2014-05-21 07:02:05

Wanawake jitokezeni kimasomaso kujenga Kanisa na Jamii!


Wajumbe wa Baraza la Makanisa Ulimwenguni, hivi karibuni wameshiriki katika mkutano mkuu wa Baraza la Wanawake wa Kimethodist, kwa kuwataka Wanawake Wakristo kushiriki kikamilifu katika ujenzi wa Makanisa na Jamii. Changamoto hii imetolewa na Hillary Clinton, aliyekuwa Katibu mkuu wa Nchi wa Marekani wakati alipokuwa anachangia hoja katika mkutano mkuu wa wanawake wa Kimethodisti. RealAudioMP3

Anasema, wanawake wanapaswa kujifunga kibwebwe ili kupambana na changamoto mbali mbali zinazoendelea kujitokeza katika ulimwengu wa utandawazi, ambako wanawake na wasichana wanaendelea kunyanyasika; kuna ukosefu mkubwa wa usawa kati ya watu, utu na heshima ya binadamu vinadhalilishwa kutokana na biashara haramu ya binadamu pamoja na ukosefu huduma makini ya afya kwa mama na mtoto.

Mkutano huu uliwajumuisha wanawake 7, 000 walioshiriki kwenye kituo cha kimataifa cha mikutano huko Kentucky, Marekani. Baraza la Wanawake wa Kimethodisti limekuwa mstari wa mbele katika kuwajengea wanawake uwezo wa kushiriki katika maendeleo ya Kanisa na Jamii inayowazunguka tangu ilipoundwa kunako mwaka 1953.

Katika kipindi cha miaka sitini, Baraza la Makanisa Ulimwenguni linasema bado kuna umuhimu wa kuwajengea wanawake uwezo ili waweze kuwa na vyama vyenye nguvu vitakavyosaidia kuharakisha ujenzi wa misingi ya haki, amani na usawa kati ya watu. Wanawake waimarishwe kiroho ili waweze kuwa na utashi wa kufanya maamuzi makubwa katika maisha yao. Mkutano mkuu wa wanawake wa Kimethodisti ulikuwa ni fursa ya kusali, kuabudu na kushirikishana mang’amuzi mbali mbali ya maisha ya kijamii.

Wajumbe wameangalia athari za utumwa mamboleo kutokana na ushuhuda uliotolewa na wahanga wa biashara haramu ya binadamu na nyanyaso za watoto wadogo, wanaofanyishwa kazi za suluba kwa ujira kidogo, lakini madhara yake ni makubwa katika makuzi na maendeleo ya watoto hawa kwa sasa na kwa siku za usoni. Bado kuna makundi makubwa ya wanawake na watoto yanayoendelea kutumbukizwa katika biashara ya ngono ya kimataifa. Hawa ni watu wanaopaswa kusaidiwa ili kutambua utu na heshima yao kama binadamu walioumbwa kwa sura na mfano wa Mungu.

Upendo kwa Mungu na jirani ndiyo urithi mkubwa ambao wanawake wanaweza kusaidia kuchangia katika malezi na majiundo ya watoto wao. Wanawake waoneshe ujasiri kwa kuwashinikiza wakuu wa Jumuiya ya Kimataifa kutekeleza sera na mikakati ya Kimataifa inayopania kudbiti uchafuzi wa mazingira, kwani madhara yake ni makubwa mno katika uso wa dunia.

Ni jukumu la wanawake Wakristo kusimama kidete kulinda na kutetea zawadi ya uhai tangu pale mtoto anapotungwa mimba tumboni mwa mama yake hadi mauti yanapomfika kadiri ya mpango wa Mungu, dhidi ya utamaduni wa kifo. Wanawake wajengewe uwezo wa kupambana na changamoto zinazoendelea kuibuka katika medani mbali mbali za maisha, kwa kuwapatia elimu makini na uwezo wa kiuchumi pamoja na kuwashirikisha katika vikao vinavyotoa maamuzi.

Wanawake wamepongezwa kwa kuendelea kutunza familia ambazo zimeathirika kutokana na athari za ugonjwa wa Ukimwi. Wajumbe, kimsingi wanasema kuna haja kwa Jumuiya ya Kimataifa kujenga uchumi unaojikita katika haki, mshikamano na udugu.








All the contents on this site are copyrighted ©.