2014-05-19 06:52:02

Miaka 50 ya mchakato wa majadiliano ya kidini!


Miaka 50 imegota tangu Mtumishi wa Mungu Papa Paulo VI alipoanzisha Baraza la Kipapa la Majadiliano ya Kidini, kama sehemu ya mchakato wa majadiliano ya kidini kati ya Wakristo na waamini wa dini mbali mbali duniani, ili kulinda, kujenga na kudumisha misingi ya haki, amani, upendo na mshikamano wa dhati kati ya watu wa mataifa. RealAudioMP3

Ilikuwa ni Siku kuu ya Pentekoste, tarehe 17 Mei 1964, Papa Paulo VI alipoanzisha Sekretarieti ya majadiliano ya kidini, leo hii ni Baraza la Kipapa la Majadiliano ya kidini linaloongozwa na Kardinali Jean Louis Tauran.

Baraza hili lilikuwa na dhamana ya kuendeleza majadiliano ya kidini , ili kuwapatia watu wengi zaidi nafasi ya kusikiliza Habari Njema ya Wokovu kwa njia ya majadiliano ya kidini; dhamana iliyoboreshwa zaidi na Mtakatifu Yohane Paulo II katika maisha na utume wake. Kipindi cha miaka hamsini iliyopita, kimekuwa ni fursa muafaka kabisa ya majadiliano ya kidini yanayosimikwa katika ukweli, ushirikiano wa dhati pamoja na kutafuta njia muafaka za kuweza kujenga na kuimarisha amani na utulivu duniani.

Kardinali Jean Louis Tauran anasema, Baraza lake limebahatika kukutana na watu mbali mbali waliojitosa kwa ajili ya kukoleza majadiliano ya kidini kati ya watu. Baraza limekuwa pia ni msaada mkubwa katika kukoleza majadiliano ya kidini kwenye Makanisa mahalia. Huu ni mchango mkubwa uliotolewa na viongozi mbali mbali waliobahatika kuongoza Baraza la Kipapa la Majadiliano ya kidini tangu kuundwa kwake.

Papa Yohane XXIII wakati alipokuwa anafungua rasmi maadhimisho ya Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican alikazia umoja kati ya watu wa mataifa unaojikita katika dhana ya kuheshimiana na kuthaminiana; kwa kusimamia misingi ya ukweli na kanuni maadili; utu na heshima ya binadamu na kwamba, Kanisa liwe ni mdau mkubwa wa majadiliano ya kidini kati ya watu, kwa kuwa ni “Neno na Ujumbe”. Waamini watambue na kuheshimu tunu msingi za maisha ya kiroho, kimaadili na kiutu zinazopatikana kwenye dini nyingine duniani. Kwa pamoja waamini wa dini mbali mbali wasimame kidete kutetea uhuru wa kuabudu; wajitahidi kujenga utamaduni wa mshikamano na udugu kati ya watu, ili waweze kusaidiana kwa dhati.

Papa Yohane Paulo wa kwanza katika utumishi wake wa siku thelathini na mitatu tu, kama Khalifa wa Mtakatifu Petro, alilitaka Kanisa kushirikiana na watu wote wenye mapenzi mema, wanaosimamia haki, wa kweli na wanyofu wa moyo ili kuondokana na vita pamoja na matumizi ya nguvu yanayopelekea mateso makubwa kwa watu wasiokuwa na hatia.

Kardinali Tauran anasema, Papa Yohane Paulo II ndiye aliyeotesha mizizi ya utamaduni wa majadiliano ya kidini, akathubutu kunako tarehe 27 Oktoba 1986 kuwakutanisha viongozi wakuu wa kidini mjini Assisi, ili kusali kwa ajili ya kuombea amani duniani sanjari na maadhimisho ya Mwaka wa Amani Duniani.

Matukio ya kigaidi ya tarehe 11 Septemba 2001 yalichafua hali ya hewa kiasi kwamba, mahusiano ya kidini yakapwaya kwa kunyoosheana kidole. Papa Yohane Paulo II akatoa kanuni za kudumisha misingi ya amani duniani. Alibahatika katika hija zake za kitume kutembelea na kukutana na waamini wa dini ya Kiislam katika Misikiti yao, kama alivyofanya tarehe 6 Mei 2001 mjini Damasko.

Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto XVI aliendeleza majadiliano ya kidini na waamini wa dini mbali mbali ili kujenga na kuendeleza urafiki kati ya watu wa mataifa, daima wakitafuta mafao ya wengi. Kanisa linatambua kwamba, lina dhamana ya kutangaza Habari Njema ya Wokovu, kwa kujadiliana na kushirikiana na watu wote wenye mapenzi mema. Ulimwengu wa utandawazi ni fursa makini ya kujenga na kudumisha udugu na mshikamano kati ya watu.

Kardinali Tauran anasema, Baba Mtakatifu Francisko katika uongozi wake wa kipindi cha mwaka mmoja, amekwisha kutana na kuzungumza na makundi ya waamini wa dini mbali mbali, lengo ni kuendeleza urafiki na hali ya kuheshimiana. Tarehe 7 Septemba 2013 aliwaalika waamini wa dini mbali mbali kufunga na kusali pamoja naye kwa ajili ya kuombea amani huko Mashariki na kwa namna ya pekee nchini Syria. Waamini wa dini mbali mbali walishiriki katika utekelezaji wa wito huu.

Hivi ndivyo Mtumishi wa Mungu Paulo VI alivyojitahidi kujadiliana na Ulimwengu, Yohane Paulo II akajenga utamaduni wa majadiliano kwa njia ya amani na Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto XVI akajikita katika majadiliano ya upendo katika ukweli na katika maadhimisho ya miaka hamsini ya mchakato wa majadiliano ya kidini, Papa Francisko anawachangamotisha waamini kujenga majadiliano ya urafiki kwa kukutana na watu.

Kardinali Jean Louis Tauran anasema, majadiliano ya kidini ni changamoto endelevu ndani ya Kanisa, inayopaswa kujikita katika ujasiri, hekima, uvumilivu na udumifu, daima kwa kuendelea kumtumainia Roho Mtakatifu, kama alivyofanya Papa Paulo VI wakati wa maadhimisho ya Pentekoste kwa Mwaka 1964, hapo ukawa ni mwanzo wa Baraza la Kipapa la majadiliano ya kidini. Mchakato wa majadiliano bado una njia ndefu na umesheheni changamoto nyingi!

Habari hii imeandaliwa na
Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.








All the contents on this site are copyrighted ©.