Serikali ya Tanzania kwa kushirikiana na Shirika la Umoja wa Mataifa linaloshughulikia
Maendeleo (UNDP) inatarajia kutoa mafunzo kwa Waandishi wa Sheria kwa lengo la kuwaongezea
uwezo wa kuandaa miswada katika lugha ya kiswahili – lugha ambayo inatumiwa na watanzania
wengi.
Naibu Waziri wa Katiba na Sheria Mhe. Angela Jasmine Kairuki amemwambia
Mkurugenzi Mkazi wa UNDP Bw. Philippe Poinsot kuwa kwa sasa Ofisi ya Mwanasheria Mkuu
wa Serikali inatekeleza mkakati wa kuandaa miswada yote inayosilishwa Bungeni katika
lugha mbili, Kiingereza na Kiswahili ili kuwawezesha wananchi wengi kuisoma.
Hata
hivyo, kwa mujibu wa Naibu Waziri Kairuki, katika kutekeleza kazi hiyo, Ofisi ya Mwanasheria
Mkuu wa Serikali kupitia Idara ya Uandishi wa Sheria inakabiliwa na changamoto kadhaa
zikiwemo uhaba wa watumishi na uwezo na hivyo kuhitaji msaada wa mafunzo.
“Kwa
sasa Ofisi ya Mwanasheria Mkuu ina kazi ya kuandaa miswada katika lugha mbili ikiwemo
Kiswahili ambayo ndiyo lugha ya taifa ambayo wananchi wengi wanaifahamu,” alisema
Bi. Kairuki katika mkutano wake na Bw. Poinsot, Jumatatu, Mei 19, 2014 Jijini Dar
es Salaam.
Mkutano huo ulifanyika katika ofisi ya Naibu Waziri Kairuki jijini
Dar es Salaam na kuhudhuriwa na Naibu Mwanasheria Mkuu wa Serikali Bw. George Masaju,
Mkurugenzi wa Mashtaka Dkt. Eliezer Mbuki Feleshi, Naibu Mwakilishi Mkazi wa UNDP
Bi. Mandisa Mashologu na maafisa wengine waandamizi wa serikali.
Akizungumza
katika mkutano huo, Bw. Masaju alisema kwa sasa Ofisi yake ina Waandishi wa Sheria
18 tu na kuwa idadi hiyo ni ndogo ikilinganishwa na majukumu ya Idara ya Uandishi
wa Sheria. “Serikali imeanzisha utaratibu huu wa kuandaa miswada katika lugha mbili
lakini tuna changamoto ya uhaba wa watumishi na hata hao waliopo, walifundishwa kuandaa
miswada katika lugha ya kiingereza na hivyo kuhitaji mafunzo,” alisema Bw. Masaju.
Akiongea
katika mkutano huo, Bw. Poinsot alisema Shirika lake limepokea maombi ya Serikali
na kuwa litayafanyia kazi kwa kushirikiana na Serikali ili hatimaye miradi hiyo itekelezwe.
“Kwetu sisi UNDP, sekta ya sheria ni muhimu sana hususan katika miradi inayolenga
kuwasaidia masikini na kujenga uwezo … ndiyo maana tupo tayari kuisadia,” alisema
kiongozi huyo wa UNDP hapa nchini.
Kwa mujibu wa Bw. Poinsot, Shirika lake
limepanga kuisaidia Serikali kupitia mradi wake unaolenga kuimarisha usimamizi wa
utoaji haki (Strengthening Administartion of Justice Project). Miradi ya awali inatarajiwa
kuanza kutekelezewa hivi karibuni kabla ya kuanza kutekelezwa kwa awamu ya pili ya
Mpango Maalum wa Shirika hilo (UNDAP II) unaotarajia kuanza kutekelezwa mwezi Januari
2015.
Maeneo mengine ambayo Serikali na UNDP zinatarajia kushirikiana ni katika
utoaji wa huduma za msaada wa kisheria; kuimarisha uwezo wa waendesha mashtaka na
watumishi wa mahakama; na kuboresha mifumo ya uendeshaji ili kupunguza mlundikano
wa kesi mahakamani.