2014-05-09 07:22:21

Mashemasi 13 kupewa Daraja Takatifu la Upadre mjini Vatican


Baba Mtakatifu Francisko, Jumapili tarehe 11 Mei 2014, Siku ya kuombea miito, anatarajiwa kutoa daraja takatifu la Upadre kwa Mashemasi 13 kutoka Jimbo kuu la Roma. Mashemasi hawa walipata bahati ya kukutana na kuzungumza na Baba Mtakatifu Francisko tarehe 25 Aprili 2014, ili kuwafahamu kabla ya kuwapadrisha.

Monsinyo Guido Marini, mshereheshaji mkuu wa Ibada za Kipapa ametoa ratiba elekezi za Ibada mbali mbali zinazotarajiwa kuadhimishwa na Baba Mtakatifu Francisko kwa Mwezi Mei, 2014, mwezi uliotengwa maalum kwa ajili ya Ibada kwa Bikira Maria.

Baba Mtakatifu Jumapili tarehe 11 Mei 2014, Jumapili ya nne ya Pasaka, Siku ya hamsini na moja ya kuombea miito mitakatifu ndani ya Kanisa inayoongozwa na kauli mbiu “Miito, ushuhuda wa ukweli” anatarajiwa kuadhimisha Ibada ya Misa Takatifu kwenye Kanisa kuu la Mtakatifu Petro mjini Vatican sanjari na kutoa Daraja Takatifu la Upadre. Ibada hii ya Misa Takatifu inatarajiwa kuanza majira ya saa 3:30 kwa saa za Ulaya.

Jumapili tarehe 18 Mei, 2014, Baba Mtakatifu Francisko anatarajiwa kutembelea Parokia ya Madhabahu ya Bikira Maria wa Upendo wa Mungu au kama inavyojulikana kwa wenyeji “Santa Maria del Divino Amore”. Hija hii ya kichungaji itafanyika majira ya saa 10: 00 Jioni kwa saa za Ulaya.

Ili wote wawe wamoja ndiyo kauli mbiu inayoongoza Hija ya kitume ya Baba Mtakatifu Francisko katika Nchi Takatifu kuanzia tarehe 24 hadi tarehe 26 Mei 2014, kama sehemu ya Maadhimisho ya Jubilee ya Miaka 50 tangu Papa Paulo VI alipokutana na kusali pamoja na Patriaki Anathegoras wa Yerusalemu, tarehe 5 Januari 1964.

Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican itaendelea kukushirikisha yale yanayojiri katika maisha na utume wa Kanisa. Kwa wale wenye haraka zao, wanaweza kutembelea kwenye mtandao wa Radio Vatican kwa habari zaidi.








All the contents on this site are copyrighted ©.