2014-05-12 09:59:55

Maboresho ya maisha Seminarini


Baraza la Maaskofu Katoliki Chile katika mkutano wake wa 107 uliofunguliwa hapo tarehe 5 na kuhitimishwa tarehe 10 Mei 2014, limejadili kwa kina na mapana kuhusu hali ya miito ya Kipadre na Kitawa pamoja na kuangalia hali ya Seminari zake, kama sehemu ya mkakati mkubwa wa maboresho unaopaniwa kutekelezwa na Maaskofu nchini Chile, kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya Kanisa. Imekuwa ni fursa ya kuangalia hali ya Chile katika ujumla wake. RealAudioMP3

Baraza la Maaskofu Katoliki Chile linasema, kuna haja kwa waamini kutolea ushuhuda angavu wa maisha yanayojikita katika imani, maadili na utu wema, ili kuwaonjesha wale wasioamini umuhimu wa kukutana, kutembea na kumkubali Yesu kuwa ni Mwalimu na Bwana katika maisha. Hii ni changamoto ambayo imetolewa na Askofu mkuu Ivo Scapolo, Balozi wa Vatican nchini Chile katika hotuba yake ya ufunguzi ambayo pia aliwasilisha salam na matashi mema kutoka kwa Baba Mtakatifu Francisko kwa Maaskofu hawa.

Maaskofu wameangalia pia utekelezaji wa Mpango wa shughuli za kichungaji nchini Chile kuanzia Mwaka 2014 hadi Mwaka 2020, unaoongozwa na kauli mbiu “Kanisa linalosikiliza, linalotangaza na kuenzi”. Maaskofu pia wamepembua kwa kina na mapana changamoto mbali mbali zinazojitokeza katika maisha na utume wa Kanisa hususan kuhusu: Mihimili mikuu ya Uinjilishaji, Elimu, Mikakati ya kichungaji katika masuala ya kijamii; Huduma na Mawasiliano.

Mkutano huu umefungwa kwa Ibada ya Misa Takatifu ya kuwaweka wakfu Maaskofu wapya wasaidizi wa Jimbo kuu la Santiago. Hawa ni: Askofu Fernando Ramos na Askofu Galo Fernandes.








All the contents on this site are copyrighted ©.