Kuna msemo uliokuwa unatumika sana miaka mitano au sita iliyopita, aliokuwa anaambiwa
mtu mwenye kuhangaika, mwenye makeke na asiye na subira labda kutokana na vurugu,
migongano na migogoro inayomkabiri alikuwa anaambiwa: “Tuliza boli”. Nadhani Yesu
angekuwa siku hizi naye angeutumia msemo huohuo katika Injili ya leo.
Mandhali
ya Injili ya leo ni ya karamu ya mwisho. Ni wakati ambao Yesu alibakiwa na muda mfupi
sana wa kuuacha ulimwengu huu. Liturjia linatuletea mazungumzo hayo wakati huu wa
Pasaka, hasa baada ya mateso na ufufuko wake kusudi ipate kueleweka vizuri zaidi,
kwa vile fasuli hii inazungumzia juu ya Tanzia au Wosia wa Yesu.
Kwa kawaida
Wosia husomwa baada ya kifo cha marehemu. Tunasoma Tanzia au Wosia wa Yesu Kristu
aliye Mwalimu wetu Mkuu baada ya kufufuka. Hiyo ni heshima kubwa sana na ni alama
ya kumwenzi. Wosia huu uliandikwa na mwanafunzi wake tena katika kipindi cha vurugu
ya hali ya juu sana ya jumuia ya wakristu ya Asia ndogo kati ya miaka 50 hadi 70 baada
ya Pasaka. Migogoro hiyo ilikuwa ya toka nje ya jumuia ya wakristu, lakini siyo ya
kumwaga damu, bali ilihusu hasa kudharauliwa na kuikebehi Injili.
Migongano
mingine ilikuwa ya ndani ya jumuia yenyewe iliyotokana na kuingia kwa ubaridi katika
kuiishi Injili hiyo. Kwa hiyo vurugu hiyo inawapelekea kuusoma Wosia huu Yesu kwa
namna ya tafakari zaidi. Wosia huu unaweza pia kuwa changamoto kwetu sisi leo tunaokabiliwa
na migongano na migogoro inayotusababishia kuwa na mahangaiko, katika jamii zetu na
katika ulimwengu wa leo kijumla.
Wosia unaanza kwa maneno ya Yesu anayowaambia
wafuasi wake: “Msifadhaike mioyoni mwenu” au angekuwa leo Yesu mwenyewe angeweza kusema:
“Tulizeni boli”. Yesu anawatuliza na kuwatahadharisha wanafunzi wake watambue kwamba
kutakuja tokea migongano, migogoro na vurugu, lakini watulie, wasihangaike. Neno la
lugha ya kigiriki lililotumika hapa linamaanisha machafuko kama yale ya baharini.
Yesu anajua kwamba, utume wake utaendelea, kwa hiyo wafuasi wake wataenda
ulimwenguni watakakokuwa kama kondoo kati ya mbwa mwitu. Wanahimizwa kutoogopa, badala
yake wamwamini Mungu na wamwimini Yeye.
Yesu anaendelea kuwatuliza na kuwaambia:
“Nyumbani mwa Baba yangu mna makao mengi, kama sivyo ningaliwaambia, maana naenda
kuwaandalia mhali.” Mahali anapoenda kuandaa Yesu, siyo mbinguni kama inavyoeleweka
na wengi, kwa sababu mbingu iko tayari toka mwanzo wa ulimwengu. Pahala anapoenda
kuandaa Yesu unaweza kupaona katika sura ya pili ya Injili ya Yohane, pale anapowafukuza
wafanya biashara hekaluni na kusema: Yaondoeni haya; msiifanye nyumba ya Baba yangu
kuwa nyumba ya biashara” (Yoh 2:16). Kwa hiyo nyumba au makao ya Baba yake ni hekalu.
Makao au hekalu hilo si kitu kingine zaidi ya Mwili wake, nafsi yake na jumuia
ya kikristu ambayo yeye mwenyewe yumo. Yesu mwenyewe ameandaa makao hayo kwa ajili
yetu sote. Hivi anaenda kuandaa hekalu ambamo anatualika sisi sote kuingia. Katika
nyumba ambayo ni jumuia ya wafuasi, kuna makao mengi. Kila mwanajamii ni makao na
kila mmoja ni makao ya Yesu.
Katika hekalu hilo la Mungu, kunatolewa sadaka
inayompendeza Mungu, sadaka ya ubani wa manukato yenye kutoa harufu nzuri inayopanda
kwa Mungu. Harufu hiyo nzuri ni upendo kwa jirani na kwa wote. Kila mmoja wetu anatofautiana
na mwingine kutokana na Mungu alivyotuumba.
