2014-05-10 09:59:06

Hongera Askofu Moses Hamungole!


Daraja ni Sakramenti ambayo kwayo utume uliokabidhiwa na Kristo kwa mitume wake huendelea kutekelezwa katika Kanisa hadi mwisho wa nyakati: hivyo hii ni Sakramenti ya huduma ya kitume na ina ngazi tatu: Uaskofu, Upadre na Ushemasi. Hawa ni walimu wa Kanisa wanaotekeleza dhamana yao katika utendaji wa kawaida wa Kanisa. Ushemasi ni ngazi ya huduma. RealAudioMP3

Mababa wa Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican wanasema kwamba utimilifu wa Sakramenti ya Daraja hutolewa kwa njia ya wakfu wa kiaskofu, ambao kimsingi ni ukuhani mkuu, yaani kilele cha huduma takatifu. Askofu ana kazi kuu tatu: kuongoza, kutakasa na kuwafundisha watu wa Mungu. Kwa maneno mengine, Askofu ni mwalimu, mchungaji na kuhani. Askofu ana dhamana kwa Kanisa mahalia lakini pia anajishughulisha kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya Kanisa zima.

Fumbo la Ekaristi Takatifu linaloadhimishwa na Askofu lina maana ya pekee kabisa kwani ni ishara ya Kanisa lililounganika kuizunguka Altare, chini ya yule ambaye kwa namna inayoonekana anamwkilisha Kristo, Mchungaji Mwema na Kichwa cha Kanisa lake.

Kwa tafakari hii inayoletwa kwako na Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican, inatupatia nafasi ya kumshukuru Mungu kwa zawadi ya Askofu Moses Hamungole wa Jimbo Katoliki Monze, Zambia, aliyewekwa wakfu na hatimaye kusimikwa kuwa ni Askofu wa Monze hivi karibuni, katika Ibada ya Misa Takatifu iliyoongozwa na Askofu mstaafu Emilio Patriarca wa Jimbo Katoliki Monze, Zambia na kuhudhuriwa na umati mkubwa wa Familia ya Mungu kutoka ndani na nje ya Jimbo Katoliki la Monze.

Askofu Raymond Mpezele wa Jimbo Katoliki Livingstone katika mahubiri yake wakati wa kumweka wakfu Askofu Moses Hamungole ameitaka Familia ya Mungu Jimbo Katoliki Monze, kumpokea na kumwonesha ushirikiano wa dhati, Askofu Hamungole, pamoja na kuendelea kumsindikiza katika maisha na utume wake kwa njia ya sala na sadaka yao ya kila siku. Amemtaka Askofu Hamungole, kumwachia nafasi Roho Mtakatifu ili aweze kumwongoza katika hekima na busara, katika imani na mapendo kwa ajili ya sifa na utukufu wa Kanisa la Kristo.

Askofu raymond Mpezele amemwomba, Askofu Hamungole kuwa na ujasiri pamoja na kujiaminisha kwa Yesu Kristo ambaye ni Bwana wa mavuno na daima aendelee kumwambia kwa njia ya maisha na matendo yake, "Bwana kaa nasi" kama walivyofanya wale wanafunzi wa Emmau, waliokuwa wamesikitishwa sana kutokana na mateso na kifo cha Kristo, kiasi kwamba, matumaini yao yalianza kuyeyuka kama mshumaa! Lakini walipokutana na Yesu Mfufuka, akawafafanulia Maandiko Matakatifu na kuumega Mkate pamoja nao, wakamtambua na hapo wakajawa furaha, nguvu na ari mpya kiasi cha kurudi tena Yerusalemu ili kutangaza ufufuko wa Kristo.

Naye Askofu mstaafu Emilio Patriarca wa Jimbo Katoliki Monze, ameishukuru Familia ya Mungu Jimboni humo kwa ushirikiano mkubwa waliomwonesha wakati wote alipokuwa anawahudumia kama Askofu na kwamba, wanastahili kupendwa na kuheshimiwa.

Askofu Moses Hamungole amemshukuru Mwenyezi Mungu na Baba Mtakatifu Francisko kwa kumteuwa kuwa Askofu wa Jimbo Katoliki Monze, hata bila mastahili yake. Amemwomba Askofu mkuu Julio Murat, Balozi wa Vatican nchini Malawi na Zambia kumfikishia Baba Mtakatifu Francisko salam zake za shukrani. Amewashukuru Maaskofu Emilio Patriarca, George Lungu na Raymond Mpezele waliomweka wakfu na kuwa Askofu mpya wa Jimbo Katoliki Monze.

Askofu Hamungole amemshukuru kwa namna ya pekee Askofu mkuu Telesphor Mpundu wa Jimbo kuu la Lusaka, Zambia kwa ushirikiano mkubwa aliomwonesha alipokuwa Padre wa Jimbo la Lusaka. Anawaomba waamini wa Jimbo Katoliki Monze kushirikiana na kushikamana na kutembea kwa pamoja ili kujenga Kanisa na kumshuhudia Kristo kwa njia ya imani tendaji. Waamini wote wanaalikwa na Kristo kushiriki kikamilifu katika kutangaza Injili ya Furaha.

Askofu Hamungole anasema, anapenda kujiweka chini ya ulinzi na usimamizi wa Roho Mtakatifu ili aweze kuwasaidia kupambanua mahitaji na vipaumbele kwa ajili ya maisha na utume wa Kanisa Jimbo Katoliki Monze! Mipango na mikakati itafanywa kwa kuishirikisha mihimili mikuu ya Uinjilishaji pamoja na kuendelea kusoma alama za nyakati.

Itakumbukwa kwamba, Askofu Moses Hamungole alizawali miaka 47 iliyopita na baada ya masomo na majiundo yake ya Kikasisi, akapdrishwa kunako mwaka 1994. Katika maisha yake kama Padre amewahi kuwa Mkurugenzi wa Kituo cha Televisheni cha Jimbo kuu la Lusaka, Zambia. Aliwahi kuteuliwa kuwa Katibu wa Idara ya Mawasiliano ya Shirikisho la Mabaraza ya Maaskofu Katoliki Afrika Mashariki na Kati, AMECEA na wakati huo huo, alikuwa ni Rais wa SIGNIS, Afrika. Kabla ya kuteuliwa kwake kuwa Askofu wa Jimbo la Monze, Zambia, alikuwa ni Mkuu wa Idara ya Idhaa ya Kiingereza na Kiswahili ya Radio Vatica.

Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican inamtakia kheri na baraka katika maisha na utume wake mpya kama Askofu wa Jimbo Katoliki Monze, Zambia.

Imeandaliwa na
Padre Richard A. Mjigwa.
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.







All the contents on this site are copyrighted ©.