Hotuba ya Rais Jakaya Kikwete wakati wa maadhimisho ya Siku ya Wauguzi Duniani kwa
Mwaka 2014.
Nakushukuru sana Ndugu Rais na viongozi wenzako wa Chama cha Wauguzi
na Wakunga (TANNA) kwa heshima kubwa mliyonipa ya kuja kujumuika nanyi katika maadhimisho
ya mwaka huu ya Siku ya Wauguzi Duniani. Nakupongeza pia Mheshimiwa Magesa Mulongo,
Mkuu wa Mkoa wa Arusha na wananchi wote wa Arusha kwa kutupokea vizuri na kwa kukubali
kuwa wenyeji wa sherehe hii na kushiriki kwa ukamilifu katika kufanikisha maandalizi
yake.
Nawapongeza nyote kwa maandalizi mazuri ya maadhimisho haya. Hakika
yamefana sana. Nimefurahishwa na maonesho kuhusu baadhi ya shughuli zinazofanywa na
wauguzi katika kuwahudumia Watanzania. Maonesho ya aina hii husaidia sana kukuza uelewa
wa wananchi kuhusu majukumu yenu, wajibu wenu na mchango wenu katika kuimarisha afya
za Watanzania.
Pamoja na kutembelea mabanda ya maonyesho, nimeshuhudia maandamano
yenu na kusoma ujumbe kwenye mabango ya washiriki. Pia nimesikiliza Risala yenu iliyosomwa
kwa ufasaha na utulivu mkubwa na Rais wa Chama cha Wauguzi Ndugu Paul Magesa. Kwa
ujumla, maadhimisho haya yanadhihirisha kuwa wauguzi ni kiungo muhimu sana katika
utoaji na maendeleo ya huduma ya afya nchini na ni nguvu thabiti ya mabadiliko.
Kauli
Mbiu
Ndugu Rais wa Chama cha Wauguzi; Ndugu Wauguzi na ndugu wananchi; Nilipopata
mwaliko kutoka kwenu sikusita kukubali kuja kujumuika nanyi siku ya leo kwa sababu
kuu mbili. Kwanza, kwamba wauguzi ni kada muhimu sana katika utoaji na maendeleo ya
huduma ya afya nchini. Bila ya kuwepo wauguzi huduma ya afya itayumba. Natambua kuwa
Wauguzi ni zaidi ya asilimia 60 ya watumishi wote wa sekta ya afya na hutekeleza asilimia
80ya shughuli zote za afya. Aidha, Muuguzi ndiye mwenye kuandaa mazingira mazuri kwa
daktari kutekeleza majukumu yake. Daktari anapomaliza kumuona mgonjwa, na kutoa maelekezo
yake, Muuguzi husimamia utekelezaji wa maelekezo hayo pamoja na tiba yenyewe. Muuguzi
ndiye anayefanya kazi ya kuuguza mgonjwa. Sote ni mashahidi kuwa wagonjwa wanatumia
wakati mwingi zaidi mikononi mwa wauguzi kuliko muda wanaoutumia mikononi mwa wahudumu
wengine wa afya.
Ndugu Rais wa Chama cha Wauguzi; Ndugu Wauguzi;
Sababu
ya pili ni kwamba nimevutiwa na kauli mbiu ya maadhimisho ya mwaka huu isemayo;“Wauguzi
ni Nguvu ya Mabadiliko na Rasilimali Muhimu ya Afya”. Ni kauli mbiu sahihi na mwafaka
kabisa. Ni ukweli ulio wazi kuwa wauguzi wanayo nafasi maalum katika maendeleo ya
huduma ya afya na sekta yenyewe kwa jumla. Ni chachu muhimu ya mabadiliko katika sekta
ya afya, na ndiyo rasilimali ya kuwezesha mabadiliko hayo kutokea na kufanikiwa.
Huwezi
kuzungumzia mabadiliko katika sekta hii bila kutambua mchango wa Wauguzi na kuwahusisha.
Ujenzi wa miundombinu ya vituo vya kutoa huduma ya afya, ununuzi na usambazaji wa
madawa, ununuzi wa vitendea kazi vya kisasa katika hospitali zetu vitakuwa na maana
tu pale ambapo wauguzi wapo na wanatimiza wajibu wao ipasavyo. Tunaweza kusema kwa
uhakika kabisa kuwa hakuna mbadala wa wauguzi.
