2014-05-15 09:25:06

Haki msingi za familia!


Baraza la Maaskofu Katoliki Ufilippini, limehitimisha Kongamano la Familia Kimataifa Barani Asia, lililomshirikisha pia Askofu mkuu Jean Laffite, Katibu mkuu wa Baraza la Kipapa la Familia aliyekazia umuhimu wa Jamii kulinda na kudumisha haki msingi za maisha ya ndoa na familia kwa kujikita katika kuenzi uhai, tunu ambayo leo hii iko hatarini kutokana na maendeleo ya sayansi na teknolojia pamoja na ubinafsi wa baadhi ya watu ambao hawataki tena kuwajibika katika masuala ya ndoa na familia!

Askofu mkuu Laffite anasema, mchako wa maandalizi na hatimaye wa maadhimisho ya Sinodi maalum ya Maaskofu kwa ajili ya familia itakayofanyika katika awamu mbili kama alivyopanga Baba Mtakatifu Francisko, ni kuliwezesha Kanisa kuangalia changamoto zinazoigusa familia katika ulimwengu mamboleo. Ni fursa ya kuangalia ni jinsi gani Kanisa linaweza kuwasadia wanandoa watarajiwa kujiandaa kikamilifu katika utekelezaji wa dhana na utume wao katika ndoa na familia, kwa kukuza na kuimarisha utume wa familia.

Kongamano hili limeongozwa na kauli mbiu "Familia Barani Asia, mwanga wa matumaini", jambo linaloonesha matumaini ya Kanisa kwa ajili ya familia kwa siku za usoni, kwa kushiriki katika mchakato wa Uinjilishaji mpya, kama alivyowahi kusema Mtakatifu Yohane Paulo II alipotembelea Ufilippini.

Ni mwaliko wa kuinjilisha kwa kuonesha mshikamano wa familia zilizoungana, familia zinazosimikwa katika imani, matumaini na mapendo, wakati wote wa maisha, kwa kujikita katika Sakramenti za Kanisa pamoja na kuendelea kujitajirisha kwa tafakari ya Neno la Mungu, linalomwilishwa katika matendo ya huruma! Familia za Kikristo zioneshe ile furaha na matumaini yanayobubujika kutoka katika maisha ya ndoa na familia, kwa kukazia pia maisha ya pamoja, mahali ambapo watu wanashirikishana mang'amuzi na kweli za maisha.

Askofu mkuu Laffite katika hotuba yake amegusia kwa kina na mapana kuhusu "Mwongozo wa Haki Msingi za Kifamilia", Waraka ambao ulikuwa umeandaliwa na Mtakatifu Yohane Paulo II kwa ajili ya Familia, lakini hakufanikiwa kuuchapa hadharani kama mwongozo wa Kanisa kuhusiana na utume wa familia ndani ya Kanisa na Jamii katika ujumla wake. Ameangalia umuhimu wa familia na ndoa kama taasisi kadiri ya sheria.

Mtakatifu Yohane Paulo II alipenda kukazia kwa namna ya pekee haki msingi za kifamilia zinazofumbatwa katika asili ya familia. Hizi ni haki zinazopaswa kuheshimiwa, kulindwa na kuendelezwa. Jumuiya ya Kimataifa haina budi kukuza na kuendeleza sera makini kwa ajili ya ndoa na familia.







All the contents on this site are copyrighted ©.