2014-05-05 15:34:02

Kikosi cha ulinzi cha Kipapa ni kielelezo cha sadaka, ukakamavu na ulinzi!


Tarehe 6 Mei 1527 walinzi kutoka Uswiss walijisadaka kwa ajili ya kulinda Kanisa na Baba Mtakatifu, kielelezo cha ujasiri wa hali ya juu kabisa na uaminifu. Ni mwaliko kwa Kikosi cha Ulinzi kutoka Uswiss kuendelea kutumikia kwa furaha, licha ya mabadiliko ya nyakati.

Huduma ya Kikosi hiki ni kielelezo cha ushuhuda wa kweli unaojidhihirisha kwa sadaka kubwa, muhimu na inayowajibisha. Ni maamuzi ambayo yanasindikizwa kwa namna ya pekee na familia na jumuiya ambayo imejitaabisha kuwafunda, wote hawa wanapaswa kushukuriwa!

Hizi ni shukrani za Baba Mtakatifu Francisko kwa Kikosi cha Ulinzi cha Kipapa wakati huu wanapofanya kumbu kumbu ya sadaka iliyotolewa na wenzi wao kunako mwaka 1527. Anasema, mji wa Roma una utajiri mkubwa wa mambo ya kale, historia na utamaduni. Ni mahali ambapo kuna umati mkubwa wa mahujaji na watallii wanaoingia na kutoka mjini Roma kwa sababu mbali mbali. Hii ni hija ya historia ya watu na wanajeshi wa Kikosi cha ulinzi cha Kipapa wanashiriki pia.

Kama Kikosi cha Ulinzi cha Kipapa wanayo dhamana ya kushuhudia utulivu na furaha kwa wale wote wanaofika mjini Vatican ili kutembelea Kanisa kuu la Mtakatifu Petro au kwa ajili ya kukutana na kuzungumza na Khalifa wa Mtakatifu Petro, changamoto na mwaliko wa kuwa imara na thabiti katika imani, wakarimu nao wenye upendo wa dhati kwa wote wanaokutana nao!

Baba Mtakatifu anakumbusha kwamba, Mwaka 2014 magwanda wanayovaa Askari wa Kikosi cha ulinzi cha Kipapa yanatimiza miaka mia moja, kielelezo cha majitoleo, ukakamavu na ulinzi. Ni magwanda yanayoonesha utukufu wa historia iliyopita, lakini ndani ya maganda haya kuna mtu mzima; kuna familia na mahali anakotoka mtu, matumaini na mipango ya maisha. Ni magwanda yanayodai uungwana, ukarimu na upendo.

Baba Mtakatifu anasema, hii ni changamoto pia kwa Askari wa Kikosi cha ulinzi cha Kipapa kujenga na kudumisha maisha ya kijumuiya, wakati wa raha na karaha, kwa kufarijiana na kusaidiana katika urafiki bila kushabikia mambo yanayoweza kuwagawa na kujikuta wanaelemewa na hali ya kutojali, nyanyaso na ubaguzi wa rangi.

Baba Mtakatifu anasema, kila siku yuko karibu na majitoleo na sadaka yao, jambo ambalo anapenda kuwashukuru kwa dhati kabisa. Anaendelea kuwahimiza kuwa waaminifu kwa kutambua kwamba, Kristo daima yuko karibu nao anawaunga mkono katika safari yao, hasa wakati wanapochoka na kuwa na wasi wasi. Baba Mtakatifu amewaweka Wanajeshi wa Kikosi cha ulinzi cha Kipapa chini ya usimamizi wa Bikira Maria pamoja na watakatifu somo na wasimamizi wao: Nikolaus, Sebastian na Martini.







All the contents on this site are copyrighted ©.