Ndugu Wananchi; Uangalizi
unaotolewa na wauguzi, upendo na huruma yao husaidia sana kurejesha matumaini ya wagonjwa
na watu wengine wanaojishughulisha na maendeleo ya huduma ya afya. Huongeza ari ya
mapambano dhidi ya maradhi na kuleta matumaini kwamba ushindi utapatikana. Ninyi ndiyo
kioo cha huduma ya afya. Ndiyo watu wa kwanza mnaokutana na wagonjwa wanapofika hospitali,
na ni watu wa mwisho kuwaona wanapotoka baada ya matibabu.
Mheshimiwa Naibu
Waziri; Rais wa Chama cha Wauguzi; Ndugu Wauguzi na ndugu Wananchi;
Kuboresha
huduma ya afya ni moja ya vipaumbele vya juu vya Serikali ninayoiongoza na ndiyo maagizo
ya Ilani ya Uchanguzi ya Chama Tawala – CCM. Kwa sababu hiyo tulipoingia madarakani
mwaka 2005 tulitoa umuhimu wa pekee kwa zoezi la kupitia upya Sera ya Afya ya mwaka
1997 kwa lengo la kuihuisha. Matokeo yake ni kupatikana kwa Sera Mpya ya Afya ya mwaka
2007 na Mpango wa Maendeleo ya Afya ya Msingi wa mwaka 2007 uliotengenezwa maalum
kuongoza utekelezaji wa Sera hiyo.
Kama mjuavyo huu ni mpango wa miaka kumi
mpaka mwaka 2017 unaolenga kuleta mageuzi na maendeleo makubwa katika sekta ya afya.
Kwa muhtasari tumepanga kufanya mambo makuu mawili. Kwanza, kusogeza huduma ya afya
karibu na wanapoishi wananchi kwa kujenga na kuimarisha vituo vya kutolea huduma za
afya. Pili, kuimarisha ubora wa huduma ya afya inayotolewa kwa wananchi kwa kuvipatia
vituo hivyo vifaa vya uchunguzi na tiba vilivyo bora pamoja na dawa za kutosha. Pia
kuvipatia rasilimali watu, kwa maana ya Madaktari, Waganga, Wauguzi, Wakunga na Wataalamu
wengine wa afya.
Ndugu Wauguzi na Ndugu Wanannchi;
Leo miaka karibu
saba baadae ninyi ndiyo mashahidi wa mafanikio tuliyoyapata katika utekelezaji wa
Mpango huu. Tumefanikiwa kwa kiasi cha kutia moyo ingawaje bado tunayo kazi kubwa
mbele yetu. Kwanza kabisa tumeongeza sana bajeti ya afya kutoka shilingi bilioni 271
mwaka 2005/2006 hadi shilingi trilioni 1.4 mwaka 2013/2014. Imekuwa bajeti ya tatu
kwa ukubwa baada ya elimu na miundombinu kutoka ya sita. Kwa sababu ya ongezeko hilo
tumeshuhudia mambo mengi mazuri yakifanyika katika kuboresha huduma ya afya nchini.
Kwa mfano, zahanati ziko 5,960 ukilinganisha na 4,930 zilizokuwepo mwaka 2007. Vituo
vya afya viko 716 ukilinganisha na 565 na hospitali ziko 249 ukilinganisha na 230
wakati ule.
Kazi kubwa imefanyika kuimarisha hospitali za Wilaya, Mikoa, Kanda
na Hospitali ya Taifa Muhimbili. Kazi bado inaendelea na tunaweza kusema ndiyo kwanza
imechanganya. Miundombinu imeongezwa na majengo mengine yanaendelea kujengwa. Huduma
zinaendelea kuboreshwa na nyingine ambazo hazikuwepo zimeanzishwa. Hali kadhalika
vifaa tiba na uchunguzi vya kisasa vimeendelea kuwekwa na uwezo wa hospitali kuchunguza
na kutibu maradhi umekuwa mkubwa.
