2014-05-05 09:33:13

Neno la Mungu na Ekaristi Takatifu ni nyenzo msingi katika hija ya maisha ya kiroho!


Baba Mtakatifu Francisko katika tafakari yake kuhusu Liturujia ya Neno la Mungu, Jumapili ya tatu ya Kipindi cha Pasaka, tarehe 4 Mei 2014 kwenye Uwanja wa Kanisa kuu la Mtakatifu Petro mjini Vatican anasema kwamba, hija ya wanafunzi wa Emmau waliotikiswa katika maisha yao, walionekana kukata tamaa, wakarudi Emmau wakiwa wamesonokena, lakini njiani wakakutana na Yesu ambaye hawakumtambua.

Yesu akawafafanulia kuhusu Maandiko Matakatifu juu ya mateso, kifo na ufufuko wa Masiha kama ilivyokuwa imetabiriwa na Manabii. Baada ya kusikia Neno la Mungu, mioyo ya wanafunzi hawa ikawaka moto wa matumaini mapya. Wakamkaribisha nyumbani mwao na kumtambua wakati alipokuwa anaumega Mkate, mara akatoweka machoni pao, wakabaki na mshangao mkubwa!

Hii ikawa ni alama iliyomtambulisha Yesu Mfufuka miongoni mwa wanafunzi wake, ambao walirejea tena mjini Yerusalem kuwashirikisha wengine mang'amuzi yao kwamba, walikuwa wamekutana na Yesu Mfufuka katika kuumega Mkate.

Baba Mtakatifu Francisko anasema, njia ya Emmau ni kielelezo cha hija ya maisha ya kiimani: Maandiko Matakatifu na Ekaristi Takatifu ni mambo makuu yanayomwezesha mwamini kukutana na Kristo. Hata leo hii kuna waamini wanaokwenda Kanisa wakiwa na wasi wasi, hofu na mashaka mioyoni mwao. Ni watu wanaobeba matatizo na hali ya kukata tamaa, kiasi hata cha kusahau mpango wa Mungu katika maisha na hatimaye, kumgeuzia Mungu kisogo.

Neno la Mungu linamwezesha Yesu kufafanua tena Maandiko Matakatifu ili kuwawashia wafuasi wake moto wa imani na matumaini na kwa kushiriki Ekaristi Takatifu anawakirimia nguvu. Kwa njia hii, waamini wanaweza kurudi tena nyumbani wakiwa na furaha kama ilivyotokea kwa wanafunzi wa Emmau. Neno la Mungu na maadhimisho ya Fumbo la Ekaristi Takatifu ni chemchemi ya furaha, matumaini na ari mpya. Baba Mtakatifu anawahimiza waamini kutafakari Neno la Mungu katika hali mbali mbali za maisha na hapo wataonja uwepo na faraja ya Mungu.

Baba Mtakatifu anawaalika waamini kumkimbilia Bikira Maria, ili aweze kuwaombea kwa Mwanaye mpendwa, waweze kuishi mang'amuzi ya wanafunzi wa Emmau, hususan katika maadhimisho ya Ibada ya Misa Takatifu, ili kutambua neema ya kukutana na Yesu anayewakirimia mabadiliko ya ndani. Neno la Mungu na Ekaristi Takatifu ni nyenzo msingi katika hija ya maisha ya kiroho.







All the contents on this site are copyrighted ©.