2014-05-07 07:01:43

Tamasha la Pasaka, Jimbo Katoliki Moshi!


Mama Kanisa anaendelea kuwekeza katika utume kwa vijana wa kizazi kipya kwa kuwataka kushiriki kikamilifu katika maisha na utume wa Kanisa, hasa wakati huu Mama Kanisa anapoendelea kujielekeza katika Uinjilishaji Mpya unaogusa mahitaji ya mtu mzima. RealAudioMP3

Anawataka vijana kulifahamu Neno la Mungu, Sakramenti za Kanisa, Mafundisho Jamii ya Kanisa pamoja na kujikita katika maisha ya sala, kama njia ya kuzungumza na kujadiliana na Mwenyezi Mungu.

Vijana wanahimizwa kujenga na kudumisha: Imani, matumaini, mapendo na urafiki na Kristo kwani, kamwe hatawadanganya wala kuwatelekeza katika matumaini na mahangaiko yao ya ndani. Baba Mtakatifu Francisko anawahamasisha vijana kufanya tafakari ya Heri za Mlimani kwani haya ni Mafundisho Makuu ya Yesu aliyoyatoa pale kando la Ziwa la Galilaya.

Mlimani kadiri ya Maandiko Matakatifu ni mahali pa ufunuo ambako Mwenyezi Mungu anapenda kukutana na watu wake. Yesu anatumia fursa hii ili kuwashirikisha wafuasi wake chemchemi ya maisha, kwa kujifunua kama Mwalimu na Musa mpya.

Hii ndiyo changamoto iliyowakutanisha Vijana Wakatoliki 850 kutoka katika shule za Sekondari 90 zilizoko Jimbo Katoliki la Moshi, wakati wa maadhimisho ya Tamasha la Pasaka kwa mwaka 2014. Vijana wanapaswa kutambua kwamba, wito ni mwaliko na zawadi kubwa kutoka kwa Mwenyezi Mungu, ambayo inapokelewa na kumwilishwa katika hali ya neema, kwa kupenda na kukumbatia wito huo. Ni maneno yaliyotolewa na Padre Mathew Mushi kutoka Jimbo Katoliki Moshi wakati alipokuwa anazungumza na vijana wakatoliki kutoka Jimbo Katoliki la Moshi.

Vijana wamekumbushwa kwamba, wito wa ndoa ni msingi wa miito mingine yote ndani ya Kanisa. Miito ya upadre na maisha ya kitawa ni maalum kwa ajili ya huduma kwa Familia ya Mungu. Mapadre na watawa wanapaswa kuonesha mifano bora ya maisha, kama ushuhuda wa nguvu ya upendo wa Mungu na maisha ya sadaka yanayofumbwa katika hija ya maisha yao ya kila siku, kwa ajili ya sifa na utukufu wa Mungu na Kanisa lake. Hili ni kundi maalum ambalo linajisadaka kwa ajili ya huduma. Ni watumishi wa Injili wanaoitwa kushuhudia kwa namna ya pekee mashauri ya Kiinjili katika maisha na vipaumbele vyao.

Tamasha la Pasaka anasema Padre Valens Assenga, Mkurugenzi wa Idara ya Katekesi, Jimbo Katoliki Moshi, huwahusisha vijana wakatoliki wanaosoma kwenye shule za sekondari na huadhimishwa mara baada ya Siku kuu ya Pasaka kila mwaka.

Tamasha la mwaka 2014 limegusia pamoja na mambo mengine kuhusu: hija ya maisha ya imani ya mwanafunzi mkatoliki; changamoto za kiimani, maisha ya mwanafunzi mkatoliki shuleni; wito wa upadre na utawa; umuhimu wa elimu pamoja na mahusiano ya mwanafunzi anapokuwa nyumbani, shuleni na katika ulimwengu ambao kwa sasa ni kamka tambara bovu!

Tamasha hili kwa namna ya pekee, ilikuwa ni fursa kwa Mashirika mbali mbali ya kitawa na kazi za kimissionari kujinadi kwa kuwaelezea vijana wakatoliki karama na utume wao ndani ya Kanisa na ulimwengu katika ujumla wake. Kwa mkurugenzi wa miito Jimbo Katoliki Moshi, ilikuwa ni fursa ya kutoa mwaliko kwa vijana kukumbatia heri za mlimani kama anavyokazia Baba Mtakatifu Francisko ili waweze kujisadaka kwa ajili ya Mungu, Kristo, Kanisa na Ulimwengu!

Baba Mtakatifu Francisko katika ujumbe wake kwa Siku ya Vijana Kijimbo, iliyoadhimishwa wakati wa Jumapili ya Matawi amewakumbusha kwamba, Yesu anajionesha kuwa ni njia inayobubujika furaha tangu pale alipozaliwa hadi alipokufa juu ya Msalaba na hatimaye, kufufuka siku ya tatu, matukio yote haya yanaonesha jinsi ambavyo alimwilisha Heri za Mlimani katika maisha yake na kukamilisha ahadi za Ufalme wa Mungu. Yesu anawaalika wafuasi wake kutembea pamoja na ye katika njia ya upendo inayowapeleka katika uzima wa milele.

