2014-05-19 08:29:11

Mjumbe wa upatanisho na msamaha Sudan ya Kusini!


Kardinali Pietro Parolin, Katibu mkuu wa Vatican, Jumamosi tarehe 17 Mei 2014 amemweka wakfu Askofu mkuu Hubertus Matheus Maria Van Megen, Balozi mpya wa Vatican nchini Sudan ya Kusini katika Ibada ya Misa Takatifu iliyofanyika kwenye Kanisa kuu la Mtakatifu Christopher, Jimboni Roermond, Ireland. Katika mahubiri yake, Kardinali Parolin amemtaka Askofu mkuu Megen kuwa ni mjumbe wa upatanisho na msamaha wa kweli miongoni mwa wananchi wa Sudan anapotekeleza dhamana yake kama Balozi wa Vatican nchini humo.

Anasema, Sudan ya Kusini inakabiliana na changamoto za vita na kinzani za kijamii. Kwa njia ya maneno, ushuhuda amini na kwa kushirikiana na Maaskofu mahalia, Askofu Megen anatumwa kuwatangazia wananchi wa Sudan ya Kusini Injili ya Upatanisho, Msamaha na Huruma ya Mungu pamoja na kuendelea kuiimarisha Jumuiya ya Waamini Sudan ya Kusini, ili iweze kuwaaminifu kwa Kristo na Kanisa lake, kwa kumwilisha ndani mwao ile Amri kuu ya Upendo kwa Mungu na jirani.

Askofu mkuu Megen amekumbushwa kwamba, atakuwa ni mhudumu wa upendo wa Yesu kwa watu wake ili kuonesha utukufu wa Mungu uliojionesha kwa namna ya pekee, kwa njia ya Yesu Kristo aliyeteswa, akafa na kufufuka kutoka katika wafu, ili kuwaimarisha waamini katika ushindi wa Msalaba dhidi ya dhambi na mauti. Awe ni uhakika wa sala na maombezi ya Baba Mtakatifu Francisko katika utekelezaji wa dhamana na majukumu yake huko Sudan ya Kusini. Awe ni mfano mwema wa kiongozi anayeandamana na Kondoo wake, akisimsikiliza kwa makini Roho Mtakatifu.

Ili kuwa kweli mchungaji mwaminifu kuna haja anasema Kardinali Parolin kukuza na karama ya toba na wongofu wa ndani, ukweli na muwazi, anayesimamia umoja na mshikamano wa Watu wa Mungu, tayari kujisadaka kwa ajili ya mafao ya wengi. Kama Balozi wa Vatican anao wajibu wa kuwaunganisha watu kiroho na kiakili, ili wote waweze kujisikia kuwa chini ya Khalifa wa Mtakatifu Petro, kwa kuwaimarisha ndugu zake katika imani, uaminifu katika Injili na utume wa Kanisa.

Kama mwakilishi wa Baba Mtakatifu nchini Sudan ya Kusini, atawajibika kupandikiza mbegu ya haki na amani kama chachu ya kukuza na kuendeleza Ufalme wa Mungu kati ya watu wa mataifa, kwa kutambua kwamba, Kanisa ni Sakramenti ya watu waliojipatanisha na kujipyaisha ndani ya Kristo. Askofu mkuu Megen amewekwa chini ya ulinzi na usimamizi wa Mtakatifu Josephina Bakhita, binti kutoka Sudan na shahidi wa neema na huruma ya Mungu inayoleta mageuzi makubwa katika maisha ya mwanadamu.

Ibada hii ya Misa Takatifu imehudhuriwa na viongozi mbali mbali wa Kanisa pamoja na Serikali ya Ireland.







All the contents on this site are copyrighted ©.