2014-05-07 08:56:22

Swiss guards watakiwa kuwa ni mkate safi kwa wale wanaokutana nao!


Kardinali Pietro Parolin, Katibu mkuu wa Vatican, Jumanne, tarehe 6 Mei 2014, katika Kanisa kuu la Mtakatifu Petro mjini Vatican, ameadhimisha Ibada ya Misa takatifu kwa ajili ya Kikosi cha ulinzi cha Kipapa katika maadhimisho ya kumbu kumbu ya miaka 508 wakati Askari 147 kutoka Uswiss walipojisadaka kwa ajili ya kulinda Kanisa na Papa Clement VII.

Ibada hii imehudhuriwa na Makamanda, wanajeshi na familia zao pamoja na viongozi kadhaa kutoka mjini Vatican. Wanajeshi wapya 30 wamekula kiapo cha utii kwa Baba Mtakatifu.

Katika mahubiri yake, Kardinali Parolin amekazia umuhimu wa kushiriki kikamilifu na kupokea Sakramenti ya Ekaristi Takatifu, ili kuzima kiu na njaa ya maisha ya kiroho, kielelezo cha imani thabiti. Yesu anasema ni mkate ulioshuka kutoka mbinguni, kumbe, ni mkate wa maisha ya uzima wa milele na alama wazi ya uwepo endelevu wa Kristo kati ya watu wake anayeendelea kuwaangazia wafuasi wake kwa njia ya Neno la Mungu na maisha ya Kisakramenti.

Kardinali Parolin anasema, Kanisa linawakumbuka kwa namna ya pekee Askari 147 waliojisadaka kwa ajili ya kulinda Kanisa na kumtetea Khalifa wa Mtakatifu Petro, ni mwaliko wa kuchota katika hazina ya imani, tunu msingi za maisha ya kiroho ambazo zimekuwa kweli ni dira na mwongozo katika historia ya wanajeshi hawa. Jambo la kwanza ni huduma kwa Kanisa na kwa Khalifa wa Mtakatifu Petro, kielelezo makini cha ushuhuda na ujasiri kwa Kristo na Kanisa lake.

Huu ni ujasiri ambao wakati mwingine unaweza kuwagharimu maisha, kama ilivyokuwa kwa Stefano shahidi wa kwanza kuyamimina maisha yake kwa ajili ya kumshuhudia Kristo aliyeteswa, akafa na kufufuka kutoka katika wafu. Hata katika majaribu kama haya, hakuna haja ya kukata tamaa, bali kusonga mbele kwa ari na ujasiri mkubwa ili kumshuhudia Kristo kwa furaha, imani na matumaini thabiti.

Kardinali Pietro Parolin amewataka Askari wa Kikosi cha Ulinzi cha Kipapa maarufu kama "Swiss guards" kuwa mkate safi kwa watu wanaokutana nao mjini Vatican, kwa kuonesha ushuhuda wa furaha ya Kikristo. Amewataka waendelee kuwa imara na thabiti katika imani, matumaini na mapendo!







All the contents on this site are copyrighted ©.