Hii ni njia inayosheheni magumu, lakini Yesu ameahidi kwamba, ataendelea kuwa pamoja nao hadi utimiifu wa dahali. Watakumbana na umaskini, watateswa na kunyanyaswa, watapamba na na ukosefu wa haki na changamoto za toba ya wongofu wa ndani, bila kusahau mapambano yanayowataka kuchuchumilia utakatifu wa maisha.

Kwa hakika anasema Baba Mtakatifu, watakabiliana na changamoto mbali mbali za maisha, mwaliko wa kuendelea kushirikiana na Yesu katika furaha na mateso, katika magumu na hali ya kukata tamaa. Kwa kushikamana na Yesu anasema Baba Mtakatifu, waamini wataweza kupata amani na furaha inayobubujika kutoka kwenye upendo wa Mungu usiokuwa na mipaka. Heri za Mlimani ni nguvu ya mabadiliko mapya inayoleta mageuzi ya furaha ya kweli na wala si kama ile inayotolewa na vyombo vya upashanaji habari. Inashangaza masikioni mwetu kwamba, Mwenyezi Mungu amejitwalia ubinadamu, akawa sawa na binadamu, hata kufa Msalabani.

Kwa mantiki ya ulimwengu huu, wale ambao wanahesabiwa na Yesu kuwa wana heri, ni watu wanyonge na waliopoteza dira na mwelekeo! Wanatukuzwa wale wanaoonesha mafanikio, wenye mamlaka, nguvu na wenye kuheshimiwa na watu! Hii ni changamoto kubwa ya imani, inayowaalika vijana kuchukua Msalaba wao na kuanza safari ya kumfuasa Yesu, kwani Yeye anayo maneno ya uzima. Vijana wakithubutu kumkubali na kumpokea Yesu katika maisha yao ya ujana, atawajaza furaha na maana halisi ya maisha!

Baba Mtakatifu anawahamasisha vijana kuwa ni watu wenye furaha inayosimikwa katika imani na ukweli, mambo yatakayowawezesha kuwa na mang’amuzi ya kweli katika maisha kwa kukataa njia za mkato ambazo mara nyingi zinahatarisha maisha yao kwa kuwatumbukiza katika raha, starehe na anasa, mambo ambayo kamwe hayawezi kuzima kiu ya maisha yao ya ndani. Inasikitisha kumwona kijana akiogelea katika utupu!

Vijana wanapaswa kuwa imara wakiwa wanaongozwa na Neno la Mungu katika maisha yao, tayari kushindana na malimwengu, wakiwa na ujasiri unaowaongoza kutafuta furaha ya kweli pamoja na kuzingatia mambo msingi katika maisha. Kwa njia hii vijana wataweza kuwajibika na kukabiliana na changamoto za maisha kwa ujasiri mkuu.

Baba Mtakatifu anasema, umaskini wa roho unajionesha kwa namna ya pekee katika Fumbo la Umwilisho, pale Yesu alipojitwalia hali ya binadamu akawa sawa na binadamu na wala hakuona kwamba, kuwa sawa na Mungu ni jambo la kung’ang’ania sana. Hapa Mwenyezi Mungu anaamua kuukumbatia umaskini, ili aweze kumtajirisha mwanadamu kwa umaskini wake. Hili ndilo Fumbo la Umwilisho linalopata utimilifu wake katika Fumbo la Pasaka, kwa kuonesha unyenyekevu na upendo wa hali ya juu kabisa kwa mwanadamu. Mtakatifu Francisko wa Assisi ni kielelezo na mfano wa kuigwa katika umaskini wa roho, kwa kuonesha upendo kwa Kristo, maskini na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii.

Umaskini wa roho ni changamoto na mwaliko wa kubadilisha mfumo wa maisha kwa kuwa huru na vitu na kutokubali kumezwa na malimwengu, utajiri na mali na matokeo yake mambo haya yanawaachia machungu katika maisha. Vijana wanahamasishwa kujiaminisha mbele ya Mungu anayewapenda na kamwe hatawasahau, jambo la msingi ni kuwa na ujasiri wa furaha na kiasi.

Vijana wanaalikwa na Mama Kanisa kwa namna ya pekee kutubu na kuongoka, kwa kukazia upendo na mshikamano wa kidugu katika mchakato wa kukabiliana na hali ya umaskini unaojionesha katika: ukosefu wa fursa za ajira, wahamiaji, matumizi haram ya dawa za kulevya na utumwa mamboleo. Vijana wawe ni kikolezo cha: ujasiri, upendo na matumaini mapya miongoni mwa vijana wenzao. Kukutana na Maskini ni fursa ya kukutana na Yesu mteseka!

Imeandaliwa na Sr. Brigitta Samba Mwawasi,
Moshi.








All the contents on this site are copyrighted ©.