Tumeendelea kupanua fursa za mafunzo na
ajira kwa Madaktari, Wauguzi na Wataalamu wengine wa afya. Kwa upande wa mafunzo kwa
mfano Madaktari waliojiunga na mafunzo wameongezeka kutoka 520 mwaka 2005 hadi 1,057hivi
sasa. Kwa Wauguzi na Wakunga wameongezeka kutoka 1,586 mwaka 2005 hadi 3,569 hivi
sasa, kwa jumla kila kada imeongezeka. Ujenzi wa Kampasi mpya ya Chuo Kikuu cha Tiba
na Sayansi Shirikishi cha Muhimbili pale Mloganzila itaongeza sana uwezo wetu wa kufundisha
Madaktari na Wauguzi kutoka Chuo hicho kutoka 3,000 mpaka 15,000.
Ukiongeza
na wanafunzi 5,000 wa Chuo cha Tiba katika Chuo Kikuu cha Dodoma tatizo la rasilimali
watu nchini litapatiwa ufumbuzi miaka michache ijayo. Tayari ujenzi wa Hospitali ya
Kufundishia ya vitanda 600umeanza pale Mloganzila. Hospitali hiyo nayo itaimarisha
ubora wa huduma ya uchunguzi na tiba ya maradhi kwa namna yake hapa nchini. Hali kadhalika
ujenzi wa Hospitali ya Kufundishia pale UDOM unatarajiwa kukamilika mwaka huu.
Hivyo
hivyo, kwa upande wa ajira nako kumekuwa na ongezeko. Idadi ya Madaktari waliosajiliwa
imeongezeka kutoka 1,339 mwaka 2006 hadi 3,133 na Wauguzi kutoka 20,115 mwaka 2007
hadi 34,740 hivi sasa. Aidha, katika kipindi cha miaka 3 iliyopita, tumeajiri wauguzi
8,659na tunatarajia kuajiri wengine 1,152kabla ya Julai, 2014. Tutaendelea kufanya
hivyo mwaka ujao wa fedha na miaka inayofuatia. Hii itasaidia kupunguza mzigo wa kazi
mlio nao sasa hivi ambao mmeutaja kwenye risala yenu.
Ndugu Rais wa Chama cha
Wauguzi; Ndugu Wauguzi;
Kwa upande wa maslahi nako, tumejitahidi kuboresha,
najua bado tunayo kazi kubwa ya kufanya mbele yetu. Bado mishahara ni midogo lakini
hatujafika mwisho, tunaendelea kuboresha. Tumekuwa tunaongeza kila mwaka na tutaendelea
kufanya hivyo mwaka huu na miaka ijayo.
Risala ya Wauguzi Ndugu
Wauguzi,
Nimesikiliza kwa makini risala yenu iliyowasilishwa vizuri na Ndugu
Paul Magesa, Rais wa Chama cha Wauguzi na Wakunga. Namna ambavyo ameiwasilisha, lugha
aliyotumia kuiwasilisha na jinsi mlivyoishangilia inathibitisha kuwa risala hii ni
shirikishi, na yaliyosemwa ni mambo muhimu kwa wauguzi kwa ujumla wenu. Ni risala
iliyosheheni ukweli kuhusu mafanikio tuliyoyapata na mambo yanayowatatiza mnayotaka
yapatiwe ufumbuzi. Kuna ushauri mzuri uliotolewa kuhusu nini kifanyike kuboresha mazingira
ya kazi ya Wauguzi na huduma ya afya nchini. Lazima nikiri kuwa nimeguswa sana na
ahadi yenu ya kuendelea kufanya kazi kwa mujibu wa viapo vyenu, licha ya changamoto
zilizopo.
Napenda kuwahakikishia kuwa Serikali inaelewa mchango wenu muhimu
na inauthamini sana hivyo basi, sisi tutakuwa watu wa mwisho kupuuza mambo ya wauguzi.
Kama kuna jambo halijafanyika haitokani na kupuuza au ukosefu wa dhamira ya kuyashughulikia
bali kuna sababu fulani fulani za msingi zinazotukwaza katika utekelezaji wake.
Nimefurahishwa
sana na dhamira yenu njema ya kutaka kuona mabadiliko yanafanyika katika sekta ya
afya na ninyi kuwa sehemu kamili ya mabadiliko hayo. Ndiyo maana sehemu kubwa ya risala
yenu ina mapendekezo ya mambo ya kubadilisha ili kuboresha utoaji wa huduma ya afya.
