Mpendwa Msikilizaji wa kipindi chetu cha Kanisa la nyumbani, Tumsifu Yesu Kristo.
Karibu katika kipindi chetu, tukumbushane na kutafakari juu ya thamani ya Kazi.
Tunafanya
hivyo katika mwezi huu wa tano ambao tuliuanza kwa kumuenzi Mtakatifu Yosefu Mfanyakazi,
ambaye Mama Kanisa alipenda kumweka kuwa ni msimamizi na mwombezi wa wote wafanyao
kazi zenye kumtukuza Mungu na kuchangia hali njema ya wanadamu.
Tangu mwanzo
wa uumbaji, Mungu mwenyewe ametuonesha sisi sote thamani ya kufanya kazi. Ni kwa njia
ya Kazi Mungu aliuumba ulimwengu. Na alitupatia sisi wanadamu agizo na wito wa kufanya
kazi ili kuutiisha ulimwengu (Mw. 1:28). Nyakati mbalimbali katika historia manabii
wa Bwana waliitwa na kushiriki kazi ya Mungu ya ukombozi wa Mwanadamu. Kristo Bwana
naye alikuja ulimwenguni humu, akafanya kazi ya kumkomboa Mwanadamu. Mungu katika
utatu, amejidhihirisha kuwa ni Mungu wa Kazi. Nasi kwa moyo wa utii kwa Mungu wetu,
tunataka kufanya kazi kwa juhudi, maarifa na uadilifu, uli tuutiishe ulimwengu, jujipatie
riziki yetu ya kila siku na pia tupate riziki ya kuwasaidia walio wahitaji, wasio
na uwezo wa kufanya kazi.
Tafanusi ya kazi nyakati zote inatuambia kwamba,
kazi ni shughuli yoyote halali yenye kumpatia mwanadamu riziki. Kwetu sisi tunaomwamnini
Mungu, kazi ni utii kwa Mungu, kazi ni shukurani kwa Mungu kwa kuumbwa kwetu kama
wanadamu, kazi ni kuendelea kujiumba katika utu. Kufanya kazi ni kushiriki kazi ya
uumbaji ya Mungu kwa neno lile ‘...mkaijaze nchi na kuitiisha’.
Mtakatifu
Yohane Paulo II anasema, kwa njia ya kazi mwanadamu anashiriki kazi ya uumbaji ya
Mungu, anaingia katika umoja na Kristo Mtenda kazi na anashiriki katika fumbo la wokovu
la Pasaka. Na hiyo ndiyo teolojia ya kazi kadiri ya imani yetu.
Hapo tunaona
jinsi kazi inavyotuunganisha na ulimwengu wetu lakini pia na ulimwengu wa kiroho.
Kinachotupatia heshima mbele za watu ni aina ya kazi tunayofanya, namna tunavyoifanya
na namma pia tunavyotumia mapato ya kazi zetu. Hapa tunapata picha ya wazi kwamba,
kazi imeunganika kwa karibu zaidi na utu wa mtu, ndiyo maana wenye busara walisema,
kazi ni kipimo cha utu.
Wazee wetu wa Mtaguso wa II wa Vaticani, wakitafakari
juu ya wito na thamani ya kazi wanatufundisha juu ya malengo ya utendaji kazi. Lengo
la kwanza la kazi ni utawala na ukamilishaji wa ulimwengu. Lengo la pili ni utoaji
huduma kwa wengine. Lengo la tatu ni ukuaji binafsi na lengo la nne ni kumpa Mungu
utukufu (Taz. Hati Furaha na Matumaini, na 67).
Tunapotafakari juu ya wito
na maisha ya Mt. Yosefu kama baba mlishi wa Yesu na Baba mwajibikaji wa familia takatifu
ya Nazareti, aliyeitunza familia yake kwa kufanya kazi, na zaidi ya hilo, alimfundisha
Mtoto Yesu kufanya kazi, tunataka nasi, familia zetu ZIWE SHULE ZA KAZI. Watoto wafunzwe
thamani ya kazi, wafunzwe kupenda kufanya kazi ili kujipatia kipato halali kwa maisha
yao.
Endapo watoto wetu hawafundishwi thamani ya kazi katika familia, hapo
ndipo kinapozuka kizazi cha watu wanaoona kuwa kazi ni adhabu. Kinazuka kizazi chenye
kuendekeza utamaduni wa uvivu., watu ambao hawajiandai kuwa watenda kazi makini katika
jamii. Watu ambao pengine hupenda kufanya kazi kidogo na kuvuna mapato makubwa mno,
kwa njia zisizo za kiadilifu, hata kwa njia ya kudhalilisha utu wao. Kadiri ya Mtume
Paulo, wavivu, wasio penda kazi anawaona kuwa ni watu ‘wahovyo’, kwa sababu wanakuwa
ni mizigo inayowaelemea wengine. Na anasema wazi, asiyefanya kazi asile (Rej. 2Thes.
3:10). Mtu asipokula manake atakufa, kwa hiyo mvivu hastahili kuishi.
