Kuna msemo ulioshamiri sana kwa Waswahili, hasa ikiwa mtu anayo matumaini ya kupata
kitu katika biashara na anakikosa anaambiwa: “Imekula kwako”. Usemi huu ungeweza pia
kutumika kwa mitume baada ya kifo na kuzikwa kwa Yesu. Mitume na wafuasi waliweka
matumaini yao yote kwa Yesu, lakini sasa baada ya kufa kwake na kupita siku mbili
tatu, wanakata tamaa na kujisikia “imekula kwao.”
Wengi wao waliingiwa na woga
na kujifungia kwenye vyumbani, ili mradi tu kwamba walikuwa wameishiana na mradi
wa kumfuata Yesu. Wengine baada ya kwisha tu sikukuu ya Pasaka ya kiyahudi siku iliyofuata
kila mmoja akaanza kuchukua njia zake. Wafuasi wawili walitanguzana mmoja hatajwi
jina na mwingine anaitwa Kleopa wakachukua zao kurudi kijijini Emmaus. Wamepoteza
muda mrefu wa kutumaini, wa kujitoa, myaka mitatu ya ushindi mkuu, miaka ya imani,
ya kusubiri, ya uzuri, miaka utamu ya mwanga. Lakini kifo kile cha Yesu ndicho kilichochafua
kila kitu. Ama kweli imekula kwao!
Wafuasi hawa wawili walijisikia kuwa kama
miali ya moto inayokaribia kuzimika. Hebu tuone jinsi Bwana mfufuka anavyoihuisha
tena: Wafuasi hao wanatembea kwenye barabara kuu wanayopita watu wote, wakiwa katika
huzuni kubwa, katika upweke, wakijadiliana. Yesu hawaiti toka mbali na kuwasimamisha,
bali anawasogelea kama mtu mwenye haraka lakini anayetaka kutanguzana nao. Wao wanageuka
na kugundua kwamba kuna mtu anawafuata. Hapa Yesu amejionesha kama msafiri wa kawaida
tu ila mwenye haraka. Yeye mfufuka angeweza kusafiri kwa mwendo wa kasi sana, kumbe
anatanguzana nao, anapima hatua zao zilingane na mwendo wao wa kuchoka, mwendo wa
waliojeruhiwa.
Wanaelekea Emmaus, yaani anatanguzana nao katika kuchanganyikiwa
kwao na katika matatizo na uchungu wao. Ndivyo Yesu anavyokutana na watu mbalimbali
hapa duniani na kutanguzana nao katika safari yao ya maisha. Kila mmoja anamkuta akiwa
na hali fulani ya pekee.
Tunasikia kwamba Magdalena alimkuta akiwa analia,
kwa wale kumi na mmoja kule kwenye ziwa jumapili ijayo, anawakuta wana uchungu na
wamechanganyikiwa baada ya kukesha usiku mzima wakivua bila kupata kitu, wakati Tomaso
jumapili iliyopita alimkuta katika hali ya kutoamini. Wafuasi hawa anawakuta katika
lindi la uchungu na la upweke. Wako wawili tu, lakini sasa wanakuwa wasafiri watatu.
Katika
uchungu wao huo wanajadiliana na kuhubiriana juu ya suala zito na muhimu la maisha.
Wanaongeana juu ya jambo linalowakereketa kabisa ndani ya mioyo yao. Wafuasi hawa
wanazungumza juu ya Upendo. Yaonekana amewakimbilia, na kuwakuta ili kuwapa moyo,
kuwahimiza na kuwangaza. Hawakatishi mazungumzo yao: Anatafuta mwanya wa kujiingiza
katika mazungumzo yao kwa utulivu, kwa utamu kwa kuuliza swali jepesi na rahisi tu.
Tena anauliza kama vile mtu mjinga asiyefahamu kilichotokea. “Ni maneno gani
haya mnayosemezana hivi mnapotembea?” Kwa swali hili Yesu anaonesha kuujali sana uchungu
wao.
Swali hilo linamfanya Kleopa na mwenzake waanze kumshangaa. Yaani msafiri
mwenzao aliyetokea upande wanakotokea wao kuwa hajavisikia vituko vilivyotokea huko
Yerusalemu.
Habari hizo zimevuma mji mzima na watu wote wanavizungumzia sana.
“Inawezekanaje, wewe unayetoka sasa hivi huko mjini usisikie habari hii ya kusikitisha?”
Angekuwa mtu mwingine yeyote angeweza kuwasimamisha na kuwaambia: “Kaeni chini
hapa niwaeleze kinaganaga cha mambo yalivyotokea.” Kumbe Yesu ameanza kwa kuwaamshia
hamu ya kujieleza zaidi hadi wanamgeuzia kibao: “Hivi wewe peke yako ni mgeni asiyejua…”.
Huwezi kujua ni jinsi gani Yesu alilipokea swali hilo la wafuasi. Swali hilo la wafuasi
linaonesha waziwazi vionjo vilivyokuwa vimejaa ndani ya mioyo yao. Hadi hapo ilimtosha
kabisa Yesu kujisikia kuaminiwa na watu hawa. Kleopa aliyekuwa katika hali mbaya
ya kukata tamaa, na aliyejaa jazba, amefanikiwa kujimwaga mbele ya mgeni huyu.