Nawaunga mkono kwa msimamo wenu huo. Nimefarijika sana kusikia kutoka Wizara ya Afya
na Ustawi wa Jamii na Wizara nyingine za Serikali kuwa mambo mengine yametekelezwa
na yapo ambayo tunaendelea kuyatekeleza. Hata hivyo, bado yapo mambo ambayo tunayavutia
pumzi kwa maana ya kujenga uwezo wa kuyatekeleza.
Ndugu Wauguzi; Hii ni
mara ya tatu napata nafasi ya kukutana na kuzungumza na viongozi wa Wauguzi. Mara
ya kwanza ilikuwa Mnazi Mmoja mwaka jana, mara ya pili Ikulu tarehe 29 Aprili, 2014
na leo ndiyo mara ya tatu hapa Arusha. Jambo mojawapo muhimu nililojifunza ni kuwa
mambo mengi yanayowatatiza wauguzi, ambayo pia yameainishwa katika risala yenu leo,
yanaweza kumalizwa kwa kuboresha mawasiliano na mahusiano kati yenu na Wizara zinazohusika
na kati yenu (wauguzi) na kada nyingine katika sekta ya afya.
Naamini kama
hayo yakifanyika mambo mengi yatapatiwa ufumbuzi na kwamba yatabaki machache yanayohitaji
msaada wa ngazi za juu. Hii itasaidia kuondoa kutiliana mashaka, kutokuaminiana na
hisia za kupuuzwa kwa wauguzi. Nimeona nitumie fursa ya maadhimisho haya ya leo kutoa
ufafanuzi kwa baadhi ya masuala tuliyozungumza siku zilizopita na yaliyoibuliwa hapa
leo kwenye mabango na risala.
Madai ya Wauguzi
Ndugu Rais wa
Chama cha Wauguzi; Ndugu Wauguzi, Katika risala yenu mmezungumzia mambo yahusuyo
muundo wa utumishi, mafunzo, posho, huduma ya makazi na mambo mengineyo muhimu. Mambo
yote haya ni ya msingi na napenda kuwahakikishia kuwa tutayachukulia kwa uzito unaostahili
na tutayafanyia kazi ipasavyo ili tuwatengenezee mazingira mazuri ya kufanya kazi
zenu.
Muundo wa Utumishi wa Uuguzi Ndugu Rais wa Chama cha Wauguzi; NduguWauguzi;
Kwanza kabisa nawapongeza kwa kukamilisha mapendekezo ya Muundo wa Utumishi. Nitawasaidia
kufuatilia kwa mamlaka husika ili uamuzi ufanyike mapema iwezekanavyo. Kukamilika
kwa zoezi hilo kutatoa ufumbuzi kwa mambo mengi yanayowatatiza hivi sasa. Itayaweka
sawa masuala ya upandishaji wa vyeo. Itawezesha kutambuliwa ipasayo kwa wauguzi wanaomaliza
shahada za uzamili na uzamivu. Kwa kweli nashangaa kwa nini watu waliojiendeleza kiasi
hicho wapate taabu ya kutambuliwa inavyostahili katika utumishi wa uuguzi.
Hivyo
hivyo nashangaa tena napata taabu kuamini kuwa mtumishi akienda masomoni kuongeza
ujuzi anasimama kupanda cheo au hata kushushwa cheo. Haya ni ya kustaajabisha mambo
ambayo hayastahili kufanyika. Naomba Wizara na mamlaka husika zihakikishe kuwa uonevu
huu hauendelei kufanyika. Iweje leo kujiendeleza iwe ni balaa kwa mfanyakazi na mwajiri
badala ya kuwa jambo jema kwa wote.
Ndugu Wauguzi; Nadhani suala la uanzishwaji
wa Kurugenzi ya Uuguzi ndani ya Wizara ya Afya limefikia hatua nzuri. Nimeambiwa kuwa
Wizara iliridhia maombi yenu na kuyawasilisha Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi
wa Umma. Wataalamu wa Mifumo katika Idara Kuu ya Utumishi walichoshauri ni kuwa Sehemu
ya Uuguzi sasa ipandishwe hadhi na kuwa Kitengo cha Uuguzi kitakachoongozwa na Mkurugenzi.
Nimeambiwa pia kwamba Wizara ya Afya imekubali na tayari imefanya marekebisho na kuwasilisha
upya pendekezo hilo. Nimesikia kuwa jambo hili litakamilishwa muda si mrefu na huenda
muundo huo ukaanza tarehe 1 Julai, 2014 hivyo kuhitimisha maombi yenu. Niruhusuni
niwapongeze kwa hatua iliyofikiwa mpaka sasa.
