2014-05-17 15:57:17

Gusweni na mahangaiko ya wagonjwa na walemavu!


Baba Mtakatifu Francisko, Jumamosi, tarehe 17 Mei 2014 amewapongeza wanachama wa Chama cha Wahudumu wa Msalaba, kinachoadhimisha Jubilee ya miaka mia moja tangu alipozaliwa Mwenyeheri Padre Luigi Novarese, muasisi wa chama hiki.

Huyu ni Padre aliyeonesha upendo wa dhati kwa Kristo na Kanisa lake, akajisadaka kwa ajili ya huduma makini kwa wagonjwa. Ni Padre aliyeonja mateso na mahangaiko makubwa katika utoto wake, akajifunza na kuguswa na mahangaiko ya binadamu, ndiyo maana akaanzisha Chama cha Wahudumu wa Msalaba wanaotekeleza dhamana na utume wao katika hali ya ukimya pasi na makeke!

Wanachama hawa walipokutana na Baba Mtakatifu walikuwa wameandamana na wagonjwa wanaowahudumia wakiwa kwenye baiskeli maalum. Hawa Baba Mtakatifu amewashirikisha kwa namna ya pekee heri za mlimani, muhtasari wa mafundisho ya Yesu, akisema heri wanaohuzunika sasa maana hao watafarijiwa. Hawa ni watu ambao wanakabiliwa na matatizo ya afya, upweke, kutoeleweka na kwamba, kuna sababu nyingi ambazo zinaweza kumpelekea mtu kushikwa na majonzi na simanzi.

Hata hivyo wanapaswa kukumbuka kwamba, Yesu aliteseka na kudharauliwa sana, akajitwika mabegani mwake mateso na mahangaiko ya binadamu hadi mauti ya Msalaba. Yesu katika maisha yake hapa duniani ameonja mateso mengi, kiroho na kimwili; ameonja uchovu na njaa; hali ya kutoeleweka, akasalitiwa na kukimbiwa na Mitume wake, akachapwa mijeledi na hatimaye, akatundikwa na kufa Msalabani.

Baba Mtakatifu anasema, mateso na mahangaiko ya watu si jambo la kufurahia lakini ni ukweli ambao unamfunda mwanadamu kuishi kwa kuwa na mwelekeo sahihi wa maisha. Kuna baadhi ya watu wanaoona mateso katika mwelekeo hasi kabisa, kiasi cha kujikatia tamaa na kuasi, hali ambayo si nzuri hata kidogo anasema Baba Mtakatifu. Ukweli wa maisha, mateso na mahangaiko ya binadamu hayana budi kupokelewa kwa imani na matumaini na kuyarutubisha kwa upendo wa Mungu na jirani kwani upendo una nguvu ya kuleta mabadiliko ya kweli!

Haya ndiyo mafundisho ya kina yaliyotolewa na Mwenyeheri Luigi Novarese kwa kuwafundisha wagonjwa na walemavu kupokea na kuthamini mateso na mahangaiko yao mintarafu mwelekeo wa kitume, unaowawezesha kutekeleza yote katika imani na mapendo kwa jirani. Wagonjwa hawana budi kuwa ni wadau katika maisha na utume wao, kwani mgonjwa au mlemavu anaweza kuwa ni mwanga angavu kwa watu wengine wanaoteseka, kiasi cha kuleta mabadiliko makubwa katika mazingira ambamo wanaishi.

Baba Mtakatifu anawahakikishia kwamba, kwa karama hii, wao kweli ni zawadi kubwa kwa Mama Kanisa. Mateso na mahangaiko yao ni kama Madonda Matakatifu ya Yesu, ambayo kwa upande mmoja yanaonekana kuwa ni kashfa katika imani lakini pia yanaimarisha imani, kielelezo kwamba, kweli Mungu ni upendo, mwaminifu, mwenyehuruma na mfariji. Kwa kuungana na Yesu Kristo Mfufuka, wagonjwa na walemavu hawa ni sehemu ya wokovu na mchakato wa Uinjilishaji.

Baba Mtakatifu anawaalika na kuwahamasisha waamini na watu wote wenye mapenzi mema kuwa karibu na wote wanaoteseka kutokana na magonjwa, ili kuwaonjesha ushuhuda wa Kristo Mfufuka. Kwa njia hii wataweza kulitajirisha Kanisa pamoja na kuendelea kushirikiana na wachungaji wa Kanisa, kwa kusali na kutolea mateso na mahangaiko yao kwa ajili ya Kanisa.

Baba Mtakatifu mwishoni, anawaombea ili Bikira Maria awasaidie kuwa kweli ni wafanyakazi wa Fumbo la Msalaba na wahudumu wa mateso na mahangaiko ya binadamu kwa kujikita katika imani na matumaini pamoja na kuendelea kushikamana na Kristo.







All the contents on this site are copyrighted ©.