2014-05-03 10:07:21

Jengeni maisha yenu katika ukweli, utakatifu, furaha na kweli za Kiinjili!


Kardinali Pietro Parolin, Katibu mkuu wa Vatican, Ijumaa, tarehe 2 Mei 2014 ameadhimisha Ibada ya Misa Takatifu kwa ajili ya wajumbe wa Chama cha Vijana Wakatoliki waliokuwa wanashiriki mkutano mkuu wa kitaifa uliofanyika mjini Roma. Katika mahubiri yake anasema, hata yeye amekuwa ni mkereketwa na mwanachama hodari, mambo ambayo yameacha chapa ya kudumu katika maisha na utume wake. Amekuwa karibu na chama cha vijana Wakatoliki kwa njia ya sala!

Kardinali Parolin anawataka vijana wakatoliki kuwa watu wapya wanaoongozwa na mwanga wa Neno la Mungu na Mafundisho ya viongozi wa Kanisa, ili kujenga msingi thabiti kwa maisha ya baadaye. Huu ni mchakato wa majadiliano ya kina unaopaswa kuendelezwa majimboni na parokiani, ili kuleta matumaini mapya. Vijana kwa njia ya ushuhuda wa maisha yao wanasukumwa kutangaza na kushuhudia Fumbo la Pasaka, yaani mateso, kifo na ufufuko wa Yesu.

Vijana wanapaswa kuwa waaminifu kwa Kristo na Kanisa lake kwa kutekekeza nyajibu zao kwa weledi na umakini mkubwa, huku wakiendelea kupata majiundo ya maisha na wito wa Kikristo katika maisha ya kiutu, kifamilia, kikazi na kisiasa. Ni mwaliko na changamoto ya kushikamana kidugu na maskini pamoja na kusimama kidete kupinga vitendo vyote vinavyosababisha uvunjifu wa haki.

Lengo kama anavyosema Baba Mtakatifu ni kuwaendelea wale wanaoishi pembezoni mwa jamii kwa kukazia mambo msingi katika maisha. Vijana waendelee kushirikiana na kuwajibika pamoja na viongozi wao wa Kanisa kama sehemu ya mchakato wa ujenzi wa Kanisa la Kristo. Hakuna haj aya kukata tamaa kutokana na mapungufu ya rasilimali na uwezo wa kukabiliana na matatizo pamoja na changamoto mbali mbali zinazojitokeza katika maisha; kama vile ukosefu wa fursa za ajira, magonjwa, vita, madhulumu na nyanyaso mbali mbali, bali kila mtu atekeleze wajibu wake kikamilifu, ili kuwasha tena cheche za matumaini kwa wale waliokata tamaa!

Kardinali Pietro Parolin anawataka vijana wakatoliki Italia kuendelea kuenzi kwa njia ya ushuhuda wa maisha yao mifano na mafundisho ya Watakatifu Yohane XXIII na Yohane Paulo II kwa kujikita katika ukweli, utakatifu wa maisha na furaha ya kweli; imani kwa Kristo na Kanisa lake pamoja na kujikita katika kweli za Kiinjili.







All the contents on this site are copyrighted ©.