2014-05-07 07:01:04

Jitihada za ujenzi wa mshikamano na udugu!


Mfuko wa Centesimus Annus kwa ajili ya Papa kuanzia tarehe 8 hadi tarehe 10 Mei 2014 utafanya mkutano wa kimataifa unaoongozwa na kauli mbiu “mafao ya jamii na mwelekeo wa fursa za ajira: Je, mshikamano na udugu vinaweza kuwa ni sehemu ya maamuzi msingi?” RealAudioMP3

Hivi karibuni Baba Mtakatifu Francisko aliwataka wajumbe wa Mfuko huu kutafakari kwa kina na mapana kuhusu fursa mbali mbali zilizopo katika mchakato wa kukuza na kuimarisha mshikamano wa kidugu katika mikakati ya kiuchumi. Hivi ndivyo anavyofafanua Bwana Domingo Sugranyes Bickel, Rais wa Mfuko wa Centesimus Annus, wakati akiwasilisha mada ya mkutano huu kwa waandishi wa habari mjini Vatican.

Tafakari hii inawajumuisha wasomi, wafanyabiashara na wawakilishi wa viongozi wa Kanisa kutoka sehemu mbali mbali za dunia, kwa kuangalia mwelekeo mpana wa kidunia katika masuala ya kiuchumi na uwezekano wa kutengeneza fursa za mshikano wa ajira kimataifa.

Hii inatokana na ukweli kwamba, kuna ongezeko la watu wenye sifa na utalaam katika kazi na kuna kundi kubwa la watu wasiokuwa na ujuzi wala utaalam; kundi la kati la wafanyakazi linaendelea kupungua na tofauti kubwa zinajionesha kati ya wafanyakazi wa viwandani kati ya nchi tajiri duniani na zile zinazoendelea. Hata katika nchi husika, bado kuna tofauti kubwa kati ya wafanyakazi, mambo ambayo kwa sasa yanaonekana kuwa kama jambo la kawaida kabisa.

Wajumbe wa Mfuko huu wanataka kupembua maana ya mshikamano wa kidugu katika masuala ya kiuchumi na kijamii katika uhalisia wake. Huu ni mchakato unaopania pia kupambana na uhalifu katika masuala ya uchumi na fedha pamoja na kusaidia mikakati ya misaada ya kijamii. Wajumbe watapata nafasi ya kuangalia jinsi ambavyo wanaweza kutekeleza dhana ya mshikamano na udugu katika shughuli zao za uzalishaji na uchumi, mambo yatakayojadiliwa katika makundi ya wajumbe watakaoshiriki katika mkutano huu na matokeo yake kuchapishwa baada ya mkutano.

Utu, heshima na maadili ni mambo msingi yanayopaswa kuzingatiwa katika shughuli za uzalishaji na uchumi, kwa kuonesha pia moyo wa ukarimu na uwajibikaji, unaowashirikisha wafanyakazi wengi zaidi. Mafundisho Jamii ya Kanisa ni msaada mkubwa katika kukuza na kudumisha umoja, udugu na mshikamano katika maeneo ya kazi, changamoto inayotolewa na Baba Mtakatifu Francisko, kwa kutoa kipaumbele cha kwanza kwa utu, heshima na mafao ya wengi.

Mfuko huu pia kwa mwaka 2014 utafanya semina kuhusu mageuzi katika mfumo wa fedha na mafao ya wengi; umaskini na uwajibikaji ili kulinda watu maskini zaidi; ni mambo yatakayojadiliwa huko New York, Marekani na Dublin, Ireland.








All the contents on this site are copyrighted ©.