeni hivi kwa ukumbusho wangu.” Yaani sasa imebaki kuwa kazi kwetu kuishi maisha kama alivyoishi Yesu.

Ikiwa kama nyongeza katika ramani hii ya hija, ningependa kuwadokezea mambo mawili, mosi, nadhani umewahi kuusikia msemo unaosema kwamba, Nchi Takatifu ni Injili ya Tano. Ningependa kukuhakikishia kwamba msemo huo ni wa kweli kabisa. Ukienda na kuona nchi ya kibiblia kwa macho yako, utaweza kushabikia vizuri zaidi Maandiko Matakatifu. Jiografia ya nchi itakuonesha wapi historia ya ukombozi ilitokea katika Biblia. Mang’amuzi utakayopata yatakupa picha ya hadithi unazozisoma katika Biblia.

Pili, utasikia watu wanaamkiana wakilitumia amkio lilelile alilolitumia sana Yesu alipokuwa anawatokea mitume wake baada ya ufufuko. “Amani kwenu”. Amkio hilo linatumika hadi leo katika maamkio ya kawaida kwa lugha ya kiyahudi shalom. Anza kufanya mazoezi ya kulitamka neno hilo, na cha muhimu zaidi ni kuliishi neno hilo Amani katika maisha yako yote.
Mwisho, ni kwamba Nchi ya Ahadi ndiyo aliyoishi Yesu aliyeitwa na Yohane Mbatizaji “Huyu ndiye Mwanakondoo wa Mungu aondoaye dhambi za dunia”. Huyo Mwanakondoo anamgeukia kila mmoja wetu na kumwalika kukaa naye kama alivyowaalika wale wanafunzi wawili waliokuwa wanamfuata akawauliza: “Mnatafuta nini?” Wakamwambia, “Rabi (maana yake Mwalimu), unakaa wapi?” Akawaambia, “Njoni, nanyi mtaona.” Wakaenda, wakaona akaapo, wakakaa kwake siku ile.” (Yoh. 1:37-39) Tunaalikwa sote kufanya hija ndani ya mioyo yetu ambayo ni makao ya Roho Mtakatifu na tukae na Yesu daima.
Imeandaliwa na
Padre Alcuin Nyirenda, OSB.








All the contents on this site are copyrighted ©.