Kwa hiyo tunagawana mapaji hayo
aliyotupatia Mungu ili kujenga maisha kamili. Tutafute jinsi ya kushirikishana mapaji
hayo ili kujenga jumuia, kudhihirisha maisha ya Mungu, ufalme wa mbingu ambao ni upendo.
Kila mmoja wetu anamhitaji mwingine. Yesu ametuandalia meza kubwa ya chakula tunapoweza
kugawiana hicho chakula, tunapoweza kunusa harufu nzuri ya manukato ya upendo.
Tunapokuwa
humo, unaweza kugundua mara moja harufu hiyo nzuri na ya pekee. Unapoinusa tu unagundua
mara moja kwamba harufu hii inatoka katika kiwanda gani, kwa sababu mchanganyiko wake
ni wa pekee. Kadhalika upendo unaotoka katika jumuia ya kikristu, huo unatoka kwa
Mungu, kwa vile hauna ubaguzi wala masherti. Harufu yake nzuri hutokana na hadhi yetu
ya kuwa wana wa Mungu. Kutokana na hadhi hiyo harufu yake inavutia watu wote wenye
kuihitaji.
Yesu aliingia wa kwanza katika nyumba hiyo inayonukia pale alipojitoa
mwenyewe kwa mateso na ufufuko wake. Kwa hiyo sisi sote inabidi kufahamu kule anakoelekea
Yeye. Kumbe kuna wengine hatupafahamu kama ilivyokuwa kwa pacha wetu Tomasi. Yeye
anajitosa kuuliza swali badala yako: “Bwana sisi hatujui uendako; nasi twaijuaje njia?”
Kwa sababu alichokuwa anakielewa Thomasi ni kwamba Yesu alikuwa anaenda kufa basi,
kwa sababu hakuwa bado na mang’amuzi ya ufufuko wa Yesu.
Jibu la Yesu ndiyo
linakuwa kiini cha Wosia au Tanzia ya Yesu: “Mimi ndimi njia, na ukweli na uzima”.
Maneno haya matatu yanaweza sasa kueleweka vizuri kwa mtazamo huo wa ufufuko, tena
ni maneno ambayo ni tahadhari kubwa sana dhidi ya maelekeo matatu potovu anayoweza
kumwingiza mkenge binadamu hapa ulimwenguni:
Neno la kwanza “Mimi ni njia”
maana ya njia ni safari, hapa inamaanisha safari ya kuelekea Pasaka. Msafara huo ni
mgumu unaodai sadaka (mateso) katika maisha. Yesu amewazungumzia mara nyingi sana
wanafunzi wake juu ya mateso hayo lakini hawakumwelewa. Aidha katika neno hili “Njia”
tunatahadharishwa kwamba yatakiwa kusafiri (maisha ni safari), lakini ni safari yenye
malengo siyo bora kupuyanga tu.
Katika mtazamo huu inakuja pia kueleweka zaidi
tamko la Yesu kuwa “nyumbani mwa baba yangu mna makao mengi”, yaani aliyekubali kuifuata
njia aliyopita Yesu, atajikuta mara moja yuko katika ufalme wa Mungu, katika nyumba
ya Baba. Nyumba hiyo siyo Paradisi, bali ni jumuia ya kikristu, humo kuna makao mengi,
yaani kuna shughuli nyingi za kufanya, kuna ujenzi wa kufanya. Kuna namna nyingi ambazo
kila mmoja anaweza kudhihirisha mwito wake katika imani. Hatujazaliwa tu bila malengo,
na hatufi tu na kuitwa akina ”kufa kunoga” au “kufabasi.”
Zaidi tena, Njia
hiyo siyo barabara ya kawaida, au kitabu fulani cha kufuata, au ramani ya safar, bali
ni nafsi yake Yesu. Yeye mwenyewe ndiyo Njia na safari inayotupeleka kwenye kituo
cha mwisho cha uwepo wetu. Kwa wengine, mwanzo wa maisha ni hewa na mwisho wake ni
hewa, kwa hiyo hata yeye mwenyewe anakuwa hewa. Hilo ndilo wazo alilo nalo Thomasi
anapoliuliza swali lake. Kumbe Yesu ni Njia anayotupelekea kwenye Ufufuko.
