Mbinu mkakati wa mapambano dhidi ya baa la njaa duniani
Jumuiya ya kimataifa na wadau mbali mbali hawana budi kujifunga kibwebwe ili kuheshimu,
kulinda, kuhamasisha na kutekeleza dhamana ya haki ya chakula kwa wote, ili kupunguza
idadi ya watu wanaokufa na baa la njaa duniani wakati kuna chakula kingi kinazalishwa
lakini kinatupwa kama taka! Watu wana haki ya kupata lishe bora, kuishi katika mazingira
bora kadiri ya mazingira yao.
Ni kweli
kwamba, Jumuiya ya Kimataifa imefanya maendeleo makubwa katika mchakato wa upatikanaji
wa chakula duniani tangu mara baada ya Vita kuu ya pili wa dunia, lakini baa la njaa
bado lina waandama watu wengi zaidi duniani, kwani takwimu zinaonesha kwamba, kuna
watu million 840 wanaoteseka na baa la njaa duniani, wengi wao ni wale wanaotoka katika
Nchi zinazoendelea duniani.
Watu hawa wanakabiliwa na kifo kinachoendelea
kukwapua maisha ya watu pole pole kutokana na utapiamlo wa kutisha, hali ambayo inawanyima
watoto fursa ya kukua na kukomaa pamoja na kujipatia maendeleo katika sekta mbali
mbali za maisha. Baba Mtakatifu Francisko anasema, hii ni kashfa kubwa kwa Jumuiya
ya Kimataifa.
Ni mchango uliotolewa hivi karibuni na Askofu mkuu Silvano Maria
Tomasi, Mwakilishi wa kudumu wa Vatican kwenye Ofisi za Umoja wa Mataifa zenye makao
makuu mjini Geneva , wakati alipokuwa anachangia kwenye mkutano wa Baraza la haki
msingi za binadamu la Umoja wa Mataifa. Baba Mtakatifu Francisko anasema, utapiamlo
wa kutisha na baa la njaa kamwe yasigeuzwe kuwa ni mambo ya kawaida katika maisha
ya mwanadamu. Kuna haja kwa Jumuiya ya Kimataifa kuweka mikakati madhubuti kisheria,
itakayowezesha kuunda sera makini za haki ya chakula, udhibiti na ugavi wa rasilimali
katika mapambano ya baa la njaa.
Askofu mkuu Silvano Maria Tomasi anasema,
Jumuiya ya Kimataifa haina budi kuzingatia madhara yanayotokana na baa la njaa kama
yanayopembuliwa na takwimu mbali mbali zinazooneshwa na Jumuiya ya Kimataifa; uzalishaji
na ugavi wa chakula pamoja na kuzijengea Familia uwezo wa kununua chakula kwa bei
nafuu. Ili kuweza kupata mafanikio katika mikakati hii kuna haja ya kubadili mfumo
wa maisha, kuondokana na ubinafsi, kuguswa na mateso pamoja na mahangaiko ya wengine,
kwa kuwa na uchu wa kupata faida kubwa.
Haki ya chakula inaweza kupatikana
ikiwa kama Jumuiya ya Kimataifa itajenga na kudumisha mshikamano wa kidugu pamoja
na kuwajengea uwezo wakulima wadogo wadogo ili waweze kuongeza tija na uzalishaji
katika mazao ya biashara na chakula. Wanawake katika nchi zinazoendelea ni wadau wakuu
wa shughuli za kilimo na uzalishaji, kumbe, kuna haja kwa Jumuiya ya Kimataifa kuwawezesha
wanawake kutekeleza dhamana hii kikamilifu zaidi. Msaada kwa wakulima hauna budi kuwashirikisha
wadau wote kwa kuwalinda na kuwapatia haki ya kuzalisha na soko la uhakika wa mazao
yao bila ya ubaguzi ambao mara nyingi unafanywa na Mataifa makubwa.
Askofu
mkuu Silvano Maria Tomasi anasema mshikamano wa kimataifa ni nyenzo msingi katika
mapambano ya kuwa na haki ya chakula duniani pamoja na kukabiliana na majanga ya maisha
yanayoibuka kila kukicha. Maadhimisho ya Mwaka wa Familia ya Wakulima Kimataifa iwe
ni fursa ya kuhakikisha kwamba, haki ya chakula inapatikana kwa wote, kwa njia ya
majiundo makini ya mshikamano kimataifa. Ni changamoto ya kuondokana na utamaduni
wa utandawazi usioguswa wala kujali mahangaiko ya watu wengine, bali utu na heshima
ya binadamu vipewe kipaumbele cha kwanza.
Imeandaliwa na Padre Richard
A. Mjigwa, C.PP.S. Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.