Maslahi ya Watumishi Ndugu
Rais wa Chama cha Wauguzi; Ndugu Wauguzi;
Kuboresha maslahi ya Watumishi
wa Umma, hususan mishahara na posho mbalimbali ni mambo ambayo Serikali imeyapa kipaumbele.
Tumekuwa yunafanya hivyo kila mwaka na tutaendelea kufanya hivyo. Maombi yenu tumeyapokea
na tutayafanyia kazi. Napenda kusema hata katika Bajeti ya mwaka ujao wa fedha hatua
kiasi fulani zitachukuliwa.
Nimesikia kilio chenu kuhusu posho zilizoamuliwa
kutokutekelezwa na ile ya sare za kazi ambayo imeahidiwa na kuongezwa kutoka shilingi
150,000 na kuwa Shilingi 300,000 kutokamilishwa mpaka sasa. Nitatoa maagizo kwa mamlaka
husika katika Serikali kufuatilia na kuwabana, watakaokaidi. Hivyo hivyo, kwa posho
ya kufanya kazi usiku, kama ilishaamuliwa ilipwe, mamlaka husika zitatakiwa kutekeleza
bila ajizi.
Nyumba za Wauguzi
Serikali inatambua umuhimu wa
wauguzi kuwa na makazi karibu na maeneo yao ya kazi. Kwa kutambua umuhimu huo Serikali
imekuwa inatenga fedha za kujenga nyumba za madaktari na wauguzi kila mwaka. Hata
hivyo kasi ya ujenzi ni ndogo ukilinganisha na ukubwa wa mahitaji kwa sababu ya ufinyu
wa bajeti. Tutatafuta njia nyingine za kuharakisha ujenzi wa nyumba hizo. Mipango
hiyo ikikamilika mtaona matokeo yake. Kwa sasa tutaendelea na kazi ya ujenzi wa nyumba
katika mikoa ya Mtwara, Rukwa, Tabora na Mara.
Nimelipokea pendekezo lenu
la kutaka msaidiwe kupata viwanja vya kujenga nyumba. Nitaagiza Wizara ya Ardhi, Nyumba
na Maendeleo ya Makazi wawasaidie. Miaka miwili iliiyopita niliagiza utengenezwe mpango
maalum wa mikopo ya nyumba kwa watumishi wa umma. Matayarisho yanaendelea, ukikamilika
utasaidia wafanyakazi wa umma wakiwemo Wauguzi kujipatia nyumba za kuishi.
Udhamini
wa Mafunzo Ndugu Rais wa Wauguzi; Ndugu Wauguzi,
Nimesikia rai yenu
ya kutaka Serikali itoe udhamini kwa wanafunzi wanaosomea shahada ya kwanza ya uuguzi
kama tunavyofanya kwa wale wanaosomea udaktari. Nakubali maombi yenu, nitaagiza mamlaka
husika walifanyie kazi. Kama hivi sasa wanafunzi hao siyo wengi tunaweza kuanza hata
bajeti ijayo lakini kama ni wengi itabidi tuanze mwaka wa fedha wa 2015/16 lazima
tujipange vizuri kwani inahusu pesa.
Naamini uamuzi huu utahamasisha wauguzi
kujitokeza kwa wingi kujiendeleza kitaaluma. Wauguzi wasiishie kwenye Cheti na Diploma
bali waende zaidi ya hapo. Napenda kuwahakikishia pia kwamba pamoja na uamuzi huu,
Serikali bado itaendelea kudhamini wauguzi wanaosomea shahada ya uzamili na uzamivu
kama tufanyavyo sasa. Nimesikia utayari wenu wa kupewa nafasi za uongozi katika Wizara
ya Afya na kwingineko kama tulivyofanya kwa Mkuu wa Mkoa wa Tanga.
