Miaka 50 ya kuzaliwa! Zawadi Kituo cha Televisheni!
Bwana Robert Olagunju kutoka Nigeria kama sehemu ya maadhimisho ya Miaka 50 tangu
kuzaliwa kwake ameamua kuanzisha kituo cha Luninga kitakachojulikana kama "Lumen Christi",
yaani "Mwanga wa Kristo" kitakachorusha matangazo yake ndani na nje ya Nigeria bila
malipo.
Matangazo haya yataanza kutolewa kwa lugha ya Kiingereza na maandishi
kwenye lugha ya Kifaransa. Mikakati iko mbioni kuhakikisha kwamba, matangazo haya
pia yanapatikana kwa njia ya maandishi kwa lugha ya Kihispania, Kireno, Kiswahili
na Kipidgin.
Lengo la kuanzisha kituo hiki chenye mwelekeo wa Uinjilishaji
Mpya Barani Afrika ni kumshukuru Mungu kwa kumwezesha kufikisha miaka 50 tangu alipozaliwa
na kama alama ya shukrani, basi anataka kuanzisha kituo cha Televisheni ili kusaidia
mchakato wa Uinjilishaji Barani Afrika. Bwana Olagunju anatambua sadaka kubwa iliyoko
mbele yake na anasema anataka kuivalia njuga, ili kutekeleza ndoto yake.
Kituo
hiki kitarusha matangazo yake kwa kipindi cha masaa 24 kwa siku. Anaomba ushirikiano
na mshikamano kutoka kwa waamini na viongozi wa Kanisa ili kutimiza ndoto yake kwa
ajili ya ustawi na maendeleo ya Kanisa Barani Afrika.