2014-05-12 12:18:31

Papa Francisko kinara kwenye mitandao ya kijamii!


Padre Federico Lombardi, msemaji mkuu wa Vatican anabainisha kwamba, mahubiri yanayotolewa na Baba Mtakatifu Francisko walau kila siku wakati wa maadhimisho ya Ibada ya Misa Takatifu kwenye Kikanisa cha Mtakatifu Martha kilichoko mjini Vatican ni chachu ya mageuzi katika mchakato wa mawasiliano ndani ya Kanisa, unaofanywa na Baba Mtakatifu Francisko kwa wakati huu.

Padre Lombardi ameyasema hayo wakati anashiriki katika mjadala kuhusu mageuzi katika nyanja za mawasiliano yanayoendelea kuletwa na Baba Mtakatifu Francisko, ulioandaliwa kwenye Onesho la Vitabu Kimataifa mjini Torino, Kaskazini mwa Italia, mwishoni mwa Juma na Vatican kushiriki kama mgeni wa heshima.

Mahubiri ya Baba Mtakatifu yanawalenga wote wanaotaka kusikiliza Kanisa linasema nini katika maisha yake ya kila siku kadiri ya Neno la Mungu na Maadhimisho ya Fumbo la Ekaristi Takatifu. Huu nimwelekeo mpya wa mawasiliano ndani ya Kanisa na Jamii katika ujumla wake.

Ni kiongozi anayegusa wengi kwa mtindo wake wa maisha na jinsi anavyozungumza kwa kugusa undani wa maisha ya mwanadamu, kwake, mawasiliano ni njia mahususi inayomwezesha mtu kukutana na jirani zake, ili kujenga umoja na mshikamano. Baba Mtakatifu ni kinara wa mawasiliano katika masuala ya imani katika mitandao ya mawasiliano kijamii.

Baba Mtakatifu Francisko anajitahidi kushirikisha mang'amuzi na uzoefu wake kwa kukutana na kuzungumza na watu, kwa njia ya mahubiri na hotuba zake mbali mbali.







All the contents on this site are copyrighted ©.