2014-05-10 11:30:17

Mwaka mmoja tangu Papa Tawadros II alipokutana na Baba Mtakatifu Francisko!


Baba Mtakatifu Francisko amemwandikia barua ya shukrani Patriaki Tawadros II, wa Kanisa la Kiorthodox la Alexandria, Misri, anapokumbuka mwaka mmoja tangu walipoonana mjini Vatican tarehe 10 Mei 2013, kama kielelezo cha kuimarisha umoja na mshikamano kati ya Makanisa, mchakato ulionzishwa na Papa Paulo VI pamoja na Papa Shenouda III kunako mwaka 1973.

Katika barua hii Baba Mtakatifu Francisko anaangalia mchakato wa upatanisho na urafiki ambao Makanisa haya yamefanya kwa pamoja. Kwa msaada wa Mwenyezi Mungu wameendelea kufahamiana na hivyo kuvuka vizingiti vya kutoelewana vilivyojengeka katika historia, kiasi kwamba Makanisa haya yanaanza kuonja cheche za umoja ambao hata hivyo haujakamilika.

Baba Mtakatifu anasema, kwa njia ya majadiliano katika upendo pamoja na uaminifu wataweza kumaliza tofauti ambazo bado ziko miongoni mwao, ili kufikia umoja kamili. Baba Mtakatifu anakumbuka ile sala ya pamoja waliyosali alipokuwa mjini Roma na kwamba, waendelee kusindikizana kwa njia ya sala kama watoto wa Mungu, waliozaliwa katika Maji na Roho Mtakatifu na hivyo kupata mwanga wa imani, ili wote wawe wamoja.

Baba Mtakatifu anapenda kumhakikishia Patriaki Tawadros II sala zake kwa ajili ya Wakristo huko Misri na Mashariki ya Kati katika ujumla wake, ili waweze kupata amani ya kudumu.







All the contents on this site are copyrighted ©.