2014-05-17 15:58:52

Mwenyeheri Anton Durcovic


Mtumishi wa Mungu Askofu Anton Durcovic aliyezaliwa kunako tarehe 17 Mei 1888 nchini Austria ametangazwa Mwenyeheri na Kardinali Angelo Amato kwa niaba ya Baba Mtakatifu Francisko, huko Bucarest, tarehe 17 Mei 2014.

Akizungumzia kuhusu tukio hili, Kardinali Angelo Amato, Mwenyekiti wa Baraza la Kipapa la kuwatangaza waamini kuwa wenyeheri na watakatifu anasema kwamba, Baba yake mzazi alifariki dunia akiwa na umri wa miaka sita na hivyo kulazimika kwenda kuishi na Mama na Kaka yake nchini Romania. Akasoma mjini Bucarest na Roma na kufanikiwa kupata cheti za uzamivu katika masomo ya falsafa na taalimungu.

Mwenyeheri Durcovic alipadrishwa kunako Mwaka 1910 na kwa miaka mingi akajisadaka kufundisha dini shuleni na shughuli za kichungaji Parokiani. Kunako Mwaka 1947 akateuliwa kuwa Askofu wa Jimbo Katoliki Ias lililoko Romania na kuwekwa wakfu kunako Mwezi Aprili 1948. Hapa akaanza kujitosa bila ya kujibakiza kwa ajili ya shughuli za kitume kwa kutembelea Parokia pamoja na kuwaimarisha ndugu zake katika Kristo ili waweze kuwa jasiri na imara katika imani.

Mwenyeheri Anton Durcovic anaongeza idadi ya Maaskofu na Mapadre kutoka Romania waliokwishatangazwa na Mama Kanisa kutokana na uaminifu wao kwa Kristo na Kanisa lake, kiasi hata cha kuyamimina maisha yao,ushuhuda wa hali ya juu wa imani katika matendo. Romani ni nchi ambayo imebahatika kuwa na Mashahidi wengi wa imani. Itakumbukwa kwamba, Mwezi Agosti 2013, Padre Vladimir Ghika alitangazwa kuwa Mwenyeheri. Hawa ni Mashahidi wanaoendelea kulipamba Kanisa.

Baba Mtakatifu Francisko katika barua yake ya kitume anamtaja kuwa ni mchungaji jasiri, mtume wa Ibada ya Kuabudu Ekaristi Takatifu na shahidi jasiri wa umoja na Khalifa wa Mtakatifu Petro. Mwenyeheri Anton Durcovic alikuwa ni mpenda amani, mtu mwenye imani, mapendo na huruma. Alionesha upendo wa pekee kwa maskini na wote waliokuwa wanasukumizwa pembezoni mwa Jamii. Jimboni mwake, kulikuwa na maskini wengi wa hali na kipato. Kwa kuguswa na mateso na mahangaiko ya watu wake, akaamua kufungua ukumbi wa chakula kwenye Shule ya Notre Dame de Sion kwa ajili ya maskini waliokuwa wanaishi mjini hapo.

Mashahidi wanasema kwamba, Mwenyeheri Anton Durcovic alibahatika kupendwa na wengi na wala hakuwa na maadui wala kutafutwa na wanasiasa, kwani kwake wote waliokuwa ni ndugu zake na kwamba, maneno yake yalikuwa ni chachu ya Injili na kwamba, alisema na kutenda yote kama Kristo mwingine na daima aliona madhulumu na mateso yakiandama maisha yake.

Kardinali Angelo Amato anasema, tarehe 26 Juni 1949 Askofu Anton Durcovic alikamatwa na kikosi cha usalama kwa kuhatarisha Ukomonisti, licha ya kuonesha unyenyekevu na hekima katika maisha yake. Hii ni siku ambayo alikuwa amepanga kutoa Sakramenti ya kipaimara kwa vijana 650 katika Parokia moja iliyokuwa pembeni mwa Jiji la Bucarest.

Akiwa njiani kwa miguu kuelekea Parokiani hapo, alikamatwa na vyombo vya usalama na kupotea bila kujulikana mahali alipokuwa, akawa anahamishwa kutoka gereza moja hadi jingine. Huko akateswa na kudhulumiwa sana, alikuwa ananyimwa maji na chakula, unyama wa binadamu! Huu ni ushuhuda uliotolewa na baadhi ya wafungwa wenzake waliobahatika kutoroka magerezani. Alitengwa na wafungwa wenzake, akafungiwa kwenye chumba cha kifo na hivyo kufariki dunia kati ya tarehe 10 na 11 Desemba 1951. Mwili wake ukachukuliwa na dereva na kwenda kuzikwa kwenye makaburi ya pamoja.

Kardinali Angelo Amato anasema, fundisho kubwa linalotolewa na Mwenyeheri Anton Durcovic ni kuwa na nguvu na wajasiri katika majaribu, kwa kutambua kwamba, upendo wa Kristo bado unawasindikiza hata katika madhulumu na mateso kama haya na kwamba, baada ya Ijumaa kuu kuna Pasaka, yaani ufufuko wa Bwana.

Mwenyeheri Anton Durcovic amekuwa kweli ni mfano wa kuigwa ndani na nje ya Romani. Bado anaendelea kukumbukwa na Familia ya Mungu Jimbo kuu la Bucarest na Jimboni kwake Ias. Hawa ni watu walioimarishwa katika maisha yao ya kiroho kiasi kwamba, wakaanza hija ya kutafuta utimilifu wa maisha ya Kiinjili. Ni kiongozi aliyeonesha utakatifu wa maisha kati ya watu wake!







All the contents on this site are copyrighted ©.