Ujumbe wa Vatican kukutana na Kamati ya kudhibiti ukatili tarehe 5-6 Mei 2014
Kunako Mwaka 1984, Nchi wanachama wa Umoja wa Mataifa waliweka sahihi Mkataba dhidi
ya ukatili, CAT. Vatican ikajiunga na kuridhia itifaki hii kunako mwaka 2002 na mwaka
2012, ikaanza kutoa taarifa ya utekelezaji wa mkataba huu. Akizungumzia kuhusu mkataba
huu, Padre Federico Lombardi msemaji mkuu wa Vatican anabainisha kwamba, mkataba huu
ni kati ya mikataba muhimu sana katika Jumuiya ya Kimataifa dhidi ya ukatili, dhuluma
na nyanyaso kwa binadamu.
Ni mkataba ambao unazishirikisha nchi wanachama
wa Umoja wa Mataifa kwa hiyari yao wenyewe na wala hakuna shuruti. Ili kuweza kuhakiki
utekelezaji wa mkataba huu, Jumuiya ya Kimataifa imeunda kamati maalum ya wataalam
wa kujitegemea, wanaoangalia utekelezaji wa mkataba huu kwa nchi zilizouridhia. Katika
mkutano wake unaofanyika kila mwaka mjini Geneva, kamati hukutana na wajumbe wa nchi
wanachama ili kujadiliana na kuona utekelezaji wake. Yote haya anasema Padre Lombardi
hufanyika kwa njia ya majadiliano ya wazi yanayoweza kuvishirikisha vyama vya kiraia
kwa njia ya kutoa maoni na mapendekezo yao
Kamati ya watu kumi ya Mkataba dhidi
ya mateso inaendelea na kikao chake cha hamsini na mbili, kilichoanza hapo tarehe
28 Aprili na kitafungwa rasmi tarehe 23 Mei 2014. Mwaka huu kamati inachambua taarifa
za utekelezaji wa mkataba huu kutoka katika nchi za: Uruguay, Thailand, Sierra Leone,
Guinea, Montenegro, Cyprus, Lithuania pamoja na Vatican.
Mkutano wa kamati
na wajumbe wa Vatican unafanyika Jumatatu tarehe 5 na tarehe 6 Mei, 2014. Wajumbe
wa Vatican watawakilisha taarifa fupi ya utekelezaji wa mkataba huu mjini Vatican
na baadaye kutakuwa na maswali na ufafanuzi. Kamati itakuwa na taarifa kwa vyombo
vya habari hapo tarehe 23 Mei 2014 na hapo itachapisha maoni na mapendekezo yake yatakayofanyiwa
kazi baadaye na Vatican.
Padre Lombardi anasema kwamba, Vatican na Kanisa Katoliki
katika ujumla wake limekuwa likitoa mkazo kuhusu umuhimu wa kusimama kidete kulinda
na kutetea utu na heshima ya binadamu, mambo ambayo yanafanyiwa rejea na Kamati dhidi
ya ukatili na adhabu zinazokwenda kinyume cha utu na heshima ya binadamu. Utekelezaji
wa mkataba huu unahusu eneo la Vatican tu na wala si vinginevyo. Mapendekezo yaliyotolewa
kwa Vatican kunako mwaka 2012 yalifanyiwa kazi kwa marekebisho ya sheria zilizoanza
kutumika kunako mwaka 2013 kuhusu makosa ya jinai mjini Vatican.
Padre Federico
Lombardi anasema, licha ya Vatican kuridhia na kufanya marekebisho katika sheria
zake kadiri ya mapendekezo yaliyokuwa yametolewa, Vatican pia imeendelea kuridhia
mikataba dhidi ya uhalifu wa kiuchumi na kifedha; ubaguzi wa rangi pamoja na haki
za mtoto. Utekelezaji wa mapendekezo yaliyokuwa yametolewa na kamati unaonesha mafanikio
makubwa.
Ni matumaini ya Vatican kwamba, wajumbe wa kamati watajielekeza zaidi
katika masuala yanayogusa utekelezaji wa mkataba na wala si kufuata shinikizo linalotolewa
na vyama vya kiraia kwa malengo binafsi ya kutaka kupata umaarufu kisiasa katika medani
za kimataifa kama ilivyojitokeza wakati wa kusikiliza taarifa ya utekelezaji wa haki
za mtoto mjini Vatican.
Kamati itekeleze wajibu wake kwa kuendesha majadiliano
katika hali ya utulivu kwa kuzingatia malengo ya mkataba, vinginevyo anasema Padre
Lombardi, kamati hii itakosa uhalali wake katika Jumuiya ya Kimataifa kwa kujikita
katika masuala ya kisiasa badala ya kujielekeza zaidi katika kulinda na kutetea haki
msingi za binadamu. Vatican itaendelea kusimama kidete kulinda na kutetea haki msingi
za binadamu dhidi ya ukatili na adhabu kali.