Baraza la Kipapa la majadiliano ya kidini lina dhamana ya kujenga urafiki na amani!
Baraza la Kipapa la Majadiliano ya kidini, Jumatatu tarehe 19 Mei 2014 limeadhimisha
Jubilee ya Miaka 50 tangu lilipoanzishwa na hivyo kuendelea kuwa ni chombo cha ujenzi
wa urafiki, amani na maendeleo ya watu sehemu mbali mbali duniani.
Hii ni
sehemu ya ujumbe kutoka kwa Baba Mtakatifu Francisko aliomwandikia Kardinali Jean
Louis Tauran, Rais wa Baraza la Kipapa la Majadiliano ya kidini wakati huu Baraza
hili linapoadhimisha Jubilee ya miaka 50 tangu kuanzishwa kwake na Papa Paulo VI hapo
tarehe 19 Mei 1964 kama sehemu ya cheche za utekelezaji wa mageuzi makubwa yaliyoletwa
na Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican kwa kujikita katika majadiliano ya kina na walimwengu.
Baba
Mtakatifu anasema, Kanisa halina budi kujielekeza katika majadiliano ya kidini mahali
linapopatikana na kuishi. Kanisa lazima lijitahidi kuwa Neno na ujumbe kwa ajili ya
mchakato wa majadiliano ili kuwashirikisha watu Injili ya Furaha ya kukutana na Yesu
kwa kutambua na kuthamini utambulisho wa Kanisa.
Huu ndio ushuhuda uliooneshwa
kwa namna ya pekee na Mtakatifu Yohane Paulo wa Pili katika maisha na utume wake kwamba:
Majadiliano ya kidini na Uinjilishaji ni chanda na pete, kwani yanategemeana na yanapaswa
kuendelezwa bila kujichanganya. Hii ni kazi ya Roho Mtakatifu anayelijenga na kulidumisha
Kanisa; ni Roho Mtakatifu ambaye pia ni mdau mkuu wa Uinjilishaji anayewakarimia watu
mapaji yake pamoja na kuendeleza mchakato wa majadiliano na watu wote.
Baba
Mtakatifu Francisko anakumbusha kwamba, Kanisa Katoliki linatambua na kuthamini umuhimu
wake katika kuhamasisha urafiki na hali ya kuheshimiana kati ya waamini wa dini mbali
mbali na kwamba, Yesu kama alivyofanya kwa Wanafunzi wa Emmau, anaendelea kulisindikiza
Kanisa katika njia ya maisha ya kila mwanadamu. Ili watu kuweza kutembea kwa pamoja,
kuna haja pia ya kufahamiana na kushirikiana na watu na tamaduni mbali mbali.
Baba
Mtakatifu anasema, Kanisa litaendeleza majadiliano ya kidini, kwa njia ya ushirikiano,
matunda ambayo tayari yameanza kuonekana pamoja na kuwa na utashi na nia ya kujenga
urafiki kwa kushiriki mikutano mbali mbali ya majadiliano.
Mwishoni, Baba
Mtakatifu anaungana na Baraza la Kipapa la majadiliano ya kidini katika kuadhimisha
Miaka 50 tangu lilipoanzishwa na anatumaini kwamba, litaendelea kutekeleza dhamana
na utume wake ili kujenga amani na kusaidia mchakato wa maendeleo endelevu.