2014-04-28 10:11:41

Cheche za maisha ya utakatifu!


Kardinali Polycarp Pengo, Askofu mkuu wa Jimbo kuu la Dar es Salaam, alikuwa ni kati ya Watu wa Mungu waliohudhuria katika Ibada ya Misa Takatifu ya kuwatangaza Wenyeheri Yohane XXIII na Yohane Paulo II kuwa ni Watakatifu, Ibada iliyoongozwa na Baba Mtakatifu Francisko, kwenye Uwanja wa Kanisa kuu la Mtakatifu Petro mjini Vatican, Jumapili ya huruma ya Mungu, tarehe 27 Aprili 2014. RealAudioMP3

Kardinali Pengo katika mahojiano maalum na Radio Vatican anakiri kwamba, bado kuna watu wana imani kuhusu uwepo wa Mungu na utakatifu wa maisha ya viongozi wa Kanisa, kama ilivyojidhihirisha kwenye kesha na hatimaye maadhimisho ya Siku kuu ya Imani kwa ajili ya kuwatangaza Wenyeheri Yohane XXIII na Yohane Paulo II kuwa ni watakatifu.

Kardinali Pengo anasema, licha ya afya yake kuwa si nzuri kwa siku za hivi karibuni lakini ameona kwamba, ni jambo la muhimu kuweza kuhudhuria katika tukio hili la kihistoria ambalo linamgusa kama mwamini binafsi na Kanisa la Tanzania na Kanisa la Kiulimwengu katika ujumla wake. Mtakatifu Yohane XXIII anakumbukwa na watanzania kwa kuwaandikia Sala ya kuombea Tanzania na kwa kuwapatia Kardinali wa kwanza Mwafrika. Ni kiongozi aliyethubutu kwa ujasiri mkubwa kuitisha maadhimisho ya Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican, ili kuleta mabadiliko katika maisha na utume wa Kanisa.

Mtakatifu Yohane XXIII alianza utume wake wakati watu wamekata tamaa kutokana na mateso pamoja na mahangaiko ya Vita kuu ya Pili ya Dunia, kiasi kwamba, watu wakapoteza imani. Kitendo cha kuitisha Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican, ni kielelezo cha utakatifu na ushujaa wa imani hasa kutokana na mazingira na hali iliyokuwepo kwa wakati ule. Mtakatifu Yohane XXIII alilitaka Kanisa kujikita katika mchakato wa kufanya upya, "aggiornamento", ili kurekebisha mambo na kusonga mbele kwa imani na matumaini pasi na kukata tamaa.

Kardinali Pengo anasema kwamba, dhambi inawakatisha watu tamaa, lakini kwa njia ya imani thabiti, watu wanaweza kupiga moyo konde na kuanza tena safari ya maisha yao, kwa kutambua kwamba, daima kuna fursa ya kuweza kuanza upya na kufanya marekebisho makubwa katika maisha, hizi ni cheche za utakatifu wa maisha. Kufanya mambo mapya ni mwaliko kwa wa kupiga hatua ya kutenda mema zaidi. Mtakatifu Yohane XXIII anakumbukwa na wengi kama "Baba Mtakatifu mwema", hali inayodhihirisha madai ya kubadilika ili kufikia utakatifu wa maisha!







All the contents on this site are copyrighted ©.