2014-05-11 15:08:29

Familia ya Mungu inawajibika kukuza na kuendeleza miito!


Baba Mtakatifu katika tafakari yake wakati wa Sala ya Malkia wa mbingu, Jumapili ya Kristo mchungaji mwema sanjari na maadhimisho ya siku ya 51 ya kuombea miito mitakatifu anasema, Yesu Kristo ndiye mchungaji mwema anayeonesha upole, unyenyekevu, ufahamu; kiongozi anayethubutu kuyamimina maisha yake kwa ajili ya Kondoo wake, ili waweze kupata utimilifu wa maisha. Huu ndio uhusiano unaopaswa kuoneshwa kati ya Wakristo na kama kielelezo cha mahusiano ya kibinadamu.

Yesu Kristo ndiye mchungaji wa kweli, anayewakirimia waja wake utimilifu wa maisha, mwaliko kwa kila mwamini kuwa na imani kwa Kristo anayewaongoza, kwa kumsikiliza wakati anapozungumza nao kutoka katika dhamiri zao nyofu, daima mioyo yao ikiwa wazi tayari kusikiliza Neno lake, ili kulisha imani na kuangazia dhamiri zao, ili hatimaye, waweze kufuata mafundisho yake kikamilifu.

Baba Mtakatifu anasema, kwa namna ya pekee, waamini wanaalikwa kusali kwa ajili ya kuwambea Mapadre wapya kumi na watatu waliopadrishwa siku ya Jumapili, kwenye Kanisa kuu la Mtakatifu Petro mjini Vatican, ili waweze kuwa kweli ni waaminifu kwa Kristo Mwalimu na viongozi wenye hekima na angavu kwa watu wa Mungu waliokabidhiwa kwao. Wajitahidi kumwiga Kristo anayewaonesha njia na matumaini kwa watu wake, ili aweze kuwa karibu zaidi kwa watu wake kwa njia ya huruma pamoja na kuwasaidia wale waliochoka na kudhohofu.

Baba Mtakatifu Francisko anasema kwamba, Kanisa linaadhimisha Siku ya 51 ya Kuombea Miito mitakatifu, changamoto ya kila mtu kutoka katika ubinafsi wake, ili kujiunga na Yesu pamoja na Injili yake, kwa kumfuasa Kristo katika furaha sanjari na kutekeleza dhamana waliyokabidhiwa na Mama Kanisa, ili kujenga urafiki wa dhati na kujitosa kimasomaso bila ya kujibakiza.

Baba Mtakatifu anawaalika waamini kusali zaidi katika nyakati hizi ambamo sauti ya Kristo Mchungaji mwema inafifishwa na kwamba, Familia ya Mungu iwajibike zaidi katika kukuza na kuhamasisha miito mitakatifu, kwa kufahamu na kujiamini. Baba Mtakatifu amewaweka wote chini ya ulinzi na usimamizi wa Bikira Maria, ili aweze kuendelea kuhamasisha miito mbali mbali ndani ya Kanisa







All the contents on this site are copyrighted ©.