2014-04-29 15:15:59

Shuhudieni uwepo wa Kristo Mfufuka kati yenu!


Baba Mtakatifu Francisko katika mahubiri yake kwenye Kikanisa cha Mtakatifu Martha, kilichoko mjini Vatican, Jumanne tarehe 29 Aprili 2014 amezungumzia juu ya Jumuiya ya kwanza ya waamini waliokuwa na roho moja na moyo mmoja katika mambo yote, hali iliyowawezesha kujenga amani na utulivu sanjari na kuendelea kutoa ushuhuda kwa Kristo mfufuka pamoja na kuwahudumia maskini na wahitaji.

Hawa ni watu waliozaliwa kwa maji na Roho na Roho Mtakatifu, wakawa ni mwili mmoja na roho moja; wakajenga amani, utulivu na msamaha kati yao. Hizi ndizo tunu msingi zinazopaswa kudumishwa na Jumuiya ya waamini, bila kuvurugwa na wivu usiokuwa na mashiko wala maendeleo kwa Watu wa Mungu; mambo yanyosababishwa na Shetani. Jumuiya bado inaendelea kujengwa na matatizo yatakuwepo, kwani haya ni mapambano yanayojikita katika mafundisho na Mapokeo pamoja na kuwania madaraka.

Jumuiya ya kwanza ya Wakristo ilisimikwa na kuwezeshwa na Roho Mtakatifu, ikajipambanua kwa mshikamano wa udugu na upendo; ikawa ni kielelezo cha ushuhuda wa imani tendaji, changamoto na mwaliko kwa Jumuiya za Kikristo kujipima kwa wakati huu, ikiwa kama: Jumuiya, Parokia au Majimbo haya yanatoa ushuhuda wa kweli wa Yesu Kristo mfufuka, anayeendelea kuwa kati ya watu wake.

Jumuiya za Kikristo hazina budi kujielekeza kwa njia ya huduma makini kwa maskini na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii, ili kuwaonjesha huruma na upendo unaobubujika kutoka kwa Kristo na Kanisa lake. Huu ni ushuhuda amini wa uwepo wa Roho Mtakatifu anayetenda kazi ndani ya Kanisa, pamoja na kulichangamotisha kujenga na kuimarisha umoja na mshikamano wa dhati.

Mwishoni, Baba Mtakatifu anawaomba waamini kumwomba Roho Mtakatifu awasaidie kutembea katika njia hii kwa kuonesha ile nguvu waliyoipata kutokana na Ubatizo katika maji na Roho Mtakatifu.







All the contents on this site are copyrighted ©.