Katibu mkuu wa Umoja wa Mataifa kukutana na Papa mjini Vatican
Baba Mtakatifu Francisko, Ijumaa, tarehe 9 Mei 2014 anatarajiwa kukutana na kuzungumza
na Katibu mkuu wa Umoja wa Mataifa Bwana Ban Ki-Moon atakayekuwa ameandamana na wakuu
wa taasisi za kimataifa kwenye Umoja wa Mataifa. Taarifa hii imethibitishwa na Padre
Federico Lombardi, msemaji mkuu wa Vatican.
Itakumbukwa kwamba, Baba Mtakatifu
Francisko, tarehe 9 Aprili 2013 alikutana na kuzungumza na Katibu mkuu wa Umoja wa
Mataifa mjini Vatican, ambaye baadaye alikutana na Kardinali Tarcisio Bertone, aliyekuwa
Katibu mkuu wa Vatican kwa wakati huo. Katika mazungumzo hayo, Baba Mtakatifu Francisko
alisema alipenda kuendeleza mazungumzo kati ya viongozi wa Kanisa pamoja na viongozi
wa Umoja wa Mataifa katika mchakato wa kudumisha misingi ya haki, amani, mafao ya
wengi pamoja na kusimama kidete kulinda na kutetea haki msingi za binadamu.
Katika
mazungumzo yao viongozi hawa wawili waligusia vita iliyokuwa inaendelea nchini Syria
na sehemu mbali mbali za dunia, ambako amani na utulivu bado ni ndoto kwa wananchi
wengi. Walizungumzia pia biashara haram ya binadamu inayodhalilisha utu na heshima
ya binadamu; hali ya wakimbizi na wahamiaji.
Katibu mkuu wa Umoja wa Mataifa
aliyekuwa anaanza awamu ya pili ya uongozi wake wa miaka mitano, aliofafanua mikakati
ya uongozi wake kwa kujikita katika mchakato wa kutafuta Mwarobaini wa kuzuia na kutibu
vita na kinzani za kijamii zinazoendelea kusababisha majanga makubwa katika maisha
ya watu; kujenga na kuimarisha mshikamano wa kimataifa; kukuza na kudumisha maendeleoendelevu
ya kiuchumi katika usawa.
Baba Mtakatifu Francisko, alikumbushia pia mchango
wa Mama Kanisa katika maendeleo ya mtu mzima yanayogusa mahitaji yake msingi: kiroho
na kimwili. Kanisa limeendelea kutoa huduma kadiri ya utambulisho na nyenzo zilizopo,
kwa ajili ya kulinda na kutetea utu na heshima ya binadamu aliyeumbwa kwa sura na
mfano wa Mungu. Kanisa linapenda kukazia utamaduni wa watu kukutana na kuzungumza
kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya wengi.