Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto wa kumi na sita, alipoingia kwenye Uwanja wa Kanisa
kuu la Mtakatifu Petro kushiriki katika Ibada ya Misa Takatifu ya kuwatangaza Wenyeheri
Yohane XXIII na Yohane Paulo II kuwa watakatifu amepokelewa kwa vigelegele na shangwe
kubwa kutoka kwa waamini waliokuwa wamefurika kwenye Uwanja wa Kanisa kuu la Mtakatifu
Petro pamoja na viunga vyake. Baba Mtakatifu mstaafu amesalimiana na baadhi ya Makardinali
na viongozi wa Serikali waliokuwa karibu naye.
Kelele za furaha zilisikika
pale Baba Mtakatifu Francisko walipokumbatiana na kusalimiana na Baba Mtakatifu mstaafu
Benedikto XVI. Kwa mara ya kwanza katika historia ya Kanisa Katoliki, kuwatangaza
Mapapa wawili kuwa watakatifu katika Ibada ambayo imehudhuriwa na Mapapa wawili, mmoja
akiwa ameng'atuka kutoka madarakani na mwingine akiwa bado anaendelea kuliongoza Kanisa
la Kristo. Itakumbukwa kwamba, Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto XVI ana historia kubwa
na uhusiano wa pekee kabisa na Watakatifu Yohane XXIII na Yohane Paulo II.
Baba
Mtakatifu Francisko mara baada ya maadhimisho ya Ibada ya Misa Takatifu, amekwenda
moja kwa moja kumsalimia na kumshukuru Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto wa kumi na
sita, kwa kuhudhuria katika Ibada ya Misa Takatifu kwa ajili ya kuwatangaza Wenyeheri
Yohane XXIII na Yohane Paulo II kuwa Watakatifu. Baba Mtakatifu pia alipata fursa
ya kuzungumza na viongozi mbali mbali waliohudhuria kwenye Ibada hii.