2014-05-13 12:20:09

Kiburi na majivuno ni sumu ya maisha ya kiroho!


Imani ni zawadi kutoka kwa Mungu inayoweza kupokelewa na mwamini akiwa ameungana na Mwenyezi Mungu pamoja na Kanisa lake na kwamba, madhulumu ndani ya Kanisa yamewawezesha waamini kuwa jasiri na hivyo kutoka kifua mbele kutangaza Habari Njema ya Wokovu kati ya mataifa, huko Antiokia na Ugiriki, watu wakamfungulia Kristo malango ya maisha yao na wengi wakabatizwa!

Ni kundi la waamini lililojiachilia mikononi mwa Roho Mtakatifu, ili aweze kutenda kadiri ya uwezo wake, hii ndiyo nguvu ya Roho Mtakatifu inayoweza kutenda hadi kuwashangaza wengi, kama alivyofanya Filipo alipombatiza Malkia wa kushi au Mtakatifu Petro aliyepelekwa kumbatiza Korneli na familia yake, changamoto na mwaliko kwa waamini kumwachia nafasi Roho Mtakatifu bila kumwekea kizingiti, bali kujivika fadhila ya unyenyekevu.

Ni sehemu ya mahubiri yaliyotolewa na Baba Mtakatifu Francisko wakati wa Ibada ya Misa kwenye Kikanisa cha Mtakatifu Martha kilichoko mjini Vatican siku ya Jumanne, tarehe 13 Mei 2014. Baba Mtakatifu anasema kuna kundi la Wakuu wa Makuhani ambalo daima lilikuwa linasigana na Yesu katika mambo mengi, kwani wao walidhani kwamba, dini ilijisimika katika Sheria na kile ambacho wao waliamini kutoka akilini mwao, wakashindwa kutambua kwamba, walihitaji upendo na uzuri wa imani, kwani hili ni kundi linalotaka maelezo basi!

Baba Mtakatifu anasema hawa ni watu waliokuwa na shingo nguvu, hata baada ya kupewa maelezo ya kina na Yesu, bado waliendelea kumfuata futa wakitaka kwanza kabisa kumnyamazisha na hatimaye kumfutilia mbali kutoka katika uso wa dunia. Walishindwa kufungua mioyo yao kwa Mtakatifu wa Mungu na kwa Roho Mtakatifu. Ni watu waliokuwa na kiburi na kujiamini kupita kiasi, ni watu ambao hawakupenda kuwa sehemu ya kundi la Kondoo wa Kristo, kwani walifunga kabisa mioyo yao.

Imani ni zawadi inayopokelewa na mtu binafsi na kuendelea kuiboresha kwa maisha ya Sakramenti za Kanisa pamoja na kushikamana na watu wa Mungu wanaofanya hija ya imani kwa kusikiliza kwa unyofu, kile ambacho Roho Mtakatifu anataka kutoka kwa Kanisa. Kiburi na majivuno anasema Baba Mtakatifu ni hatari kwa ustawi wa maisha ya kiroho, mwaliko kwa waamini kumwomba Roho Mtakatifu ili aweze kuwasaidia kuwa wasikivu na wanyenyekevu kwa Roho Mtakatifu na kutekeleza kile anacho waambia.







All the contents on this site are copyrighted ©.