2014-05-13 11:56:22

Kumbu kumbu ya Bikira Maria wa Fatima


Patriaki Fouad Twal wa Yerusalemu ni kati ya wageni mashuhuri walioshiriki katika mkesha na maadhimisho ya Kumbu kumbu ya miaka tisini na saba, tangu Bikira Maria alipowatokea Watoto wa Fatima: Yacinta, Francis na Lucia; Siku kuu ambayo inaadhimishwa na Mama Kanisa kila mwaka ifikapo tarehe 13 Mei. Ni siku ambayo, watu wengi wanakumbuka, jaribio la kutaka kumuua Mtakatifu Yohane Paulo wa Pili.

Patriaki Twal amewataka waamini kusali kwa ajili ya kuombea haki na amani huko Mashariki ya Kati pamoja na kuendelea kuwasaidia kwa hali na mali pamoja na kuhakikisha kwamba, sheria za kimataifa zinaheshimiwa na kutekelezwa huko Mashariki ya kati kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya wengi. Patriaki Twal anasema, nia yake ni kumwomba Bikira Maria wa Fatima, ili aweze kusaidia kufanikisha hija ya kichungaji ya Baba Mtakatifu Francisko huko Mashariki ya Kati, inayoongozwa na kauli mbiu, ili wote wawe wamoja, itakayoanza hapo tarehe 24 hadi tarehe 26 Mei 2014. Hapa Baba Mtakatifu anatarajiwa kutembelea Yordan, Palestina na Israeli.

Patriaki Twal amewataka waamini na watu wote wenye mapenzi mema kumsindikiza Baba Mtakatifu Francisko katika hija yake ya kichungaji na kiekumene huko Mashariki ya Kati, huko ni mahali ambapo Ukristo umeota mizizi inayoonesha historia nzima ya Ukombozi.







All the contents on this site are copyrighted ©.