2014-05-11 09:13:34

Kanisa lina thamini shule!


Baraza la Maaskofu Katoliki Italia, Jumamosi, tarehe 10 Mei 2014 limeadhimisha Siku kuu ya shule nchini Italia kwa kukutana na Baba Mtakatifu Francisko kwenye Uwanja wa Kanisa kuu la Mtakatifu Petro mjini Vatican. Zaidi ya watu laki tatu walifurika kwenye Uwanja wa Mtakatifu Petro na viunga vyake kushudia kwa mara nyingine tena, Kanisa likihimiza umuhimu wa shule kama hija ya majiundo ya mtu mzima: kiroho na kimwili, dhana ambayo vijana wa kizazi kipya wanapaswa kurithishwa kwa ukamilifu zaidi.

Tukio hili limewawezesha watu kusikia shuhuda mbali mbali zilizotolewa na watu maarufu kutoka Italia jinsi ambavyo wameweza kufanikiwa katika maisha yao kwa kukazia: umuhimu wa mtu kujiwekea malengo katika maisha na kujisadaka ili kuweza kufanikisha malengo haya kwa kutambua kwamba, katika maisha hakuna njia ya mkato na kama ipo, hiyo ni njia itakayomwachia mtu madonda ya kudumu. Kuna haja ya kukazia tunu msingi za maisha ya kiroho na kimwili; uaminifu, ukweli, uwazi na udumifu pamoja na kuwa na matumizi sahihi ya vyombo vya habari kama mahali pa kukutana na watu ili kujiendeleza zaidi.

Kardinali Angelo Bagnasco, Rais wa Baraza la Maaskofu Katoliki Italia anasema kwamba, sekta ya elimu nchini Italia inakabiliwa na matatizo makubwa yanayojikita katika miundo mbinu, hali ambayo wakati mwingine inakatisha tamaa. Lakini ikumbukwe kwamba, shule ni mahali ambapo mtu anafundwa kuwa na upembuzi yakinifu katika maisha yake; kwa kutambua kanuni maadili pamoja na kuendelea kuwa wazi kwa mawazo mbali mbali yanayoendelea kujitokeza. Hapa ni mahali ambapo wanafunzi wanapaswa kutafuta na kupata ukweli, wema na uzuri.

Baraza la Maaskofu Katoliki Italia katika mikakati yake ya kichungaji kwa kipindi cha miaka kumi, linatoa kipaumbele cha kwanza katika sekta ya elimu kama sehemu ya mchakato wa Uinjilishaji, ili kuwawezesha waamini kufanya mageuzi ya ndani, kwa kujenga utamaduni wa kukutana na kuthaminiana ili hatimaye kutambua ukweli. Kanisa Katoliki nchini Italia limechangia kwa kiasi kikubwa katika maendeleo ya sekta ya elimu, ndiyo maana linaendelea kutoa changamoto ya kuwekeza zaidi katika sekta ya elimu kwa ajili ya vijana wa kizazi kipya, kwani hii ni haki yao msingi.

Kardinali Bagnasco anasema, wazazi wanayo haki ya kuchagua mfumo na mahali ambapo watoto wao wanaweza kupata elimu bora zaidi, kama inavyobainishwa na Katiba ya nchi. Baraza la Maaskofu Katoliki Italia linamshukuru Baba Mtakatifu Francisko kwa kuwasaidia waamini kukua kiumri, hekima na neema, inayobubujika kutoka katika kweli za Kiinjili.

Naye Waziri wa Elimu nchini Italia Bibi Stefania Giannini anasema, kwake tukio hili halitaweza kufutika kwa urahisi moyoni mwake, kupata nafasi ya kuzungumza mbele ya Baba Mtakatifu pamoja na kusikilizwa na umati mkubwa wa watu uliokuwa umefurika kwenye Uwanja wa Kanisa kuu la Mtakatifu Petro.

Hii inaonesha kwamba, kuna haja ya kuwaelimisha wanafunzi kutambua na kuheshimu umuhimu wa shule na kazi na kwamba, shule uwe ni mfumo unaowashirikisha wengi. Shule ni kwa ajili ya mafao ya wengi, changamoto ya kuendeleza mshikamano wa dhati pamoja na kuongeza rasilimali watu na fedha ili kufanikisha mikakati ya elimu.

Baba Mtakatifu Francisko, Jumamosi jioni alitumia dakika 45 kuzunguka na kuzungumza na wanafunzi, wazazi na waalimu waliokuwa wamefurika kwenye Uwanja wa Kanisa kuu la Mtakatifu Petro. Katika hotuba yake, ameonesha mambo makuu matatu yanayomfanya kupenda shule: yaani shule inamwezesha mtu kuuona ukweli; ni mahali pa kukutana na kwamba, hapa ni mahali ambapo mtu anafundwa kufahamu kilicho kweli, chema na kizuri.

Baba Mtakatifu mwishoni, alitumia fursa hii kusalimiana na wanafunzi na walimu wagonjwa na baadaye akarudi kwenda kijipumzisha baada ya pilika pilika za siku nzima!







All the contents on this site are copyrighted ©.