Mama Helen Moshi ni kati ya maelfu ya mahujaji kutoka ndani na nje ya Italia waliofika
mjini Vatican kushuhudia Wenyeheri Yohane XXIII na Yohane Paulo II wakitangazwa kuwa
ni Watakatifu, tukio la kihistoria ambalo halijawahi kutokea ndani ya Kanisa. Hii
ni siku inayoonesha matendo makuu ya Mungu katika hija ya imani ya watu wake anasema
Mama Helen ambaye ni mwamini kutoka Jimbo kuu la Dar es Salaa, Tanzania.
Papa Yohane
Paulo II amejipambanua kwa kuwa ni mchungaji mkuu wa Kanisa aliyekazia maisha na utume
wa kimissionari, akasiamam kidete kulinda na kutetea zawadi ya uhai, akawaonesha vijana
kwamba, Kristo ndio tumaini lao la daima na kwamba, msamaha wa kweli unaweza kupatanika
kwa njia ya majadiliano yanayosimikwa katika ukweli wa maisha. Alikuwa ni mpole na
mkarimu na kwamba, amejionesha kuwa ni mtu wa watu kutokana na maisha pamoja na utume
wake kugusa watu wengi duniani.
Mama Helen Moshi anasema, kilichomgusa kwa
namna ya pekee katika maisha na utume wa Papa Yohane Paulo II ni imani thabiti hata
katika mateso na mahangaiko ya magonjwa na maisha. Ni mtu aliyekuwa na matumaini thabiti,
kiasi hata cha kujiachilia mikononi mwa Bikira Maria, ndiyo maana alikuwa na Ibada
kubwa kwa Mama wa Mungu na Kanisa, mfano wa kuigwa katika maisha ya utakatifu.