2014-05-15 12:32:28

Nigeria yashutumiwa kwa kutaka kujadiliana na magaidi!


Serikali ya Nigeria imeonesha nia ya kutaka kujadiliana na Kikundi cha Kigaidi cha Boko Haram, ili kupata muafaka utakaokiwezesha kikundi cha Boko Haram kuwaachilia huru wasichana wa shule waliotekwa nyara, Kaskazini mwa Nigeria, jambo ambalo limeshutumiwa vikali na Serikali ya Marekani kwa kusema kwamba, hakuna haja ya kuzungumza na magaidi!

Kwa kipindi cha miaka minne, Boko Haram imehusika na umwagaji wa damu ya watu wasiokuwa na hatia nchini Nigeria pamoja na kusababisha uharibifu mkubwa wa miundo mbinu na mali za watu. Serikali ya Nigeria ilianzisha opresheni maalum ya kuwasaka wanajeshi wa Kikundi cha Boko Haram, lakini hadi sasa hakuna mafanikio yoyote na watu wanaendelea kupoteza maisha yao.

Hivi karibuni, Rais Goodluck Jonathan wa Nigeria aliomba msaada kutoka kwenye Jumuiya ya Kimataifa na kwamba, tayari kuna baadhi ya nchi zimekwishatuma makachero wake kufanya kazi hii, ili kupambana na Kikundi cha Boko Haram. Hali ya hatari iliyotangazwa na Serikali ya Nigeria kwa kipindi cha miezi sita, inafikia ukomo wake, tarehe 15 Mei 2014! Kifuatacho nchini Nigeria bado kimebaki kuwa ni kitendawili!







All the contents on this site are copyrighted ©.