2014-05-16 08:47:25

Mambo yameiva huko Nchi Takatifu!


Padre Federico Lombardi msemaji mkuu wa Vatican anasema kwamba, hija ya kitume ya Baba Mtakatifu Francisko nchini Takatifu kuanzia tarehe 24 hadi tarehe 26 Mei 2014 imesheheni utajiri mkubwa wa maisha na utume wa Kanisa katika mchakato wa majadiliano ya kiekumene yaliyoanzishwa na Mtumishi wa Mungu Papa Paulo VI kwa kukutana, kuzungumza na kusali na Patriaki Anathegoras wa Yerusalemu, miaka hamsini iliyopita.

Kilele cha hija hii ya kiekumene ni pale Baba Mtakatifu Francisko watakapokutana na kusalimiana, kuzungumza na kusali pamoja na Patriaki Bartolomeo wa kwanza, Jumapili jioni, kwenye Kaburi Takatifu. Kuna matukio mengine muhimu sana katika hija hii ya kiekumene, adhimisho la Ibada ya Misa Takatifu mjini Amman na ile itakayoadhimishwa kwenye Pango la Mtoto Yesu mjini Bethlehemu pamoja na kutembelea maeneo makuu ya historia na maisha ya Yesu hapa duniani.

Padre Lombardi anasema, Baba Mtakatifu atakutakana na waamini, viongozi wa Kanisa na Serikali pamoja na wawakilishi wa wahamiaji na wakimbizi walioko huko Mashariki ya Kati, wanaohudumia kwenye kambi mbali mbali. Baba Mtakatifu akiwa katika Nchi Takatifu atakutana na kuzungumza na Rabbi Abraham Skorka Rabbi mkuu kutoka Argentina ambaye ataambatana na Bwana Omar Abboud, Rais waTaasisi ya Majadiliano ya Kidini mjini Buenos Aires.







All the contents on this site are copyrighted ©.