2014-05-10 10:24:22

Umoja wa Mataifa wamwalika Papa Francisko mjini New York!


Kwa niaba ya Familia ya binadamu wote, Katibu mkuu wa Umoja wa Mataifa Bwana Ban Ki-Moon amemshukuru Baba Mtakatifu Francisko, Ijumaa tarehe 9 Mei 2014 kwa kuwapatia fursa ya kuweza kuzungumza na wakurugenzi wakuu wa mashirika yanayosimamiwa na Umoja wa Mataifa, waliokuwa wanafanya mkutano wao wa kupanga mikakati ya Umoja wa Mtaifa mjini Roma.

Mkutano huu hufanyika mara mbili kwa mwaka ili kwa pamoja waweze kujadili dhamana yao katika medani za kimataifa, kulinda amani pamoja na kuweka mikakati ya maendeleo endelevu. Kama Familia ya Umoja wa Mataifa wanakabiliana na changamoto nyingi kama vile: ongezeko kubwa la ukosefu wa usawa na haki; hali ya watu kutovumiliana kwa misingi ya kidini pamoja na vita inayoendelea kusababisha maafa makubwa kwa wananchi wanaoishi: Jamhuri ya Watu wa Afrika ya Kati, Sudan ya Kusini, Syria na Ukraine ambako hali bado ni tete sana!

Katibu mkuu wa Umoja wa Mataifa anasema kwamba, dunia inaendelea kuguswa na athari za mabadiliko ya tabianchi, hali ambayo itakuwa na madhara makubwa kwa vizazi vijavyo, ndiyo maana Umoja wa Mataifa unaandaa mkutano wa kimataifa utakaojadili kwa kina na mapana athari za mabadiliko ya tabianchi ili kuibua mbinu mkakati wa kupambana na hatimaye, kudhibiti athari zake. Umoja wa Mataifa unaendelea na kampeni yake ili kuhakikisha kwamba walau Malengo ya Maendeleo ya Millenia kwa Mwaka 2015 yanafikiwa.

Katibu mkuu wa Umoja wa Mataifa anasema, hapa kunahitajika, uvumilivu, ujasiri, ushirikiano pamoja na kuguswa na mahangaiko ya watu. Baba Mtakatifu Francisko katika hotuba yake kwa Katibu mkuu wa Umoja wa Mataifa na wakurugenzi wa Mashirika ya Umoja wa Mataifa alisema kwamba, kanuni hizi msingi ni dira na mwongozo wa watu wote. Umoja wa Mataifa unamshukuru na kumpongeza Baba Mtakatifu Francisko katika jitihada zake za kupambana na umaskini duniani kwa kujielekeza katika mikakati ya maendeleo endelevu.

Umoja wa Mataifa anasema, Katibu mkuu una matumaini makubwa na utaendelea kushirikiana na Kanisa Katoliki katika kulinda na kudumisha utu na heshima ya binadamu. Mwishoni, Bwana Ban Ki-Moon alitumia fursa hii kumkaribisha rasmi Baba Mtakatifu Francisko kutembelea Makao Makuu ya Umoja wa Mataifa, New York, Marekani, kwani hii inaweza kuwa ni fursa kwa Baba Mtakatifu kuweza kushirikisha mwono na matumaini yake kwa binadamu.

Akigusia hija ya Baba Mtakatifu Francisko nchini Korea, mahali alipozaliwa Katibu mkuu wa Umoja wa Mataifa Bwana Ban Ki-Moon anasema kwamba, ana matumaini kuwa Baba Mtakatifu atawapelekea ujumbe wa amani, utakaosaidia kuponya na kuendeleza mchakato wa upatanisho kati ya Korea ya Kaskazini na Korea ya Kusini.







All the contents on this site are copyrighted ©.