2014-05-08 11:48:50

Hija ya Baba Mtakatifu Nchi Takatifu!


Familia ya Mungu huko Jordan inaendelea na maandalizi kamambe kwa ajili ya hija ya kichungaji ya Baba Mtakatifu Francisko kuanzia tarehe 24 hadi tarehe 26 Mei, 2014, itakayomwezesha Baba Mtakatifu kutembelea: Yordan, Palestina na Israeli. RealAudioMP3

Katika wimbo rasmi kwa ajili ya mapokezi ya Baba Mtakatifu, waamini kutoka Jordan wanamwimbia Mwenyezi Mungu kwamba, ni mwingi wa huruma na mapendo, amlinde na kumwongoza Papa Francisko anapotembelea Nchi Takatifu, mahali alipozaliwa Yesu, akabatizwa, akafundisha, akateswa, akafa na kufufuka kutoka katika wafu.

Wanamwomba Mwenyezi Mungu awe pamoja na Papa Francisko, ambariki na kumlinda kila hatua atakayofanya kati ya ndugu zake katika imani, ili kwamba, hija yake ya maisha ya kiroho, iwawezeshe watu wengi zaidi kumwona mwalimu mwenye busara na kiongozi mnyenyekevu. Wanaomba ili hija ya kichungaji ya baba Mtakatifu iwe kweli ni chemchemi ya haki, amani na utulivu huko Mashariki ya kati.

Waamini wanasali sala hii kila siku na wakati wote waamini wanapokutana katika Ibada, Liturujia au mkutano. Huu ni mkazo ambao umetolewa na Askofu mkuu Maroun Lahham wa Jimbo kuu la Amman, Yordan. Waamini katika mwezi Mei, uliotengwa maalum kwa ajili yak usali Rozari takatifu, wanamkumbuka na kumwombea Baba Mtakatifu Francisko, ili Bikira Maria aweze kumwongoza katika hija yake ya maisha ya kiroho. Hivi ndivyo waamini kutoka Yordan wanavyoendelea kujiandaa kiroho kwa ajili ya hija ya kichungaji itakayofanywa na Baba Mtakatifu Francisko huko Mashariki.

Katika sala na nia zao, wanaendelea pia kusali kwa ajili ya kuombea umoja na mshikamano miongoni mwa Wakristo, kama kielelezo cha kukoleza ushuhuda wa pamoja katika mchakato wa Uinjilishaji mpya. Patriaki Bartolomeo wa kwanza wa Costantinopoli atakutana na kusali pamoja na Baba Mtakatifu Francisko, kama sehemu ya kumbu kumbu endelevu ya hija ya kichungaji iliyofanywa na Papa Paulo VI kwa kukutana na kusali na Patriaki Anathegoras wa Yerusalemu. Ili wote wawe wamoja ndiyo kauli mbiu inayoongoza hija ya kitume ya Baba Mtakatifu Francisko katika Nchi Takatifu.

Waamini wanaendelea kusali, ili kwamba, mkutano kati ya Baba Mtakatifu na viongozi mbali mbali wa Serikali na Siasa, uweze kuamsha tena ari na moyo mpya wa kutaka kujikita katika ujenzi wa misingi ya haki, amani na utulivu kati ya watu. Wanamwombea Baba Mtakatifu ili aweze kuwaimaarisha ndugu zake katika imani na kuwakirimia utambulisho wa Kikristo wanaopaswa kuutolea ushuhuda hata katika mazingira magumu kama ya kwao!

Usuhuda uoneshe Fumbo la Pasaka, yaani mateso, kifo na ufufuko wa Kristo; matumaini kwa wakimbizi, wahamiaji na watu wasiokuwa na makazi ya kudumu, bila kuwasahau maskini na wote wanaosukumizwa pembezoni wa jamii.








All the contents on this site are copyrighted ©.