Kwa mujibu wa habari katika gazeti la Nipashe, mtu mmoja amefariki dunia katika Hospitali
ya Mwananyamala jijini Dar es Salaam kwa ugonjwa wa dengue. Kiongozi wa Idara ya
Wagonjwa wa Nje (OPD) katika Hospitali ya Mwananyamala, Dk. Mrisho Lupinda,akizungumza
na waandishi wa Nipashe, juu ya kifo cha mtu huyo, ameeleza kuwa, walimpokea mgonjwa
huyu, ambaye tayari alikuwa amepata maambukizi ya dengue na kwamba hali yake ilikuwa
ni mbaya, na alifariki wakiwa katika jitihada za kumhudumia. Na kwamba, hadi Jumanne,
jumla ya wagonjwa 150 waligundulika kuwa na maambukizi ya ugonjwa wa dengue. Na ametaja
maeneo yaliyo na ambukizo kubwa kuwa ni pamoja na Tandale, Kinondoni, Mwananyamala,
Mikocheni na Masasani.
Aidha ametoa wito kwa wakazi wa maeneo hayo na mengine
kuendelea na kampeni ya kusafisha mazingira ikiwa ni pamoja na kufukia madimbwi, kufunika
vizuri vyombo vya kuhifadhia maji kama, mapipa, ndoo na kuwahi matibabu pindi zinapojitokeza
dalili za ugonjwa huo.