Matatizo ndani ya Kanisa yanatatuliwa kwa njia ya upembuzi yakinifu, majadiliano na
sala!
Baba Mtakatifu Francisko katika tafakari yake wakati wa Sala ya Malkia wa mbingu,
Jumapili tarehe 18 Mei 2014 anasema, Liturujia ya Neno la Mungu, inaonesha matatizo
yaliyojitokeza kwenye Jumuiya ya Wakristo wa mwanzo, baada ya Kanisa kukua na kuongezeka
kadiri ya mapenzi ya Kristo na hivyo, kufungua mipaka kwa watu kutoka tamaduni nyingine.
Hali hii ilisababisha manung'uniko kama inavyojitokeza hata leo katika baadhi
ya Parokia. Maskini, wajane na yatima wa Kiyunani walisahauliwa katika huduma msingi
zilizokuwa zinatolewa, Waebrania wakapewa upendeleo wa pekee. Katika hali kama hii
anasema Baba Mtakatifu, Mitume waliamua kulivalia njuga tatizo hili kwa kukutana na
kujadili kwa pamoja, kwa kutambua kwamba, kulikuwa na tatizo lililokuwa linahitaji
kupatiwa ufumbuzi. Hapa viongozi wa Kanisa na waamini wanajadiliana na hatimaye, kugawana
majukumu katika Kanisa.
Mitume wakaamua kujikita katika kutangaza Neno la Mungu
na Sala na Mashemasi saba waliochaguliwa wakapewa dhamana ya kuhudumia mezani pamoja
na kuwasaidia maskini. Hawa ni watu waliochaguliwa kwa sababu ni watu waliokuwa waaminifu,
wenye imani na wamejaa Roho Mtakatifu pamoja na kuwa na hekima. Mashemasi hawa wakaombewa
na Mitume. Hali ikawa shwari na Kanisa likasonga mbele.
Baba Mtakatifu Francisko
anasema, matatizo na changamoto mbali mbali ndani ya Kanisa zinatatuliwa kwa njia
upembuzi yakinifu, majadiliano na sala, kwa kutambua kwamba, umbea, wivu na kijicho
ni mambo ambayo hayana tija wala mashiko kwa ustawi na maendeleo ya Kanisa na kamwe
hayataweza kuleta amani na utulivu. Waamini hawana budi kumwachia nafasi Roho Mtakatifu
ili aweze kuwaongoza katika mchakato wa kufikia umoja, amani na utulivu kwa kuheshimu
na kuthamini zawadi na karama mbali mbali zilizoko ndani ya Kanisa.
Mara baada
ya Sala ya Malkia wa mbingu, Baba Mtakatifu Francisko aliyaelekeza mawazo yake huko
Serbia na Bosnia ambako zaidi ya watu thelathini walifariki maji baada ya kukumbwa
na mafuriko na wengine zaidi ya elfu kumi na tano hawana makazi baada ya nyumba zao
kusombwa na mafuriko, mwishoni mwa juma. Baba Mtakatifu amewahakikishi uwepo wake
wa karibu kwa njia ya sala.
Baba Mtakatifu amemkumbuka pia Mwenyeheri Askofu
Anton Durcovic, shahidi wa imani, mchungaji mwaminifu na jasiri, aliyeuwawa kikatili
na utawala wa kinazi kunako mwaka 1951. Baba Mtakatifu anaungana na waamini wa Jimbo
la Ias na Romania katika ujumla wake kwa ajili ya kumshukuru Mungu kwa kulijalia Kanisa
mwamini shujaa na shupavu katika imani.