2014-05-21 16:03:02

Paji la elimu liwasaidie kumwona Mungu katika yote!


Baba Mtakatifu Francisko katika Katekesi zake anazotoa kila Jumatano ametafakari kuhusu Mapaji Saba ya Roho Mtakatifu, yaani: Hekima, Akili, Ushauri na Nguvu, Elimu, Ibada na Uchaji wa Mungu. Jumatano tarehe 21 Mei 2014, Baba Mtakatifu Francisko ametafakari kuhusu paji la elimu zawadi inayomwezesha mwamini kwa njia ya kazi ya uumbaji, kupokea ukuu na upendo wa Mungu na mahusiano yake ya dhati na kila binadamu na kutenda kadiri ya mapenzi yake.

Baba Mtakatifu anasema, kwa njia hii, watu wanaweza kuona: uzuri, ulinganifu na wema wa viumbe vyote vinavyomzunguka mwanadamu kwa kutumia jicho la Mwenyezi Mungu ambaye ndiye Muumbaji wa vyote. Kama inavyojionesha katika maisha ya Mtakatifu Francisko wa Assis na kwa watakatifu wengi, Paji la Elimu linamwezesha mwamini kufikia kiwango cha hali ya juu kabisa cha tafakari kuhusu asili ya dunia na hatimaye kumwimbia Mwenyezi Mungu utenzi wa furaha.

Mwelekeo unaotolewa na paji hili la maisha ya kiroho anasema Baba Mtakatifu, linawawezesha watu kuheshimu zawadi ya uumbaji na kutawala rasilimali ya dunia kwa hekima na uwajibaki zaidi kwa ajili ya mafao ya familia yote ya binadamu. Huu ni mwaliko wa kuwa na mwono mpana zaidi si tu katika watu na vitu vya dunia hii na kusahau kwamba katika utaratibu wake, thamani na uzuri wake unamwelekea Mwenyezi Mungu, kama kiini na hitimisho lake.

Baba Mtakatifu Francisko anawaalika waamini na watu wote wenye mapenzi mema kumwomba Roho Mtakatifu ili awasaidie kukuza ndani mwao Paji la Elimu, ili liweze kuwasaidia kuona upendo wa Mungu unaoiongoza dunia na kujibu kwa moyo wa shukrani na sifa kwa Mwenyezi Mungu mwingi wa wema na upendo usiokuwa na mipaka.

Baba Mtakatifu ametambua uwepo wa mahujaji kutoka Jimbo Katoliki la Pointe Noire, Congo Brazaville na Afrika ya Kusini. Anawataka waamini kushuhudia upendo wa Mungu kwa kuumwilisha katika matendo ya huruma kwa jirani zao. Waamini wawe na ujasiri wa kuona chapa ya uwepo wa Mungu kwa kila kiumbe chake, ili kutambua utupu wa mtu na hatimaye kuungama ukuu wa Mungu.

Mwezi Mei uwawezeshe waamini kuimarisha imani yao pamoja na kuendelea kumtumainia Bikira Maria. Anawaomba kumwombea ili aweze kuifanikisha hija yake ya kichungaji huko Nchi Takatifu. Anawaomba waamini kudumisha Ibada ya Kuabudu Ekaristi Takatifu, kwa kutoa kipaumbele cha kwanza kwa uwepo wa Mungu katika hija ya maisha yao ya kila siku.







All the contents on this site are copyrighted ©.