Neno
la pili, “Mimi ni Ukweli”. Neno hili ni la msingi sana kwani linatutahadharisha juu
ya kumwelewa Mungu. Kukosea jinsi ya kumwelewa Mungu ni kosa nzito linaloweza kumgharimu
sana binadamu, kwa sababu linakufanya umkosee pia binadamu mwenzako, kuyakosea haki
maisha yako, kukosea jinsi ya kupambanua wema na ubaya na hatimaye kuikosea hata historia
nzima ya maisha. Inatisha na kusikitisha sana kukutana na mtu wenye huzuni kwa sababu
anao utambuzi mdogo sana tena wa kimakosa juu ya Mungu.
Yesu bila kuchoka
anatuonesha Mungu wa kweli aliyepanua mikono wazi ili kutupokea, Mungu mwenye moyo
mpendevu, Mungu mwenye haki na huruma. Maisha yetu ni kumwongokea Mungu anayetudhihirishia
Yesu Kristu. Hivi hapa “Ukweli” siyo kitu cha kiakili au kidhahania, bali ni nafsi,
na mtu kweli aliyefaulu, ambaye Mungu amejidhihirisha kwake naye ni Yesu Kristu.
Neno
la tatu ni “Mimi ni Uzima” linatutahadharisha juu ya maelekeo ya kifo ambayo tunayapakilia
akilini mwetu pale tunapojitumbukiza katika dimbwi la maisha yasiyo na maana, katika
kuangamiza maisha yetu. Yesu ni uzima, siyo uzima ule wa kibaolojia, bali ni maisha
ya Mungu ambayo hayajaguswa na maisha ya kibayolojia.
Wosia unaendelea kutuambia:
“Mngalinijua mimi, mngalimjua na Baba, tangu sasa mnamjua, tena mmemwona” Filipo anamwambia:
“Bwana utuonyeshe Baba yatutosha.” Yesu akamjibu: Mimi nimekuwapo pamoja nanyi siku
hizi zote, wewe usinijue, filipo? Aliyeniona mimi amemwona Baba.” Binadamu anayo hamu
kubwa ya kumwona Mungu kwa sababu ulimwengu huu haumtoshelezi. Kwa hiyo, jinsi pekee
ya kuweza kuutafakari uso wa Mungu Baba ni kumtafakari Mwana.
Mara mbili tunaisikia
sauti ya Mungu Baba ikimnadisha huyo Mwanae. Nafasi ya kwanza alipobatizwa na nafasi
ya pili alipogeuka sura, Mungu alisema: “Huyu ni mwanangu mpenzi, niliyependezwa naye,
msikilizeni yeye”. Kwa hiyo, tukitaka kumtambua Mungu, tumwangalie Yesu. Angalia anavyoishi,
anavyopenda, anavyowapokea watu wote. Angalia anavyoenda kukabili mateso na anavyomwelewa
Mungu na anavyoyaelewa maisha.
Wakati mwingine tunasikia watu wakisema: dini
zote ni sawa, au miungu wote ni sawa. Kwa vyovyote Mungu ni mmoja ila kila mwamini
anamwita huyo Mungu kadiri ya imani yake. Tofauti iliyoko kati ya dini na dini nyingine
ni ile sura anayoisema Yesu anapomjibu Filipo kuwa: “Ukiniangalia mimi na matendo
yangu niliyoishayafanya utagundua kuwa ni namna hiyohiyo ya kutenda, na ni matendo
hayohayo anayofanya Baba wa mbinguni.” Kwa hiyo, sura ya Mungu katika Yesu Kristu,
siyo sura "feki".
Mungu huyo ni Baba wa maskini, Baba wa wajane, ni Mlinzi
wa wanaoonewa, ni Mlinzi wa wageni, ni Mkombozi wa wanaokandamizwa. Sura ya Mungu
aina hiyo ndiyo unaiona katika Kristu. Uso wa Mungu unauona katika Kristu ambaye kilele
chake unakiona pale Kalvari anapotoa maisha yake kwa ajili ya kuwapenda wengine. Mungu
wa Kristu ni yule ambaye hata kama umemkosea yeye anasema: Mimi ninakupenda. Upendo
huo unauona Msalabani.
Kisha wosia unahitimisha kwa kututia moyo: “Yeye aniaminiye
mimi kazi nizifanyazo mimi, yeye naye atazifanya; naam na kubwa kuliko hizo atafanya,
kwa kuwa mimi naenda kwa Baba.” Endapo Yesu peke alikuwa amefanya kazi hiyo nzuri
tena kwa muda wa miaka mitatu tu na katika nchi ndogo, kumbe sisi sasa tulio katika
jumuia ya wakristu wengi iliyoitwa kueneza upendo wa Kristu ulimwengu kote tutafanya
makubwa zaidi. Kwa hiyo, “Tulizeni boli ndo kwaanza mchezo unaanza”.