Utamaduni
wa kuchukia kazi, utamaduni wa uvivu ni hatari kubwa sana kwa kanisa na taifa. Ndiyo
maana tunazigeukia familia na wote wenye dhamana ya malezi, tuwafundishe watoto wetu
kazi. Ile aina ya wazazi na walezi wenye tabia ya kufuga watoto katika uvivu, watambue
kuwa ni hatari, wanawaangamiza watoto wao. Kwa nje wanaonekana kama wanawaonea huruma
watoto wao wasihangaike na kazi, kwa sababu pesa ipo watenda kazi wapo, hivyo watoto
wakae tu, wastarehe. Mwisho wa huruma kama hizo, ni uangamizi.
Familia ya
watu wavivu ni kichaka cha matatizo mengi, ni chimbuko la ombaomba, chanzo cha mafarakano
mengi na ni hatari kwa amani ya majirani. Uvivu ni moja ya vyanzo vikubwa vya dhambi
na kila aina ya uovu na ndiyo maana wachaji wa zamani walisema ‘uvivu ni adui wa roho’.
Sisi tunakaza kusema, kazi ni afya na uvivu ni chanzo cha magonjwa ya kimwili, kiakili
na kiroho. Kazi ni heshima kwa Mungu, uvivu ni fahari ya shetani na unatufanya tuajiriwe
naye. Tukifikiri vizuri tutagundua kuwa dhambi nyingi za mawazo, maneno au matendo
huwa tunatenda tunapokuwa wavivu. Uvivu ni mlango wa dhambi nyingi na matatizo mengi.
Taasisi
zinazohusika na malezi-elimu kwa vijana wanaokuwa mashuleni, nao waone namna sahihi
ya kupandikiza roho ya kupenda kufanya kazi kwa vijana hao wawapo shuleni na baada
ya kuwa wamehitimu masomo yao. Ajabu sana nyakati zetu hizi, watu watahitimu masomo
na pengine watajaliwa kupata ajira, lakini hawapendi kujituma kufanya kazi walioitafuta,
badala yake wataendekeza uvivu tu na kudai mishahara mikubwa na marupurupu mengi.
Matokeo yake hakuna maendeleo yanayoonekana hata kama takwimu zitaonesha kuwa
na idadi kubwa ya wafanyakazi. Katika taasisi nyingi za huduma ndani na nje ya Kanisa,
kuna vilio vya kukosa huduma stahiki. Sio kwamba wahudumu hawapo. Wapo ila ni wavivu
mno. Walipenda ajira tu, hawakupenda kazi. Wanaona kazi ni mzigo, ni bugudha. Hivi
hata anayekuja kutafuta kuhudumiwa naye anonekana kuwa ni bugudha. Utamaduni w-hatarishi
wa uvivu unaendelea kujengeka na kukomaa katika jamii zetu. Hiyo ni hatari kwa familia
ya mwanadamu.
Tukitaka kujenga heshima ya kweli ya jamii zetu, kila mmoja wetu
ni vema ajenge dhamiri ya kupenda na kuthamini kazi. Sio tu kutafuta ajira na kuwinda
mishahara pasipo kujituma kufanya kazi. Kutokana na dhana hii ya uvivu, itashangaza
sana nyakati zetu wote ‘wenye ajira na wasio na ajira’ wanakuwa wavivu na mwishoni
mwa siku watalalamika maisha ni magumu. Hata aliyeelimika katika ufundi na kilimo,
naye atalalamika sawa na yule ambaye hakubahatika kabisa kwenda shule. Tunadhani wakati
umefika sasa, tunahitaji mapinduzi ya kifikra. Dhana ya kazi, uwajibikani na maisha
mema vipandikizwe kwa bidii katika kuanzia katika kizazi kichanga.
Pamoja na
mwito huo wa kufanya kazi, tukumbuke kwamba katika nyakati zetu hizi kuna watu ambao
ni walevi wa kazi. Ni wale ambao kwao kazi ndiyo kila kitu. Wakipata kazi, hawamjali
Mungu, wala familia, wala jirani. Wao ni kazi masaa yote, na mwisho wa siku kazi inakuwa
ndiyo mungu wao. Tunataka kazi tufanyazo ziendelee kujenga utu wetu na sio kutunyang’anya
utu wetu. Kazi isitutenge na Mungu na jirani bali ituunganishe zaidi na Mungu na jirani.
Mtakatifu Yohane Paulo II alitufundisha akisema ‘kazi ni sehemu mojawapo inayomsaidia
mwanadamu kupata utakatifu’. Endapo tutaiabudu kazi, basi hapo haitatupatia utakatifu
bali itatunyang’nya utakatifu.
Tunaomba na kusihi, kwa maombezi ya Mtakatifu
Yosefu na kwa heshima kwa Mungu wetu, sote tupende kufanya kazi kiadilifu. Tuimarishwe
na Neno lisemalo ‘Mungu hakosi haki, yeye hataisahau kazi mliyoifanya au upendo mliyoonesha
kwa ajili yake katika huduma mliyowapa na mnayowapa sasa watu wake....Msiwe wavivu,
bali muwe kama wale wanao amini na wenye uvumilivu wakapokea yale aliyoyaahidi Mungu
(rej. Ebr. 6:10-12). Kutoka Radio Vatican ni Mimi Padre Pambo Martin Mkorwe, OSB.