Wito
kwa Wauguzi Ndugu Rais wa Chama cha Wauguzi; Ndugu Wauguzi,
Tunapoadhimisha
siku ya wauguzi, tunakumbuka pia siku ya kuzaliwa kwa Bi. Frorence Nightlingale, mwanzilishi
wa taaluma na fani hii adhimu ya uuguzi. Mama Nightlingale aliyeishi kati ya mwaka
1820 hadi 1910 ndiye aliyeanzisha shule ya kwanza ya wauguzi huko London katika Hospitali
ya Mtakatifu Thomas. Alianzisha huduma hii baada ya uzoefu wake katika kuwashughulikia
majeruhi wa kivita, na wanajeshi wagonjwa wakati wa vita.
Sifa yake kubwa
ilikuwa ni wito na moyo wa kujitolea na huruma vitu ambavyo aliamini ndio misingi
ya kuwa muuguzi. Alipata kunukuliwa akisema, “Kama muuguzi atakacha kutoa huduma kwa
sababu yoyote ile au kusema haimuhusu, basi uuguzi kwake sio wito”. Kutokana na maisha
yake ya kuwaangazia nuru wagonjwa na kuwatembelea usiku akiwa na taa ya kandili kuwafariji
na kuwahudumia, alipewa jina la “Mwanamke Mwenye Kutembea na Nuru”. Ndugu Wauguzi;
Ninyi
ni watu wenye dhamana kubwa juu ya maisha ya watu na mnategemewa sana. Nawapongeza
kwa kazi kubwa na nzuri muifanyayo. Kwa sababu yenu mmeokoa maisha ya watu wengi na
kuwapunguzia maumivu wagonjwa. Wakati mwingine moyo wenu kuonyesha kujali, upendo
na huruma hutoa matumaini kwa mgonjwa na kumrejeshea siha yake. Hivyo, nawaomba muendelee
kuwa na kauli nzuri na nyuso zenye tabasamu na nyoyo za huruma na upendo kwa wagonjwa.
Tabia hiyo ni tiba ya aina yake.
Nimeona niikumbushe hadithi ya muasisi Mama
Florence Nightngale ili kuwaomba wakati wote iwaongoze na muendelee kukumbushana kuizingatia.
Minong’ono kuwa mienendo ya baadhi yenu inalalamikiwa na wagonjwa kuwa hailingani
na mafundisho ya muasisi wa kazi hii adhimu inanisumbua sana. Kama nilivyosema awali,
ninyi ndiyo watu wa kwanza mnaokutana na mgonjwa akifika hospitali na ni watu wa mwisho
anapotoka hospitali baada ya matibabu. Ikiwa mtakuwa na nyuso za ukatili na ulimi
mkali au wa kebehi, mtakuwa mnawakwaza wagonjwa na hata kuongeza ukali wa maumivu
yao. Wengine wanaweza kukata tamaa na hata kupoteza uhai. Msifanye watu wajutie kufika
zahanati au hospitali. Narudia kuwasihi mzingatie kiapo chenu na maudhui ya kauli
mbiu yenu ya kutaka mabadiliko. Kwa maana nyingine naomba mtambue kuwa kauli mbiu
yenu ya mabadiliko inawahusu na nyie pia kama inavyotuhusu sote. Lazima mabadiliko
yaanze na ninyi wenyewe.
Homa ya Dengue
Ndugu Wananchi; Kabla
ya kumaliza hotuba yangu naomba nizungumzie ugonjwa mpya wa Homa ya Dengue uliojitokeza
katika jiji la Dar es Salaam hivi karibuni. Huu si ugonjwa asili kwetu. Ni ugonjwa
wa huko Asia na Bara la Amerika lakini ndiyo umeshafika. Kwa mara ya kwanza ugonjwa
huu ulijitokeza Jijini Dar es Salaam mwaka 2010 na kuathiri watu 40 ambao walipatiwa
matibabu na kupona. Ugonjwa huu ulitoweka lakini ukaibuka tena Mei na Juni, 2013 ulipojitokeza
tena na kuwakumba watu 172.Mwaka huu ugonjwa huo umerudia tena kwa kasi kubwa zaidi.
Kati ya Januari na Aprili 6, mwaka huu wagonjwa 399 wamethibitika kuugua katika Jiji
la Dar es Salaam. Kati ya wagonjwa hao 322 walitoka Wilaya ya Kinondoni, 61 Wilaya
ya Ilala na 16 Wilaya ya Temeke. Kwa bahati mbaya wawili kati yao walipoteza maisha.