Yesu
anawaacha waendelee kujimwaga. Bila kujitambua wakaendelea kujieleza hadi kufikia
kuzungumza mambo ya kiroho waliposema: “Mambo ya Yesu wa Nazareti, aliyekuwa mtu nabii,
mwenye uwezo katika kutenda na kunena mbele za Mungu na watu wote; tena jinsi wakuu
wa makuhani na wakubwa wetu walivyomtia katika hukumu yak ufa, wakamshulibisha… Tena
wanawake kadha wa kadha wa kwetu walitushitusha waliokwenda kaburini asubuhi na mapema,
wasiuone mwili wake; wakaja wakasema ya kwamba wametokewa na malaika waliosema kwamba
yu hai. Na wengine waliokuwa pamoja nasi walikwenda kaburini wakaona vivyo hivyo kama
wale wanawake walivyosema, ila yeye hawakumwona.” (Lk 24:19-20, 22-24).
Hapa
unaona kama vile wamechanganyikiwa. Yaani, wanaonekana kwa upande mmoja kama vile
wanasadiki lakini halafu kwa upande mwingine hawasadiki. Watu hawa wanateseka sana
kisaikolojia lakini walikuwa bado na imani mioyoni mwao. Kwa hiyo Yesu anawaambia:
“Enyi wenye mioyo mizito ya kuamini yote waliyoyasema manabii!” (Lk.24:25).
Yaani,
hawa walikuwa watu wa kutibiwa, siyo wa kuwalaani, watu wa kuwasahihisha na siyo kuwaachilia
tu, watu wa kuwapoza siyo kuwagombeza! Baada ya kuwatulia kidogo, Yesu anaanza kuwapa
dawa ya tiba. Anaanza kuwaelezea historia ya mambo yaliyokuwa kadiri ya Maandiko matakatifu
hadi wanakaribia kijiji cha Emmaus.
Baadaa ya kumaliza kuwaeleza, Yesu angeweza
kusema: “Sasa jamani baada ya kuwaeleza haya yote, tafadhali rudini Yerusalemu na
mkawahabarishe wenzenu haya niliyowaambia ili msikose tena imani. Yesu hafanyi hivi
badala yake anajifanya kama vile anapitiliza na kuendelea na safari zake. Hahitaji
chochote, wala haulizi chochote, na wala hategemei chochote toka kwao. Ndiyo maana
hawa wasafiri wawili wanaamua kumshawishi: “Kaa pamoja nasi, kwa kuwa kumekuchwa,
na mchana unakwisha.” (Lk 24:29). “Mgeni afike mwenyeji apone”. Je, sisi tumwambie
nani “Kaa pamoja nasi”?
Tunaweza kumwambia mtu aliyetutendea jema fulani “kaa
nasi”, au mgeni yule ambaye hatutii hasara, mtu asiyekuwa mzigo. Wageni namna hiyo
wako wachache sana na pengine hawako kabisa. Kumbe Yesu aliye Mungu hahitaji chochote.
Yesu aliyesukumwa na upendo mtupu hataki kumtuliza tu mtu. Hatukani mtu, hasemi maneno
yasiyo na maana, huyu mgeni alitoa maneno ya kuhuisha. Aligusa hata mioyo yao, aliwatia
moyo, hadi wanamkaribisha kwao.
“Wakakikaribia kile kijiji walichokuwa wakienda,
naye alifanya kama anataka kuendelea mbele.” (Lk 24: 28). Katika nafasi nyingine Yesu
aliwapita wanafunzi wake: Mathalani kwenye mto Yordani, au mbele ya Yohane Mbatizaji
kule Genesareti, au usiku ule wa dhoruba. Anapita pembeni ya Kanani bila kusimama.
Anampita kipofu bila kumponya. Yesu anafanya hivi ili mmoja uweze kumtafuta, au uweze
kumwita. Yesu anapenda kuitwa. Wakati mwingine anaweka hata mazingira ya kuja kwake
na matendo yake ili aweze kuitwa na binadamu. Anavuvia, anadokeza, anashawishi, anahimiza
lakini anasubiri. Wanafunzi wanamwomba atulie, abaki akae nao.
Wao wanahoja
zao kinyume na ukweli ule wa ndani kabisa. Hoja wanayotoa ya kumshawishi abaki ni
kwamba: “kumekuchwa, na mchana unakwisha.” Badala ya kumwambia kwamba tunapenda kuwa
na wewe. Tumeshakupenda, licha ya kutukosoa na kutusahihisha, na hasa kutokana na
hilo tunataka ubaki nasi. Yesu alilazimisha kwa wema. Alikuwa yeye wa kwanza kuwajongelea.
Sasa wamekuwa wao kutaka kumshikilia asiondoke. Anaingia na katika tendo la kumega
mkate, wanamtambua. Mioyo yao inafunguka: “Ni Yeye” wakasema. Lakini kabla hawajafanikia
kuwasiliana naye, akawa ameshatoweka machoni pao.
Kumbe, ili aweze kutambulika,
haoneshi vyeti vyake vya utambuilisho, na vyeti vya shule. Anajitambualisha kwa kumega
mkate. Tendo ambalo wanafunzi wake wanamtambua mara moja. Yawezekana walimzoea akifanya
hivyo kila walipokuwa wanakula pamoja. Aidha tendo hilo alilirudia karibuni tu kwenye
karamu ya mwisho alipowaambia: “Fanyeni hivi kwa kunikumbuka mimi.” (Lk. 22:19).
Hapo
hapo wale wanafunzi wawili wakaanza safari ya kurudi Yerusalemu, wale ambao walipokuwa
wanakuja Emaus walikuwa wamechoka, na kuchanganyikiwa. Sasa wanarudi kwa mbio wakiwa
na kiherehere cha kwenda kuwasimulia wenzao kwamba Yesu amefufuka, anaishi, na kwamba
wao wameonana naye. Waliochoka kutembea sasa wanakimbia.
Kumbe umoja aina hii
na Kristu unaleta nguvu mpya na ari mpya. Tunaalikwa kutanguzana na Kristu katika
maisha yetu.