Baba Mtakatifu Francisko amemteua Askofu Bernadin Mfumbusa wa Jimbo Katoliki Kondoa
kuwa msimamizi wa kitume wa Jimbo Katoliki la Dodoma, baada ya Baba Mtakatifu kumhamisha
Askofu Gervas Nyaisonga kwenda Jimbo Katoliki la Mpanda na kusimikwa rasmi tarehe
4 Mei 2014 katika Ibada iliyoongozwa na Askofu mkuu Francisco Montercillo Padilla,
Balozi wa Vatican nchini Tanzania.
Baba Mtakatifu Francisko katika salam zilizosomwa
kwa niaba yake na Askofu mkuu Padilla anamtakia utume mwema unaosimikwa katika utii
na unyenyekevu na majitoleo kwa ajili ya Familia ya Mungu Jimboni Mpanda. Anawaalika
waamini na watu wote wenye mapenzi mema, kumpokea na kushirikiana na Askofu Gervas
Nyaisonga kwa mikono miwili, ili aweze kutekeleza utume wake wa kufundisha, kuongoza
na kuwatakatifuza watu wa Mungu kwa ari na moyo mkuu. Waamini wamchukulie si tu kama
mchungaji mwema, bali kama baba na rafiki katika Parokia na nyumba zao.
Baba
Mtakatifu anamtaka Askofu Nyaisonga kujitoa bila ya kujibakiza pamoja na kuendelea
kujibidisha kuwatafuta Kondoo, lakini hasa zaidi wale walipotea, ili kuwasaidia tena
kurudi nyumbani, ili waonje huruma na upendo wa Mwenyezi Mungu. Kama Askofu aendelee
kutoa faraja kwa wale waliokatika shida na magumu ya maisha kwa kuendelea kutekeleza
utume ulioanzishwa na Yesu wa kuwahubiria watu Habari Njema ya Wokovu, kwa kupita
katika miji na vijiji vya watu.
Familia ya Mungu Jimbo Katoliki Mpanda inapaswa
kuguswa na huruma na upendo wa Mungu kutokana na majitoleo yanayooneshwa na Askofu
Nyaisonga. Bila shaka ataendelea kuwa ni Msamaria mwema, kwa kuwasikiliza, kuwahudumia
na kuwaganga waamini wa Jimbo Katoliki Mpanda: kiroho na kimwili. Amewataka waamini
kujiruhusu kufundwa na Yesu kwa kusikiliza Neno la Mungu, maisha ya sala na maadhimisho
ya Sakramenti za Kanisa, lakini zaidi Sakramenti ya Ekaristi takatifu inayopaswa kuadhimishwa
kwa uchaji na ibada.
Kwa njia ya maadhimisho haya Mwenyezi Mungu atatukuzwa
na mwanadamu kutakatifuzwa; upendo na udugu vitaweza kujengeka na kushamiri kati ya
watu na kwamba, kwa njia ya Ekaristi waamini wa Jimbo Katoliki Mpanda wanaweza kujitoa
bila ya kujibakiza kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya Kanisa.
Baba Mtakatifu
katika salam zake, amemshukuru Askofu Damian Kyaruzi wa Jimbo Katoliki Sumbawanga
kwa kulisimamia Jimbo Katoliki la Mpanda hadi wakati huu linapopata mchungaji mkuu.
Askofu
Kyaruzi katika mahubiri yake, amewataka waamini wa Jimbo Katoliki Mpanda kuwa na imani
thabiti na kamwe wasikate tamaa. Askofu Nyaisonga atawasindikiza kwa njia ya Neno
la Mungu na Sakramenti za Kanisa pamoja na mashauri yake ya kibaba!
Askofu
Tarcisius Ngalalekumtwa, Rais wa Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania, amemtaka Askofu
Nyaisonga kusindikizwa na mang’amuzi makuu, busara na hekima, ili kuendeleza na kuboresha
yale yaliyoanzishwa na mtangulizi wake. Ameitaka Familia ya Mungu kumpatia ushirikiano
wa dhati, ili Askofu Nyaisonga aweze kutekeleza wajibu wake barabara katika mchakato
wa uinjilishaji.
Mkuu wa mkoa wa Katavi Dr. Rajabu Lutengwa, kwa niaba ya Serikali
ameahidi kutoa ushirikiano wa dhati kwa Askofu Nyaisonga katika utekelezaji wad hamana
na utume wake Jimboni Mpanda, ili kuendeleza mipango na mikakati ya maendeleo ya watu
kiroho na kimwili. Mkoa wa Katavi kuna fursa nyingi za maendeleo, ambazo zikitumika
barabara zitakuwa ni msaada mkubwa kwa wananchi wa Mpanda na Katavi katika ujumla
wake.
Mama Tunu Pinda, mke wa Waziri mkuu wa Tanzania amelishukuru Kanisa
kwa kuwapatia tena mchungaji mkuu baada ya kifo cha Askofu Paschal Kikoti. Amewataka
waamini kuendelea kujikita katika sala bila kutoa nafasi kwa Shetani ambaye anaweza
kulisambaratisha Kanisa.