2014-05-01 09:31:38

Watakatifu Yohane XXIII na Yohane Paulo II walikuwa ni watetezi wa wafanyakazi!


Maadhimisho ya Siku kuu ya Mtakatifu Yosefu mfanyakazi kwa Mwaka 2014 yanatajirishwa kwa namna ya pekee na uzoefu pamoja na mafundisho ya kina yaliyotolewa na Watakatifu Yohane XXIII na Yohane Paulo II, waliosimama kidete kulinda na kutetea utu na heshima ya binadamu, haki, amani, ustawi na maendeleo ya wengi. Hawa ni watakatifu waliotangazwa na Papa Francisko hivi karibuni hapa mjini Vatican.

Watakatifu hawa wameshuhudia mateso na mahangaiko ya wafanyakazi kutoka sehemu mbali mbali za dunia enzi ya maisha na utumishi wao kama Mapadre, Maaskofu na baadaye kama Mapapa. Hawakukata tamaa kuonesha umuhimu wa kutoa kipaumbele cha kwanza kwa utu na heshima ya binadamu kwa njia ya ushuhuda wa maisha yao wenyewe!

Ni ujumbe kutoka kwa Askofu mkuu Cesare Nosiglia wa Jimbo kuu la Torino, Italia katika maadhimisho ya Siku ya Wafanyakazi Duniani. Anasema, kuna haja ya waamini pamoja na watu wote wenye mapenzi mema kujikita katika kujenga, kulinda na kudumisha misingi ya haki katika maeneo ya kazi, ili kuamsha tena matumaini miongoni mwa wafanyakazi wanaoendelea kukata tamaa ya maisha bora kutokana na athari za myumbo wa uchumi kimataifa.

Askofu mkuu Nosiglia anawataka wafanyabiashara kuwekeza zaidi katika shughuli za uzalishaji mali na utoaji wa huduma, kama sehemu ya mchakato wa kutengeneza fursa za ajira hasa miongoni mwa vijana. Juhudi hizi hazina budi kwenda sanjari na urahisishaji wa huduma kwa kuondokana na ukiritimba usiokuwa na mashiko kwa ustawi na maendeleo ya wananchi.

Anawataka vijana kujenga matumaini kwa kuwekeza katika karama na vipaji walivyokirimiwa na Roho Mtakatifu ili kutengeneza fursa za ajira, kwa kushirikiana na kushikamana kwa pamoja, mwanadamu akipewa kipaumbele cha kwanza kabisa.

Vyama vya wafanyakazi, vishikamane kulinda na kutetea masilahi ya wafanyakazi, washirikiane na wafanyakazi pamoja na waajiri wao, ili kuleta tija na ufanisi mkubwa katika uzalishaji na utoaji wa huduma kwa jamii. Kuna haja ya kuwekeza katika mafunzo kazini, kwa kuthamini tunu msingi za maisha ya kifamilia pamoja na kutafuta suluhu ya matatizo na changamoto katika ulimwengu wa wafanyakazi kwa busara!

Wafanyakazi wajenge imani kwa Mungu na binadamu, waongeze mtazamo wao katika masuala ya kiulimwengu na kamwe wasijitafute wenyewe katika ubinafsi wao, kwani watajikuta wakitumbukia katika umaskini si tu wa kiuchumi bali hata pia umaskini wa kitamaduni. Woga na wasi wasi, hasira na chuki ni mambo yasiyokuwa na maendeleo katika shughuli za uzalishaji na utoaji wa huduma.

Askofu mkuu Cesare Nosiglia wa Jimbo kuu la Torino, anawataka wafanyakazi kuiga mfano wa maisha ya Mtakatifu Yosefu Mfanyakazi. Kanisa linakiri na kufundisha juu ya Neno wa Mungu aliyefanyika mwili, akawa sawa na binadamu, akafanya kazi, akateswa, akafa na kufufuka kutoka katika wafu na hivyo kufanya yote mapya!

Mtakatifu Yosefu Mfanyakazi na Watakatifu Yohane XXIII na Yohane Paulo II waendelee kuwaombea wafanyakazi sehemu mbali mbali za dunia ili watambue kwamba, kazi ni utimilifu wa utu na heshima ya binadamu inayomshikirisha pia katika kazi ya uumbaji kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya jamii inayowazunguka!







All the contents on this site are copyrighted ©.