2014-05-02 14:02:08

Mfuko wa Kipapa umechangia maendeleo ya watu duniani!


Baba Mtakatifu Francisko amewapongeza wajumbe wa Mfuko wa Papa waliomtembelea mjini Vatican, Ijumaa tarehe 2 Mei 2014, wakati huu Wakristo sehemu mbali mbali za dunia wanapoendelea kusherehekea ushindi wa Kristo dhidi ya dhambi na kifo pamoja na kupokea zawadi ya Roho Mtakatifu anayefanya yote kuwa mapya.

Baba Mtakatifu anawaombea furaha na amani ya kweli inayobubujika kutoka kwa Kristo mfufuka na kwamba, hija ya sala katika Makaburi ya Watakatifu na wafiadini viwawezeshe kuendelea kuwa waaminifu kwa Kristo na Kanisa lake. Baba Mtakatifu anasema, tangu kuanzishwa kwa Mfuko wa Kipapa, umesaidia kugharimia utume na maisha ya Kanisa kwa njia ya matendo ya huruma kadiri ya nia za Khalifa wa Mtakatifu Petro.

Baba Mtakatifu amewapongeza wajumbe wa Mfuko wa Kipapa kwa mchango wao katika maendeleo na ustawi wa Kanisa katika nchi zinazoendelea duniani. Mchango huu umekuwa ni msaada mkubwa katika huduma kwenye sekta ya elimu, miradi ya huduma, pamoja na kusaidia kugharimia majiundo kwa waamini walei, watawa na mapadre wanaosoma mjini Roma.

Kwa njia hii, Mfuko wa Kipapa umekuwa mstari wa mbele katika kunoa akili na mioyo ya vijana wa kizazi kipya kadiri ya kweli za Kiinjili na hekima inayobubujika kutoka katika Mafundisho Jamii ya Kanisa, kwa kukazia umoja na mshikamano ndani ya Kanisa kwa ajili ya huduma kwa binadamu wote.

Baba Mtakatifu anawatakia kheri na mafanikio mema, ili waendelee kuimarishwa katika neema ya ubatizo inayowasukuma kuwa kweli ni wamissionari wa Habari Njema ya Wokovu, wakati huu Mama Kanisa anapomwimbia Mwenyezi Mungu utenzi wa sifa na shukrani kwa watakatifu Yohane XXIII na Yohane Paulo II, ili wanapokutana na Yesu Mfufuka awe kweli ni chemchemi ya furaha yao ya ndani.







All the contents on this site are copyrighted ©.