2014-05-13 07:47:21

Katiba ni sheria mama!


Serikali ya Mauritius hivi karibuni imeanza mchakato wa mabadiliko ya kuandika Katiba Mpya na Baraza la Maaskofu Katoliki nchini humo linasema, Katiba mpya haina budi kuwapatia wananchi wa Mauritius utu na heshima ya kidemokrasia. Maaskofu wamepongeza rasimu ya Katiba mpya kwa kuondoa harufu ya ukabila ndani ya Katiba, jambo ambalo ni sumu na kikwazo cha maendeleo endelevu wakati wa kupiga kura. RealAudioMP3

Askofu mkuu Maurice Piat wa Jimbo Katoliki la Port-Louis anasema, pamoja na hatua hii ambayo imefikiwa na Serikali ya Mauritius kwa sasa lakini bado kuna haja ya kujenga na kuimarisha umoja na mshikamano wa kitaifa, kwa kuhakikisha kwamba, wabunge wanaochaguliwa na wananchi wanawakilisha maoni, matatizo na changamoto wanazokabiliana nazo katika maisha yao ya kila siku.

Kwa sasa wananchi wengi hawana imani na wabunge wao kutokana na kujikita mno katika ubinafsi na kusahau mafao ya wengi, mambo ambayo yanaweza kuchangia kusuasua kwa mchakato wa kukuza na kuimarisha demokrasia na utawala wa sheria nchini humo.

Uwakilishi wa wanawake ndani ya Bunge ni kati ya mabadiliko makubwa yanayooneshwa kwenye Muswada wa Katiba Mpya, ili kuleta uwiano na ubora katika mijadala mbali mbali ndani ya Bunge kwa kuwashirikisha wanawake katika kuchangia na kutoa maamuzi katika ustawi na maendeleo ya wengi.

Maaskofu wanapongeza pia mchango wa Tume huru ya uchaguzi katika kupanga na kuteua wabunge kufuatana na vipaumbele vya majina kutoka katika vyama husika. Jambo muhimu la kuzingatia ni kuhakikisha kwamba, Tume huru ya uchaguzi inatekeleza dhamana yake kwa kuzingatia kanuni msingi za ukweli, uwazi na mafao ya wengi, kama njia ya kufutilia mbali rushwa na ufisadi ambao umekuwa ni sumu ya demokrasia ya kweli. Ili kukuza haki msingi za binadamu, utawala wa sheria, mafao ya wengi na amani ya kudumu, viongozi wa kisiasa hawana budi kutafuta mwarobaini wa matatizo na changamoto zilizoko nchini mwao ili kutibu kuanzia kwenye mizizi yake.

Rasilimali ya nchi haina budi kutumika kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya wananchi wote na wala si kwa ajili ya kuwanufaisha watu wachache wenye uchu wa mali na madaraka. Katiba Mpya iwe kweli ni sheria mama itakayorudisha hadhi na demokrasia ya kweli nchini Mauritius.








All the contents on this site are copyrighted ©.