Ndugu wananchi;
Wataalamu wa afya wanasema kuna aina tatu za ugonjwa
wa dengue. Aina ya kwanza ni Homa ya Dengue, aina ya pili ni Dengue ya Damu na aina
ya tatu ni Dengue ya Kupoteza Fahamu. Hapa kwetu Homa ya Dengue ndiyo ugonjwa uliothibitika
kuathiri wagonjwa wote. Homa hii ina dalili kubwa tatu: homa kali ya ghafla, kuumwa
kichwa, na maumivu ya viungo au uchovu. Kwa vile dalili za ugonjwa huu zinafanana
sana na dalili za ugonjwa wa malaria, ipo hatari kwa watu waliozoea kutumia dawa bila
kupima kumeza dawa za malaria wakati wanaugua Homa ya Dengue. Wakifanya hivyo watahatarisha
maisha yao. Natoa wito kwa mtu yeyote anayejisikia dalili hizi aende hospitali akapimwe;
asinywe dawa bila kupima kama baadhi yetu tulivyozoea. Ni hatari kwa maisha yetu.
Ndugu
Wananchi; Ugonjwa huu unaambukizwa na mbu aina ya Aedes akishamuuma binadamu.
Tena huuma mchana. Hatua za kupambana na mbu huyu ni sawa na zile zinazochulikuwa
kupambana na mbu wa Anophelesanayeambukiza malaria. Watu waendelee kutumia vyandarua
vilivyotiwa dawa, kupaka dawa za kuzuia kuumwa na mbu na kuharibu maeneo ya mazalia
ya mbu.
Nimetoa maelekezo kwa Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii kuhakikisha
kuwa Bohari Kuu ya Madawa ya Serikali (MSD) wanaleta kits za kupimia maradhi haya
(Dengue Rapid Test Kits) za kutosha na kuzisambaza kwenye hospitali na vituo vya afya.
Nimeambiwa hivi sasa vipimo hivi havipo vya kutosha. Hii ni dharura ya kitaifa ambayo
lazima ipewe uzito na uharaka unaostahili na Wizara ya Afya na Hazina.
Hitimisho Ndugu
Rais wa Chama cha Wauguzi; Ndugu Wauguzi;
Niruhusuni nimalize hotuba yangu
kwa kurudia kuwashukuru kwa kunialika na kwa risala yenu nzuri. Nimejifunza mengi
na kama nilivyosema, nakwenda kuifanyia kazi risala yenu na yote niliyosikia na kuona
yanayohitaji kuchukuliwa hatua. Yale masuala ya kimuundo na mengineyo nitakwenda kuyakwamua
huko yalikokwama, ili utekelezaji uanze. Yale yahusuyo posho, kama nilivyoeleza, baadhi
yake yatashughulikiwa katika bajeti ijayo na mengine tutaendelea kuyashughulikia kadri
uwezo utakavyoruhusu.
Ninachoweza kusema kwa uhakika kabisa ni kuwa tunawapenda,
tunatambua umuhimu wenu na tunawathamini sana. Katu hakuna upungufu wa dhamira bali
tunakwazwa na uwezo mdogo wa mapato ya Serikali kuweza kutosheleza mahitaji yote ya
kuboresha huduma ya afya na maslahi kwa watumishi wa afya nchini. Narudia kusisitiza
kuwa kamwe sio kutokana na kukosekana kwa utayari wa kutatua changamoto zinazowakabili
wauguzi au watumishi wengine wa umma.
Upo ushahidi wa wazi wa juhudi za Serikali
ninayoiongoza ya kufanya mambo mengi makubwa na madogo ya kuboresha mazingira ya kazi
kwa kila kada na sekta kadiri uwezo unavyoruhusu. Mtakubaliana nami kuwa hali ya kada
ya wauguzi ilivyo leo, si sawa na ilivyokuwa miaka 10 iliyopita.
Tumepiga
hatua kiasi chake lakini bado tuna safari ndefu na tutaendelea kufanya zaidi. Ni dhahiri
kwamba tumesogea kutoka pale tulipokuwa, ingawa hatujafika tunapodhamiria kwenda.
Kwa vile msimamo na muelekeo wetu ni sahihi, naamini baada ya muda si mrefu tutafika.
Penye nia pana njia. Inawezekana Timiza Wajibu wako. Mungu Ibariki Afrika, Mungu
Ibariki Tanzania. Asanteni sana kwa kunisikiliza.