2014-05-07 08:28:45

Sitisheni vita!


Katibu mkuu wa Umoja wa Mataifa Bwana Ban Ki-Moon, Jumanne, asubuhi tarehe 6 Mei 2014, amewasili mjini Juba, Sudan ya Kusini kwa ziara ya siku moja ili kujaribu tena kutoa ushawishi kwa makundi hasimu nchini humo kuanza tena mazungumzo yanayopania kujenga na kudumisha amani na utulivu Sudan ya Kusini, ambayo kwa sasa imetumbukia katika vita ya wenyewe kwa wenyewe ambayo tayari imekwisha sababisha maafa makubwa kwa watu na mali zao!

Katibu mkuu wa Umoja wa Mataifa pamoja na kuzungumza na viongozi wakuu wa Sudan ya Kusini ametembelea kambi ya wakimbizi wa Sudan ya Kusini ambamo kuna zaidi ya watu themanini elfu waliokimbilia humo ili kupata hifadhi kutokana na vita inayoendelea kurindima nchini Sudan ya Kusini.

Wachunguzi wa masuala ya kisiasa wanasema, vita na machafuko ya kisiasa yanayoendelea Sudan ya Kusini ni matokeo ya uchu wa mali na madaraka kutokana na utajiri mkubwa wa mafuta unaopatikana Sudan ya Kusini, ambao badala ya kuwa ni neema umegeuka kuwa taabu na mateso ya wananchi wa Sudan ya Kusini, kiasi cha kuanzisha vita na kinzani za kikabila, mchezo mchafu uliopitwa na wakati!

Katibu mkuu katika ziara yake hii amewataka viongozi wakuu wa Serikali na wapinzani kusitisha vita mara moja, ili kutoa nafasi kwa wakulima kuendelea na shughuli za uzalishaji kwani hadi sasa kuna jumla ya watu millioni moja wanaokabiliwa na uhaba mkubwa wa chakula na kwamba, majadiliano ya amani ni njia pekee ya kumaliza vita na kinzani za kijamii.







All the contents on this site are copyrighted ©.