2014-05-03 08:20:38

Mashirika ya Kipapa ya Kimissionari kuanza mkutano wake tarehe 5-10 Mei 2014 mjini Roma


Kardinali Fernando Filoni, Mwenyekiti wa Baraza la Kipapa la Uinjilishaji wa Watu pamoja na Askofu mkuu Protase Rugambwa, Katibu mwambata na Rais wa Mashirika ya Kimissionari ya Kipapa ni kati ya viongozi wakuu watakaotoa taarifa kwenye mkutano mkuu wa Mashirika ya Kimissionari ya Kipapa katika mkutano wake mkuu wa mwaka unaoanza Jumatatu tarehe 5 hadi tarehe 10 Mei 2014. Mkutano huu unawashirikisha wakurugenzi wa Mashirika ya Kipapa kutoka sehemu mbali mbali za dunia.

Sehemu ya kwanza ya mkutano mkuu ni kuanzia tarehe 5 hadi tarehe 6 Mei 2014 kwa kujikita katika mikakati ya shughuli za kichungaji. Hapa Makatibu wakuu wa Mashirika ya Kipapa wataangalia shughuli na mikakati ya Uinjilishaji kati ya watu; mafundisho ya viongozi wakuu wa Kanisa na utekelezaji wake katika Makanisa mahalia. Hapa Askofu mkuu Rugambwa na viongozi wenzake watatoa ufafanuzi wa kina.

Sehemu ya pili itakayoanza hapo tarehe 7 hadi 10 Mei 2014 itashughulikia masuala ya kawaida ya Mashirika ya Kimissionari ya Kipapa na wahusika wakuu ni Makatibu wakuu wa Mashirika ya Kipapa kutoka mjini Vatican. Hawa wataangalia taarifa na utekelezaji wa maazimio ya mwaka 2013, watapanga mwelekeo wa bajeti kwa Mwaka 2014- 2015, msaada unaoombwa kutoka katika Makanisa mahalia; majadiliano na hatimaye kupitisha miradi itakayokuwa imeridhiwa na wajumbe wa mkutano mkuu wa Mashirika ya Kimissionari ya Kipapa katika mkutano wao.

Ratiba elekezi inaonesha kwamba, tarehe 9 Mei 2014 kutafanyika mikutano ya Mabara ili kupembua kwa kina na mapana maamuzi yaliyofikiwa, kupitisha bajeti na miradi kadiri ya maeneo husika. Askofu mkuu Protase Rugambwa anatarajiwa kutoa hotuba ya kufunga na Jumamosi, tarehe 10 Mei 2014 wajumbe wanatarajiwa kukutana na kuzungumza na Baba Mtakatifu Francisko.







All the contents on this site are copyrighted ©.